2012-12-20 08:02:07

Familia ni kitalu cha miito mitakatifu, kamwe waamini wasiwe ni kikwazo cha Mapadre wakaanguka na kugeuka kuwa mnara wa chumvi!


Askofu mkuu Yuda Thadeus Ruwaichi wa Jimbo Kuu la Mwanza, Tanzania katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, ametusaidia kutafakari kuhusu utume wa Nabii, dhamana na wito wa kipadre, leo katika makala haya anapembua utume wa Familia ya Kikristo katika kulea, kukuza na kuimarisha wito wa Kipadre. RealAudioMP3

Askofu mkuu Ruwaichi anasema kwamba, Padre ni baba wa Kanisa. Wazazi baada ya kuhangaika naye katika malezi na majiundo na hatimaye kulikabidhi Kanisa, wanapaswa kumruhusu mtoto wao ili aweze kuijenga nyumba yake, yaani Kanisa analokabidhiwa na kamwe huu usiwe ni mradi binafsi au kitega uchumi kwa Familia, Ndugu, Jamaa na Marafiki, vinginevyo atakuwa ni Padre asiye na raha na amani; asiye aminika wale kuheshimika kwani watu wengi watadhani kwamba, anatumia Kanisa kwa ajili ya kuwafaidisha ndugu zake tu!

Wazazi wanapaswa kutambua kwamba, mwana wao ni Padre wa Kanisa lote: Moja, Takatifu, Katoliki na la Mitume. Idadi ya Mapadre inayoongezeka kila mwaka majimboni inuie kukuza ubora na thamani na ufuasi wa Kristo; wakipania kumtangaza Kristo kwa njia bora zaidi, mpya, hai na endelevu. Ni wajibu wa Familia ya Mungu kuendelea kusali kwa ajili ya kuombea miitomitakatifu ndani ya Kanisa, ili Kristo aweze kujipatia vijana wachapakazi, wachamungu na hodari, tayari kujitoa kimaso maso, kumtangaza, kumpenda Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu.

Askofu mkuu Ruwaichi anazitaka Familia kuweka nia wazi na thabiti ya kuboresha vitalu vya miito mitakatifu, kwani kila kuhani ni tunda la Familia. Miito mizuri na dumifu ni matokeo ya Familia imara, zenye imani thabiti, mshikamano, amani na upendo. Ni Familia ambazo ziko tayari kurithisha imani na kulea maadili bora, kwa kutambua kwamba, Familia ni kitalu cha kuzalisha miito mitakatifu na kamwe waamini walei wasiwe ni kikwazo cha kuanguka kwa Mapadre kwa kuwafanya wageuke na kuwa ni minara ya chumvi!

Askofu mkuu Ruwaichi anawakumbusha Mapadre kwamba, wanapoitikia wito kutoka kwa Mungu, wafanye hivyo kwa nia safi na wawe tayari kuitikia kila siku ya maisha yao; katika raha, na furaha; magumu na shida na kamwe wasijutie kuwa Mapadre, bali wawe imara na watakatifu!







All the contents on this site are copyrighted ©.