Salam za Noel kutoka kwa Baba Mtakatifu Benedikto XVI kwa watoto wagonjwa waliolazwa
katika Hospitali ya Bambino Gesù
Kardinali Tarcisio Bertone, katibu mkuu wa Vatican, Jumanne tarehe 18 Desemba 2012
alitembelea Hospitali ya Bambino Gesù, inayomilikiwa na kuendeshwa na Vatican ili
kuwasalimia watoto wagonjwa waliolazwa Hospitalini hapo pamoja na kuwashirikisha salam
na matashi mema ya Siku kuu ya Noeli kutoka kwa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na
sita.
Amewapongeza na kuwashukuru wafanyakazi wa Hospitali ya Bambino Gesu
kutokana na kuunganisha kwa umakini mkubwa huduma na weledi katika kuwatibu watoto
wanaolazwa Hospitalini hapo, hali inayoonesha mshikamano wa dhati miongoni mwa wafanyakazi
katika vitengo mbali mbali Hospitalini hapo.
Anasema, Baba Mtakatifu Benedikto
wa kumi na sita, anafuatilia kwa umakini mkubwa huduma mbali mbali zinazotolewa Hospitalini
hapo na anawapongeza kwa kufungua tawi jipya la Hospitali ya Bambino Gesù, kwenye
eneo la Kanisa kuu la Mtakatifu Paulo Nje ya kuta za Roma; kituo ambacho kimepewa
jina la Benedikto XVI na kitatumika kwa ajili ya kutoa tiba sanjari na kufanya tafiti.
Kardinali
Bertone amefurahi kukutana na watoto wagonjwa wanaotibiwa Hospitalini hapo wakifurahia
huduma na tiba, jambo ambalo linapaswa kupewa kipaumbele cha pekee kwa kila mtoto.
Bado Jumuiya ya Kimataifa imeshikwa na bumbuwazi kutokana na mauaji ya kinyama waliofanyiwa
watoto wa mjini Connencticut, nchini Marekani hivi karibuni. Masikitiko kutokana na
mauaji ya watoto hao yamegeuka kuwa ni sala kwa kila mtu, lakini hasa wale waliopewa
dhamana ya kuhakikisha ulinzi na usalama wa raia wanatekeleza wajibu wao kikamilifu
kwa kulinda maisha ya watoto.
Ili mtoto aweze kukua na kukomaa barabara anahitaji
kuonjeshwa furaha na amani, mambo ambayo yanapaswa kuanzia ndani ya familia yenyewe.
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anabainisha kwamba, mtoto anahitaji kuonja
uwepo wa karibu na matumaini yanayobubujika kutoka katika upendo; haya ndiyo mang'amuzi
ya kwanza kabisa ambayo watoto wanapaswa kuyaonja anasema Kardinali Bertone.
Watoto
wanapaswa kusaidiwa kupata majibu ya maswali yao ambayo bado yanaelea angani, kwani
wana hamu ya kufahamu na kuelewa; utume unaotekelezwa shuleni na ndani ya Familia.
Watoto hawa wafahamishwe na kueleweshwa maana ya mateso wanayokabiliana nayo. Huu
ni wajibu wa wazazi na walezi kuwasaidia kufahamu undani wa maisha haya ili waweze
kujifunza kupenda.
Kardinali Bertone anasema, Siku kuu ya Noeli liwe ni tukio
jipya linaonesha utashi na ukarimu wa Mwenyezi Mungu kwa ajili ya binadamu; anayependa
kila kiumbe chake sanjari na kumweka Kristo kuwa ni kiini cha historia ya mwanadamu
yaani: Kabla na Baada ya kuzaliwa kwa Kristo; Yeye ni Alfa na Omega, Mwanzo na Mwisho,
Nyakati zote ni zake; changamoto ya kuuvua utu wa kale unaogubikwa katika ubinafsi
na badala yake kujivika utu mpya na kuanza kutembea katika ukweli na nyakati mpya
za uwepo wa Kristo.