2012-12-19 07:25:34

Mwaka wa Imani: Wongofu wa ndani, Kanisa na Imani ni maneno yanayopaswa kupewa uzito unaostahili!


Askofu mkuu Francis Joseph Chaput, wa Jimbo kuu la Philadelphia, Marekani, anabainisha kwamba, Wongofu wa ndani, Kanisa na Imani ni maneno ambayo yanapaswa kupewa uzito unaostahili katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani. RealAudioMP3

Ni mwaliko kwa waamini kuchuchumilia wongofu wa ndani kama sehemu muhimu sana ya utekelezaji wa utume wake katika ulimwengu mamboleo. Kila mwamini anaalikwa kuwa mtakatifu, wito na mwaliko kwa kwanza kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Mwamini mwenye Imani thabiti hawezi kuyumbishwa na kinzani na migogoro inayoletwa na maendeleo ya sayansi na teknolojia au kwa watu kupenda kukumbatia mawazo mepesi mepesi hata katika maisha ya ndoa na familia. Wanandoa wanapaswa kumwongokea Mwenyezi Mungu, daima wakisaidiana katika hija ya maisha yao ya ndoa, ili kwa pamoja waweze kufikia utakatifu wa maisha. Hizi ni juhudi zinazohitaji kuimarishana katika imani, mapendo na matumaini.

Askofu mkuu Chaput anasema kwamba, kuna wakati katika historia ya Kanisa, waamini waliyachukulia maisha na utume wa Kanisa kama jambo la kawaida na kuyafanya kuwa ni sehemu ya mazoea, kiasi hata cha kupoteza dhamana na utume wake katika Ulimwengu. Ndivyo inavyoweza kutokea hata katika maisha ya wanandoa, pale wanapodhani kwamba, maisha yao ni jambo la kawaida na hakuna jipya, basi hapo wanaweza kuanguka katika utupu na hali ya mazoea.

Kwa njia ya toba na wongofu wa ndani, Mwenyezi Mungu ameweza kulijalia Kanisa Watakatifu ambao wamekuwa ni chachu ya wongofu na utakatifu wa maisha kwa mamillioni ya waamini. Baadhi yao ni: Mtakatifu Bernardo, Mtakatifu Francisco wa Assisi, Theresa wa Avila na Katarina wa Siena. Ni watakatifu waliolisaidia Kanisa kutubu na kuongoka, likaanza tena kuchuchumilia hija ya utakatifu katika maisha na utume wake. Ni watu ambao waliwasha moto wa imani na matumaini mintarafu dhamira ya Kristo mwenyewe.

Hali kama hii inaendelea kujidhihirisha kwa namna ya pekee kabisa kwa njia ya Vyama vya kitume ambavyo vimeibuka mara baada ya Maadhimisho ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican. Ni vyama ambavyo vinajikita katika kusoma, kutafakari na kumwilisha Injili ya Mapendo. Vyama hivi ni kielelezo cha neema na huruma ya Mungu kwa Kanisa lake. Kumbe, hakuna haja ya kuwa na wasi wasi wa uwepo wa Vyama vya Kitume ndani ya Kanisa, bali kila Chama kitekeleze wajibu na dhamana yake, daima kikijitahidi kudumisha umoja, upendo na mshikamano na Familia ya Mungu katika eneo husika.

Mama Kanisa daima yuko katika hija ya toba na wongofu wa ndani, ili aweze kuendelea kuwa ni mwaminifu kwa Mungu na Kwa Kristo mchumba wake. Ikumbukwe kwamba, Kanisa ni Jumuiya ya Waamini wanaomfuasa Kristo. Ni Mama na Mwalimu; Kiongozi na Mfariji wa wote wanaoteseka kiroho na kimwili. Kanisa ni mchumba amini wa Kristo na kwamba ni mali ya Kristo ambaye amewakabidhi binadamu wenye karama na mapungufu yao kuliongoza. Kanisa linaendelea kufuata msingi wa Kweli za Kiinjili uliowekwa bayana na Kristo mwenyewe kwa njia ya Neno la Mungu na Mapokeo hai.

Waamini wanakumbushwa kwamba, hawawezi kamwe kuwa na Mungu kama Baba yao bila kuwa na Kanisa kama Mama yao, kama alivyosema Mtakatifu Cypriani; kila mwamini anapaswa kujisikia kuwa ni sehemu ya Kanisa. Kanisa halina budi kuwa ni sehemu ya maisha na utume wa kila mwamini; mahali ambapo wanashibishwa na Neno la Mungu, Maisha ya Kisakramenti na Katekesi ya kina.

Kanisa ni uwanja ambapo waamini kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao wanatangaza kwa ujasiri mkubwa Injili ya Upendo unaoonesha Imani wanayokiri kwa vinywa vyao, Imani wanayoiadhimisha kwa njia ya Sakramenti za Kanisa; Imani wanaojitahidi kuimwlisha kwa kufuata Amri za Mungu ambazo ni dira na mwongozo wa maisha adili na matakatifu.

Utume ni mwanzo na kilele cha maisha ya Kanisa linaloendelea kutekeleza kwa dhati kabisa ile Amri ya Kristo, nendeni ulimwenguni kote mkawafanye watu wote kuwa ni wanafunzi wangu. Huu ni ujumbe ambao unamgusa kila mfuasi wa Kristo tangu wale wa Kanisa la Mwanzo hadi leo hii katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.

Utume wa Kanisa unapata chimbuko lake kutoka katika Fumbo la Utatu Mtakatifu. Waamini kwa pamoja, wanachangamotishwa na Mama Kanisa kushiriki katika kazi ya Ukombozi iliyoanzishwa na Kristo mwenyewe yapata miaka elfu mbili ya ukristo, wakitambua kwamba, Yesu mwenyewe yuko pamoja nao hadi utimilifu wa dahali, jambo la msingi ni kuhakikisha kwamba, Imani yao kwa Kristo inaendelea kuwa hai daima.

Askofu mkuu Chaput anakumbusha kwamba, Imani kimsingi ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu, kumbe mwamini ana uhuru kamili wa kuipokea na kuifanyia kazi au kuikataa na hatimaye, kumezwa na malimwengu. Mwenyezi Mungu ndiye anayejitaabisha kukutana na mwamini kwa njia ya Yesu Kristo na Kanisa lake, ndiyo maana waamini wanayo haki ya kuendelea kumtumainia Yesu Kristo Mkombozi wa dunia. Imani ni jiwe kuu katika maisha ya mwamini, lakini Imani bila matendo hiyo inakufa na kunyauka.








All the contents on this site are copyrighted ©.