2012-12-18 15:00:20

Maadhimisho ya Mwaka wa Imani Barani Asia


Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Asia, katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani, linalenga kuwasaidia waamini kumwilisha Imani yao kwa Kristo na Kanisa lake katika medani mbali mbali za maisha; wakitambua kwamba, wanakabiliana na changamoto ya kumwilisha Imani hii kwa njia ya majadiliano ya kidini na kiekumene; daima wakiwa wameshikamana katika kutafuta ukweli.

Maadhimisho ya Mwaka wa Imani Barani Asia, yanakwenda sanjari na changamoto mbali mbali zilizoibuliwa wakati wa maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya sanjari na Jubilee ya miaka hamsini ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican. Bara la Asia ni kubwa na kila nchi ina vipaumbele vyake; lakini kwa pamoja wanaunganishwa na dhamana ya kuendeleza majadiliano ya kidini na waamini wa dini ya Kiislam, ambao katika kipindi cha miaka ya hivi karibuni, kumekuwepo na kinzani kubwa pamoja na madhulumu ya kidini.

Dhamana ya pili ni kujenga utamaduni wa kutafuta haki, amani na upatanisho wa kweli kwa kutambua tofauti za kidini, kiimani na kitamaduni zinazojitokeza kati yao na kwamba, huu ni utajiri mkubwa unaoweza kutumiwa kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano wa kitaifa, kwa kutafuta mafao ya wengi.

Maaskofu Katoliki Barani Asia, wanatambua na kuthamini maendeleo makubwa yanayojionesha katika sekta ya sayansi na ukuaji wa uchumi. Wanasema ni wajibu wao kusaidia Jamii kuhakikisha kwamba, maendeleo haya yanakumbatia pia misingi ya maadili na utu wema, Mwenyezi Mungu akipewa pia kipaumbele cha kwanza, vinginevyo, watu wengi watajikuta wanatumbukizwa katika ombwe na utupu! Matokeo yake ni kudhalilisha utu na heshima ya binadamu pamoja na kuongezeka kwa baa la umaskini.

Maendeleo ya kiuchumi, yajengeke katika misingi ya: ukweli, uwazi, uaminifu pamoja na uwajibikaji fungamanishi; daima wanasiasa na watunga sera wakijitahidi kutafuta mafao ya wengi kwa kutoa huduma makini na endelevu inayogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Vijana wajengewe misingi bora ya elimu, itakayowawezesha kupambana vyema na mazingira, ili kuzifanya nchi zao kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi. Maendeleo ya sayansi na teknolojia, kimsingi hayakinzani na imani, bali yanategemeana. Ni matumaini ya Maaskofu wa Asia kwamba, waamini wataweza kutolea ushuhuda wa imani yao kwa njia ya maisha adili na aminifu yanayojikita katika Kweli za Kiinjili.










All the contents on this site are copyrighted ©.