Amri kumi zinazolenga kuleta tija na maboresho katika sekta ya kilimo nchini Tanzania
Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amefanya ziara ya ghafla kwa kukagua mashamba
ya viongozi wa mkoa wa Katavi kwa kuanza na shamba la Mkuu wa Mkoa huo, Dk. Rajab
Rutengwe. Pia alikagua shamba la na Katibu Tawala wa Mkoa, Mhandisi Emmanuel Kalobelo.
Mashamba yote mawili yako katika kijiji cha Songambele eneo la tankifupi, kata ya
Nsimbo, wilayani Mlele, mkoani Katavi.
Shamba la Mkuu wa Mkoa lenye ukubwa
wa ekari tano lilikuwa limepandwa mahindi na linatumika kama shamba darasa wakati
lile la Katibu Tawala wa Mkoa lenye ukubwa wa ekari nne na nusu lilikuwa limepandwa
mahindi na miembe ya kisasa. Pia kulikuwa na banda la ng’ombe. Waziri Mkuu alichukua
uamuzi huo Jumatatu, Desemba 17, 2012 mara baada ya kuzungumza na wakazi wa kijiji
cha Songambele kwenye kata ya Nsimbo na kuwatangazia amri 10 za kuendeleza mkoa huo
na wilaya yao mpya.
Waziri Mkuu ambaye alikuwa katika siku ya tano ya ziara
yake jimboni kwake Katavi wilayani Mlele, mkoani Katavi alisema amelazimika kuandaa
amri hizo 10 kwa sababu anatambua kwamba kila mtu anahitaji kula chakula bila kujali
kama mtu huyo ni kiongozi wa ngazi ya juu, mwananchi wa kawaida au ni kiongozi wa
dini. “Tumbo halijali wewe ni Waziri Mkuu, mwalimu, Mkuu wa Mkoa au Askofu, njaa ikiuma
linataka kulishwa. Kama kila mtu anahitaji kula, basi ni lazima kila mtu alime. Tutakaowasamehe
ni watoto, wazee na wagonjwa,” alisema.
Akifafanua kuhusu wale wenye ulemavu,
Waziri Mkuu alisema: “Wako walemavu ambao wanaweza kulima, nao pia walime.” Alisema
yeye ameandaa amri 10 za kuharakisha maendeleo ya mkoa na kuzitaja kuwa ni: Kila mtu
lazima ale; kila mtu lazima aondokane na umaskini; kila mtu mwenye uwezo wa kufanya
kazi ni lazima alime; kila mtu awe na ekari moja ifikapo mwaka 2013 na maandalizi
ya shamba yaanze mapema.
“Ekari hizi mojamoja ziwe zinaongezeka kila mwaka
ekari moja, yaani mwaka 2014 mtu awe na ekari mbili na mwaka 2015 awe na ekari tatu,
mkifanya hivyo mtaona matunda yake,” aliongeza. Akitaja amri nyingine, Waziri Mkuu
alisema kila ekari itakayolimwa ni lazima iwe imepimwa kitaalam kwamba ina ukubwa
wa hatua 70 kwa 70; ekari hiyo ilimwe kwa sesa na siyo matuta; ekari hiyo ipandwe
kwa kutumia mbegu bora, kwa mistari na kwa nafasi wanazoelekeza wataalamu.
“Ni
lazima ekari moja ikupe miche 16,000 ya mahindi. Nalisema hili kwa uchungu kwa sababu
nimetembea hapa nchini na nje ya nchi na kuona jinsi wenzetu walivyoendelea kutokana
na kilimo,” alisema. “Panda ekari yako kutumia mbolea ya Minjingu mazao sababu yenyewe
haihitaji kuongeza mbolea ya kukuzia na tena panda kwa mstari kwa kutumia kamba,”
alisisitiza huku akitumia lugha za Kiswahili, Kifipa na Kipimbwe.
Akitaja amri
ya nane, Waziri Mkuu alisema ni lazima palizi ifanyike kwa wakati. Alisema wanapaswa
kuvuna kwa wakati na kuhifadhi ghalani mazao yao. “Siku hizi mahindi hayakai ghalani,
bali yanaishia kwenye magunia, hii hapana, haifai.” Akitaja amri ya 10, Waziri Mkuu
alizitaka Halmashauri za Mkoa huo, kila kijiji kuhakikisha wanatunga sheria ndogondogo
za kuwasaidia wananchi kutekeleza amri hizo. Aliwataka viongozi wa Chama cha Mapinduzi
(CCM) mkoani humo wawe wakulima kwanza ndipo waisimamie Serikali kuona kama inatekeleza
yale iliyoyazimia.