2012-12-17 10:22:23

Parokia iwe ni mahali pa kusikiliza na kutafakari Neno la Mungu; Maadhimisho ya Sakramenti za Kanisa na Majiundo endelevu katika Imani


Kipindi cha Majilio ni wakati muafaka kwa waamini kutubu na kuongoka, tayari kumpokea Mwana wa Mungu anayezaliwa kati yao. Kanisa linamngoja Mkombozi wa dunia kwa moyo wa furaha; mwaliko wa pekee katika Liturujia ya Neno la Mungu, Jumapili ya tatu ya Kipindi cha Majilio.

Hii ndiyo furaha iliyooneshwa kwa namna ya pekee na Bikira Maria alipopashwa habari kwamba, atakuwa ni Mama wa Mungu.Hakuna sababu ya kuhuzunika wala kukata tamaa kwani uwepo wa Yesu Kristo Mkombozi wa Ulimwengu unaleta vijito vya furaha katika maisha ya waamini.

Ni maneno ya Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, wakati wa mahubiri yake aliyoyatoa kwenye Parokia ya Mtakatifu Patrizio, iliyoko nje kidogo ya Mji wa Roma, wakati wa ziara yake ya kichungaji, Jumapili iliyopita, tarehe 16 Desemba 2012. Waamini wanapaswa kutambua kwamba, kweli Mungu yuko pamoja nao na wala hayuko mbali; anajionesha katika Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu na katika Uhai wa Kanisa. Mwaliko ni kwa kila mwamini kuhakikisha kwamba, anakuwa ni mjumbe wa uwepo endelevu wa Mungu katika ulimwengu na kwa njia hii, wataweza kupata furaha inayobubujika kutoka kwa Mungu mwenyewe!

Baba Mtakatifu anasema, hakuna jambo lolote linaloweza kuwatenganisha waamini na upendo wa Kristo, ikiwa kama watajitenga na dhambi na daima wawe wapesi kukimbilia huruma na upendo wa Mungu katika Sakramenti ya Upatanisho. Anawaalika waamini kusali kwa bidii kwani Mungu anawasikiliza, anawafahamu na anawatekelezea maombi yao, hata kama si kama vile walivyoomba. Furaha inayobubujika kutoka kwa Mwenyezi Mungu ikutane na upendo wa binadamu unaopania kutekeleza mapenzi yake kwa moyo wa ukarimu na kamwe ubinafsi usipate nafasi.

Yohane Mbatizaji aliyetambua dhamana na utume wake wa kumwandalia Yesu Njia, anawaonesha wafuasi wa Kristo namna ya kumfuasa kwa ujasiri na uaminifu mkuu wakiwa tayari kubadili maisha yao, ili kukutana na Kristo anayebatiza kwa Maji na Roho Mtakatifu ili kusafisha maisha ya watu wake na hatimaye, kujenga umoja na kuendelea kufurahia amani na utulivu hata nyakati za magumu na udhaifu wa kibinadamu.

Baba Mtakatifu amewashukuru na kuwapongeza wadau mbali mbali wanaojitoa kimasomaso kwa ajili ya Uinjilishaji mpya Parokiani hapo. Anawapongeza watoto ambao wanajiandaa kwa ajili ya kupokea Sakramenti ya Ekaristi Takatifu pamoja na kuimarishwa kwa Kipaimara, kielelezo makini cha uhai wa Kanisa. Parokia hii iliyozinduliwa kunako mwaka 2007 iwe ni mahali pa kusikiliza Neno la Mungu, kuadhimisha Sakramenti za Kanisa na kujichotea nguvu na neema katika hija ya maisha, daima wajikitahidi kujenga na kuimarisha umoja, upendo na mshikamano wa dhati.

Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu kiwe ni kiini cha maisha ya mwamini binafsi na Jumuiya; changamoto ya kuendelea kutambua umuhimu wa Jumapili kuwa ni Siku ya Mungu, Siku ya Kristo, Siku ya Kanisa na Siku ya Mwanadamu; inayowapatia fursa ya kuadhimisha Fumbo la Mateso, Kifo na Ufufuko wa Kristo. Waamini waonje huruma na upendo wa Mungu kwa njia ya sakramenti ya Upatanisho.

Baba Mtakatifu anasema, Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, iwe ni fursa ya kujikita katika Katekesi ya kina, kwa kujifunza Kanuni ya Imani, kama njia ya kukutana na Mungu aliye hai katika hija ya maisha yao ya kila siku. Ni mwaliko kwa Familia kutekeleza wajibu wake kwa upendo, ukarimu na uwepo wao. Vijana wajifunze kuwa wasikivu kwa walezi wao wakitambua kwamba, wao pia ni wadau katika Uinjilishaji Mpya.







All the contents on this site are copyrighted ©.