2012-12-15 09:02:14

Uinjilishaji Mpya unajikita katika: Katekesi ya kina, maisha adili, ukweli na uwazi!


Kardinali Polycarp Pengo, Rais wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Magascar, SECAM katika mahojiano maalum na Radio Vatican anabainisha umuhimu wa viongozi wa Kanisa Barani Afrika kutoa katekesi ya kina inayopata chimbuko lake katika mafundisho tanzu ya Kanisa, maisha adili, ukweli, uwazi kama sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji Mpya, dhamana inayotekelezwa na Mama Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo. RealAudioMP3

Vyama vya kitume ndani ya Kanisa havina budi kupewa katekesi ya kina inayogusa kwa undani zaidi kuhusu: Imani, Sakramenti, Maisha adili na Sala, ili wanachama wa vyama hivi waweze kufahamu lengo pamoja na kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa, daima wakipania kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao kuyatakatifuza malimwengu; vinginevyo, wanaweza kujikuta wamepotoka.

Kardinali Pengo anawahimiza Viongozi wa Kanisa kuwa karibu na tayari kutoa katekesi ya kina inayojengeka katika mhimili wa maisha adili na nyofu; ukweli na uwazi, kwani hii ni changamoto kubwa kwa Mama kanisa wakati huu linahamasisha juhudi za Uinjilishaji Mpya. Toba na wongofu wa ndani pamoja na ushuhuda wa Imani katika matendo ni mambo msingi kwa wakati huu.







All the contents on this site are copyrighted ©.