Mpendwa msikilizaji wa Radio Vatican, nakukaribisha tena katika mfululizo wa vipindi
vyetu vya uinjilishaji wa Kina ambapo leo tunaendelea na uchambuzi wa Lineamenta ya
Sinodi ya Maaskofu. Juma hili tuendelee kuchambua juu ya ufundishaji wa dini ulio
utoaji wa Elimu katika kweli. Tega sikio tuwe pamoja tuendelee kumegeana na kushirikishana
Roho Mtakatifu anayejidhihirisha kwetu sote.
Kanisa linapofundisha juu ya Mungu
au linapozungumza juu ya Mungu linatoa elimu katika ukweli, elimu inayolenga kumjenga
Mwanadamu katika ubinadamu wake. Tangu mwanzo Kanisa limejikita katika Elimu si kwa
sababu nyingine yoyote bali kumwinua binadamu katika ubinadamu akapate kujifahamu
yeye ni nani, ametoka wapi na kwa nini yuko pale alipo. Mtaguso Mkuu wa Vatikan umesisitiza
pia juu ya mfungamano kati ya uinjilishaji na utoaji wa Elimu.
Baba Mtakatifu
Benedikto XVI anakazia uzito ukweli huu anapozungumzia utume msingi wa Kanisa wa uinjilishaji
unaotoa kipaumbele katika elimu na kuwianisha na malengo ya Taifa lolote kuendeleza
na kuiinua jamii katika hadhi inayotegemewa. Ikumbukwe kwamba Kanisa katika utume
wake linaoanisha daima dhana za imani na akili kwamba imani huiangaza akili kutambua
ukweli na hivyo kumfanya binadamu kuutambua ukweli ulio msingi wa maisha adilifu yampasayo
kuishi.
Baba Mtakatifu Benedikto XVI anakazia kuwepo kwa muungano kati ya uinjilishaji
na utoaji wa elimu hasa nyakati hizi ambapo elimu dunia inaelekea kumpoteza mwanadamu
katika ulimwengu. Hivyo amelialika Kanisa kulichukulia makini suala la uenezaji wa
Imani kufungamana na utoaji wa elimu ili kweli elimu itoe ujuzi na maarifa ya kumwendeleza
mtu mzima kiroho na kimwili.
Baba Mtakatifu Benedikto XVI ametahadharisha
kuwa mfumo wa elimu hivi sasa umeshindwa kutoa malezi bora kwa kizazi kipya kiasi
kwamba imedhihirika wazi uwepo wa mmomonyoko wa maadili katika jamii. Elimu inayotolewa
ni elimu maarifa tu bila thamani za maisha.
Nyakati hizi watu wengi wanaogopa
kusema ukweli na badala yake kukimbilia propaganda za kidunia na utumbuaji wa maisha
tu. Matokeo yake watu wanapumbazwa na propaganda za biashara na kuishia kufikiria
kwamba maisha ni ponda mali kufa kwaja bila kuangalia thamani halisi ya maisha ya
Mwanadamu.
Ulimwengu wa leo unatoa elimu amabayo haimwajibishi mwanadamu katika
matendo yake na baadaye anapokutana na changamoto za maisha anakosa mwelekeo na kuishia
kuchukua hatua zisizo za kibinadamu kwani ndani yake kakosa utu kageuka kitu ambacho
kikikosa thamani yake hutupwa jalalani au kuchomwa moto. Baba Mtakatifu na Kanisa
zima lazima liguswe na hili kwani utume wake si kuokoa roho tu bali na mwili pia ambao
ndilo hekalu la roho hapa duniani.
Wajibu wa Kanisa kujikita katika utoaji
Elimu ni kuboresha mazingira ya maisha ya mwanadamu. Baba Mtakatifu anasema Kanisa
litawajibishwa na Bwana iwapo halitapigania kujenga utu wa mwanadamu jinsi ile alivyokusudiwa
na Muumba. Hivi sasa kumekosekana heshima kwa ubinadamu hivi kwamba, watu hawathamini
tena zawadi ya maisha, wanaona kama mzigo, au kitu cha kufanyia utafiti kwenye maabara
kwa malengo ya kiburi tu; mimba kutupwa ovyo, biashara zilizokithiri za viungo na
miili ya binadamu, na watoto kuuzwa kama bidhaa. Iko hatari hapa ya ubinadamu kukengeuka
kama enzi za Sodoma na Gomora. Hivyo Kanisa lililo Mwili wa Kristo halina budi kusimama
kidete kurudisha tena hadhi na thamani ya binadamu iliyo hatarini kupotea.
Baba
Mtakatifu Benedikto XVI amemnukuu Baba Mtakatifu Paulo VI, kuwa Mwanadamu wa leo husikiliza
zaidi ushuhuda kuliko mafundisho ya mwalimu, vinginevyo Mwalimu atasikilizwa kwa sababu
anatoa ushuhuda. Hivyo amelitaka Kanisa kutumia ushuhuda wa maisha katika utoaji wa
elimu kwa jamii. Maisha ya ushuhuda yanayoshuhudia ukweli wa Imani na maisha, ndicho
kifundishio pekee kwa jamii ya leo.
Changamoto kwa Kanisa na Wanakanisa ni
kujitoa mhanga kutoa mifano hai ya maisha yaliyojengwa katika dhamiri iliyo safi,
hai na adilifu. Maisha ya utakatifu, usafi, unyenyekevu, upole, amani, haki na mshikamano
ndizo silaha pekee za kumfikisha Yesu Mkombozi wa dunia kwa watu.
Mpendwa msikilizaji
ni matumaini yangu tumejichotea maarifa ya kutosha na mang’amuzi tele kutuwezesha
kusoma vizuri hati itakayotoka baada ya Sinodi ya Mababa. Kufikia hapa tunafunga uchambuzi
wetu wa limeamenta ya Sinodi ya Maaskofu.
Nakutakia kheri na Baraka katika
kumshuhudia Yesu katika ulimwengu wa leo ambao unaonekana kupoteza maarifa. Shime
Mkristu mwenzangu twende tukalirudishe lile tumaini la Kristu kwa watu hawa kwani
sisi tumeona mwanga basi tuupeleke mwanga huu na kwa wengine.
Kutoka studio
za Radio Vatican ni mimi mtayarishaji na msimulizi wako Padre George wa Bodyo.