2012-12-10 10:00:03

Padre Moses Mapela achaguliwa kuongoza Umoja wa Wanafunzi Wakatoliki Watanzania wanaosoma Roma!


Umoja wa Wanafunzi Wakatoliki Watanzania wanaosoma na kuishi mjini Roma, Jumapili tarehe 9 Desemba 2012 pamoja na kusherehekea miaka 51 ya uhuru wa Tanzania, pia walifanya uchaguzi mkuu wa viongozi ambao wamepewa dhamana ya kuongoza Umoja huu kwa kipindi cha Mwaka mmoja. RealAudioMP3

Usimamizi wa uchaguzi uliongozwa na Mheshimiwa Padre Philip Massawe mmoja wa walezi wa wanafunzi hao na kuhudhuriwa pia na Askofu mkuu Protase Rugambwa, Katibu Mwambata wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa Watu na Rais wa Mashirika ya Kimissionari ya Kipapa.

Askofu mkuu Rugambwa amewashukuru na kuwapongeza viongozi waliopita kwa kujitoa kimasomaso kuendeleza umoja na mshikamano wa wanafunzi watanzania wanaosoma mjini Roma. Anawaalika viongozi wapya kukuza nguvu ya umoja na udugu ili kukabiliana na changamoto za malimwengu na ubinafsi ambao ni sumu ya maendeleo katika kukuza na kuendeleza mshikamano, maridhiano na umoja.

Hizi ni tunu ambazo zinapaswa kutangazwa kwa nguvu zote, lakini zaidi lazima zimwilishwe katika uhalisia wa maisha. Uongozi ni dhamana inayohitaji majitoleo na nidhamu ya hali ya juu. Wakati mwingine si rahisi kupokea dhamana hii.

Yafuatayo ni majembe mapya yaliyochaguliwa kuongoza Umoja wa Wanafunzi Watanzania Wakatoliki wanaosoma Roma:

Padre Moses Mapela kutoka Jimbo kuu la Mwanza anakuwa Mwenyekiti mpya.
Padre Alister Makubi kutoka Jimbo kuu la Dar es Salaam anakuwa Katibu.
Sr. Theresa Tarimo kutoka Shirika la Kazi za Roho Mtakatifu: mtunza hazina.
Padre Joseph Mahela kutoka Shirika la Kazi za Roho Mtakatifu: Liturujia.
Padre Nikodemo Mayala: Mkutubi.







All the contents on this site are copyrighted ©.