Padre Moses Mapela achaguliwa kuongoza Umoja wa Wanafunzi Wakatoliki Watanzania wanaosoma
Roma!
Umoja wa Wanafunzi Wakatoliki Watanzania wanaosoma na kuishi mjini Roma, Jumapili
tarehe 9 Desemba 2012 pamoja na kusherehekea miaka 51 ya uhuru wa Tanzania, pia walifanya
uchaguzi mkuu wa viongozi ambao wamepewa dhamana ya kuongoza Umoja huu kwa kipindi
cha Mwaka mmoja.
Usimamizi
wa uchaguzi uliongozwa na Mheshimiwa Padre Philip Massawe mmoja wa walezi wa wanafunzi
hao na kuhudhuriwa pia na Askofu mkuu Protase Rugambwa, Katibu Mwambata wa Baraza
la Kipapa la Uinjilishaji wa Watu na Rais wa Mashirika ya Kimissionari ya Kipapa.
Askofu
mkuu Rugambwa amewashukuru na kuwapongeza viongozi waliopita kwa kujitoa kimasomaso
kuendeleza umoja na mshikamano wa wanafunzi watanzania wanaosoma mjini Roma. Anawaalika
viongozi wapya kukuza nguvu ya umoja na udugu ili kukabiliana na changamoto za malimwengu
na ubinafsi ambao ni sumu ya maendeleo katika kukuza na kuendeleza mshikamano, maridhiano
na umoja.
Hizi ni tunu ambazo zinapaswa kutangazwa kwa nguvu zote, lakini
zaidi lazima zimwilishwe katika uhalisia wa maisha. Uongozi ni dhamana inayohitaji
majitoleo na nidhamu ya hali ya juu. Wakati mwingine si rahisi kupokea dhamana hii.
Yafuatayo
ni majembe mapya yaliyochaguliwa kuongoza Umoja wa Wanafunzi Watanzania Wakatoliki
wanaosoma Roma:
Padre Moses Mapela kutoka Jimbo kuu la Mwanza anakuwa Mwenyekiti
mpya. Padre Alister Makubi kutoka Jimbo kuu la Dar es Salaam anakuwa Katibu. Sr.
Theresa Tarimo kutoka Shirika la Kazi za Roho Mtakatifu: mtunza hazina. Padre Joseph
Mahela kutoka Shirika la Kazi za Roho Mtakatifu: Liturujia. Padre Nikodemo Mayala:
Mkutubi.