2012-12-10 07:15:13

Balozi wa Vatican nchini Pwani ya Pembe afariki dunia kwa ajali ya gari!


Askofu mkuu Ambrose Madtha, Balozi wa Vatican nchini Pwani ya Pembe, amefariki dunia Jumamosi jioni tarehe 8 Desemba 2012 baada ya gari alilokuwa anasafiria kugongana uso kwa uso nje kidogo ya Mji wa Abijan. Askofu mkuu Madtha alikuwa anarejea nyumbani baada ya maadhimisho ya Siku kuu ya Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili. Dereva wake pia amefariki katika ajali hii. Katibu wa Balozi pamoja na mtawa mmoja wamesalimika ingawa wamepata majeraha.

Rais wa Pwani ya Pembe ametuma salam za rambi rambi kwa Kanisa Katoliki nchini Pwani ya Pembe pamoja na kwa familia ya Marehemu Askofu mkuu Ambrose Madtha kutokana na msiba huu mkubwa. Anasema, amepokea kwa majonzi makubwa habari za msiba wa Askofu mkuu Ambrose Madtha.

Marehemu Askofu mkuu Madtha alizaliwa kunako mwaka 1955 nchini India; Akapadrishwa mwaka 1982. Baada ya kutumikia sehemu mbali mbali za Balozi za Vatican, kunako mwaka 2008, Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, alimteua kuwa Balozi mpya wa Pwani ya Pembe. Anakumbukwa na wengi nchini humo kutokana na jitihada zake za kuhimiza majadiliano kama njia ya kumaliza mgogoro wa kivita uliokuwa umeitikisa Pwani ya Pembe kwa miaka ya hivi karibuni.







All the contents on this site are copyrighted ©.