Papa apokea "Papamobile" kwa ajili ya shughuli za kichungaji
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Ijumaa tarehe 7 Desemba 2012 amepokea gari
jipya aina ya Mercedes Benz kwa ajili ya matumizi ya Khalifa wa Mtakatifu Petro. Ni
gari ambalo limetengezwa maalum ili kumwezesha Baba Mtakatifu kuwa karibu na watu
wanaotaka kumwona wakati wa hija zake za kichungaji sehemu mbali mbali za dunia; kwa
kuzingatia pia viwango vya usalama na utulivu.
Kwa mara ya kwanza gari hili
linaanza kutumika wakati Baba Mtakatifu atakapokwenda kuweka shada la maua kwenye
Sanamu ya Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili iliyoko kwenye Uwanja wa Spagna, mjini
Roma. Gari hili ni fupi ikilinganishwa na magari mengine ya kipapa yaliyotangulia
ili kutoa nafasi ya kuweza kubebwa kwenye ndege bila usumbufu mkubwa wakati wa hija
za kichungaji zinazofanywa na Khalifa wa Mtakatifu Petro sehemu mbali mbali za dunia.
Kampuni
ya Mercedes Benz kwa zaidi ya miaka themanini imekuwa ikitoa magari maalum yanayotumiwa
na Mapapa mjini Roma na wakati wa hija zao za kichungaji. Kwa mara ya kwanza Mercedes
Benz ilitoa gari kwa Vatican kunako mwaka 1930 na ufunguo wake akakabidhiwa Baba Mtakatifu
Pio wa kumi na moja.
Akielezea kuhusu gari la Papa, kama linavyojulikana na
wengi kuwa "Papamobile", Bwana Alberto Gaspari mratibu wa hija za kichungaji za Khalifa
wa Mtakatifu Petro anabaianisha kwamba, kwa mara ya kwanza, neno "Papamobile" lilianza
kutumiwa na wananchi wa Uingereza kunako mwaka 1982; mwaka mmoja tu baada ya jaribio
la kutaka kumuua liliposhindikana kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini
Vatican.
Tangu wakati huo, makampuni yaliyokuwa yanatengeneza magari kwa ajili
ya matumizi ya Papa yalipaswa kuzingatia pamoja na mambo mengine usalama wake. Uingereza
na Hispania ni kati ya nchi za kwanza kabisa kutengeneza magari kwa viwango na sifa
zilizokuwa zinahitajika, ili kupunguza gharama za kumsafirisha Baba Mtakatifu, magari
maalum yakawa yametengenezwa na kusafirishwa pale yanapohitajika. Baadhi ya magari
haya yako kwenye Jumba la Makumbusho ya Vatican, ukifika mjini Vatican, usikose kwenda
kuchungulia.
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, wakati wote huu ameendelea
kutumia gari lililoachwa na Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili. Gari jipya linakidhi
viwango na sifa zinazohitajika.