Sehemu ya kwanza ya Mahubiri kwa Baba Mtakatifu na Wasaidizi wake: Umuhimu wa Katekisimu
Mpya ya Kanisa Katoliki
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita pamoja na wasaidizi wake wa karibu, Ijumaa
tarehe, 7 Desemba 2012 wamefanya tafakari ya kwanza ya kipindi cha Majilio iliyoongozwa
na Padre Raniero Cantalamessa, mhubiri wa nyumba ya kipapa ambaye amezungumzia juu
ya Mwaka wa Imani, mintarafu Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki kama chombo makini
kitakachowawezesha waamini kuishi na kuadhimisha kikamilifu Mwaka wa Imani, kwani
huu ni muhtasari wa Mafundisho Makuu na Imani ya Kanisa.
Ni changamoto kwa
waamini kuhakikisha kwamba, wanaifahamu Imani yao ili kuleta furaha ya ndani, vinginevyo,
Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki itabaki imehifadhiwa kwenye Maktaba bila ya kuwa
na manufaa makubwa katika maisha ya waamini. NI mwaliko wa kuisoma, kuitafakari na
kuimwilisha katika ushuhuda wa maisha kama kielelezo cha Imani wanayoungama, Adhimisha,
Ishi na Kusali. Kiini cha Katekisimu hii ni Yesu Kristo anayeendelea kuandama na Kanisa
lake, kwa njia ya Maandiko Matakatifu na Mapokeo hai ya Kanisa.
Kwa njia ya
Yesu Kristo anasema Padre Cantalamessa, waamini wapate fursa ya kukutana na Mwenyezi
Mungu aliyejifunua katika Agano la Kale na hatima yake ni katika Agano Jipya. Ni mwaliko
wa kuendeleza majadiliano ya kidini na Wayahudi, kama wanavyohimiza Mababa wa Mtaguso
Mkuu wa Pili wa Vatican.
Mama Kanisa anatumwa kutangaza Habari Njema ya Wokovu
inayojikita kwa Yesu aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu. Ili waamini
waweze kuiungama vyema Imani yao kwa Kristo, kuna haja ya kuwa na majiundo endelevu,
kama walivyofanya Mitume kwa Kanisa la Mwanzo. Hizi ni jitihada za kuunganisha mwanga
wa maisha ya mwanadamu na yale ya Kimungu, kama inavyojidhihirisha pia katika Injili,
Kanuni ya Imani na Maadhimisho ya Sakramenti za Kanisa.
Familia ya Mungu inawajibu
wa kutangaza Kweli za Kiinjili, kama sehemu ya mchakato wa kukuza na kuimarisha Imani
dhamana inayotekelezwa na Mama Kanisa katika Uinjilishaji Mpya kwa kutafuta mbinu
na nyenzo mintarafu mazingira na watu wanaoishi katika ulimwengu wa utandawazi.
Katekisimu
Mpya ya Kanisa Katoliki iwe ni nyenzo kwa ajili ya majiundo makini ya Imani kwa kutambua
maudhui, madai na utekelezaji wake unaojionesha katika Imani tendaji. Ni mwelekeo
mpya wa Imani unaohitaji toba na wongofu wa ndani. Baada ya kupokea zawadi ya Imani,
mwamini anatakiwa kuikuza Imani hiyo ili iweze kufikia utimilifu katika maisha ya
Kikristo, kwani Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki ni kumbu kumbu hai na endelevu
juu ya tafakari ya kina kuhusu Imani thabiti wanayopaswa kuiungama na kuitolea ushuhuda
amini wafuasi wote wa Kristo.
Waamini kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo na
Kipaimara wamempokea Roho Mtakatifu, Mwaliku wa kweli anayewafundisha Ukweli Wote
kama wanavyosema Mababa wa Kanisa, tayari kuutolea ushuhuda katika uhalisia wa maisha,
kwani wamelifahamu na kuamini katika pendo la Mungu na kwa njia hii, wamemwamini Yesu
Kristo kuwa ni Mtakatifu wa Mungu, mwaliko wa kujenga na kuimarisha uhusiano wao pamoja
naye.
Kwa njia ya Roho Mtakatifu, Neno wa Mungu alifanyika mwili akakaa kati
ya watu wake, atakuja tena kuwahukumu wazima na wafu na ufalme wake hautakuwa na mwisho.
Waamini wakifahamu undani wa Imani yao wataweza kuiungamana na kumtolea ushuhuda Yesu
Kristo na huu ndio mchakato wa Uinjilishaji Mpya. Waamini wafahamu kwa dhati kabisa
kweli za Kiinjili ili kuziungama kwa furaha kubwa.
Kristo ni Neno wa Mungu
aliyefanyika Mwili kwa njia ya Roho Mtakatifu kwake Bikira Maria akawa mwanadamu.
Kutokana na ukweli huu, Bikira Maria ni kielelezo cha kila Mwinjilishaji na Katekisita.
Ni mwaliko wa kumpokea Kristo, ili kumtoa pia kwa ajili ya wengine. Waamini wakumbuke
kwamba, wamempokea pia Roho Mtakatifu, kumbe wanadhamana ya kumtangaza Kristo kwa
ujasiri mkubwa zaidi; wana heri wale wanaoamini katika Kipindi hiki cha Neema, kama
alivyofanya Bikira Maria.