Rais Joachim Gauck wa Ujerumani akutana na Papa Benedikto XVI mjini Vatican
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Alhamisi tarehe 6 Desemba 2012 amekutana
na kufanya mazungumzo na Bwana Joachim Gauck, Rais wa Shirikisho la Ujerumani na baadaye
kiongozi huyo na ujumbe wake, walikutana na Kardinali Tarcisio Bertone, katibu mkuu
wa Vatican pamoja na viongozi wengine waandamizi kutoka Vatican.
Viongozi
hawa wamejadili pamoja na mambo mengine uhusiano mzuri kati ya Vatican na Ujerumani.
Wamegusia mtazamo wa Kikristo kuhusu mwanadamu na changamoto zinazoendelea kujitokeza
katika ulimwengu wa utandawazi. Wamebadilishana pia mawazo kuhusu masuala mbali mbali
ya kimataifa: athari za myumbo wa uchumi kimataifa Barani Ulaya na mchango ambao Kanisa
Katoliki linaweza kuchangia katika hali kama hii.