2012-12-05 10:24:28

Ujumbe wa Kipindi cha Majilio kutoka kwa Askofu mkuu Rowan Williams


Askofu mkuu Rowan Williams wa Kanisa kuu la Cantebury ambaye ni Kiongozi mkuu wa Jumuiya ya Waanglikani Duniani katika ujumbe wake Kipindi cha Majilio kwa Mwaka 2012 anawaalika waamini wa Kanisa Anglikani kugundua na kuthamini utambulisho wao kama Familia kubwa wanamoshirikishana matumaini na kwamba, mbele ya Mwenyezi Mungu wanawajibika kwa ajili ya mafao ya wengine.

Jumuiya ya Waangalikani yenye waamini wapatao millioni themanini na kwamba, anamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwakirimia Kiongozi mwingine Askofu Justin Welby wa Jimbo la Durham atakayemrithi. Anawaalika waamini kumsindikiza kwa njia ya Sala wakati huu anapojiandaa kuanza kutekeleza utume wake hapo mwakani. Anakazia umoja na mshikamano miongoni mwa waamini kwa kutambua kwamba, majadiliano ya kitaalimungu yanatishia kuleta mpasuko mkubwa miongoni mwa Waamini wa Kanisa Anglikani.

Anawataka kuonesha ushuhuda thabiti na endelevu wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, heshima miongoni mwao na kwa viongozi waliopewa dhamana. Umoja miongoni mwa waamini wa Kanisa Anglikani umekumbatana na kinzani na hali ya kutoeleweka hadi leo hii, lakini wanayo bahati ya kuuona utukufu wa Mungu unaojidhihirisha kwa njia ya uso wa Yesu katika medani mbali mbali za maisha. Lengo liwe ni kuimarisha umoja na mshikamano ili kutekeleza utume wa Kanisa.

Kipindi cha Majilio, iwe ni fursa kuimarisha Injili ya Upendo; Umoja na Mshikamano kati ya waamini wa Kanisa Anglikani katika Majimbo mbali mbali duniani, hata kama bado kuna maswali kadhaa ambayo hayajapata majibu muafaka kuhusiana na Mafundisho Tanzu ya Kanisa. Kwa pamoja washikamane ili kukabiliana na changamoto zilizopo kwa sasa. Utengano isiwe ni sababu ya kuvuruga ujenzi wa Ufalme wa Mungu.

Waamini washikamane katika Uinjilishaji Mpya; katika utoaji wa huduma kwenye sekta ya afya; kusimama kidete kulinda na kutetea utu na haki msingi za binadamu, bila kusahau kuhifadhi mazingira. Ni rahisi mno kuweza kuiona sura ya Kristo, lakini ukweli ni kwamba, waamini wasipokuwa makini, itawawia vigumu kuweza kupata suluhu ya matatizo na changamoto wanazokabiliana nazo. Mshikamano wa upendo pamoja na kuaminiana unaweza kuleta mabadiliko yanayokusudiwa.







All the contents on this site are copyrighted ©.