Uwepo wa Baba Mtakatifu Benedikto XVI kwenye mtandao wa Twitter, mwendo ni mdundo!
Zaidi ya watu laki nne tayari wamekwishajiandikisha katika akaunti ya Baba Mtakatifu
Benedikto wa kumi na sita kwenye mtandao wa kijamii wa twitter katika lugha saba,
tangu ulipozinduliwa siku ya Jumatatu tarehe 3 Desemba 2012 , ingawa Baba Mtakatifu
atuzindua rasmi kwa kujibu maswali wanayoendelea kumuuliza hapo tarehe 12 Desemba
2012.
Hii inaonesha kwamba, Jukwaa la Mitandao ya Kijamii lilikuwa na hamu
na kiu ya kutaka kuwasiliana na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, pamoja na
wasaidizi wake wa karibu, moja kwa moja, mahali walipo; jambo linalowezeshwa kutokana
na maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari na mawasiliano, ili kugusa akili,
nyoyo na matamanio ya watu wanaoogelea katika mitandao hii.
Ni maneno ya Padre
Federico Lombardi, Msemaji mkuu wa Vatican wakati alipokuwa anajibu maswali kuhusu
mafanikio ambayo yamepatikana kutokana na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita,
kuanza kutumia mitandao ya kijamii kama njia ya kujenga na kudumisha majadiliano ya
kina kuhusu imani, matumaini na mapendo. Baba Mtakatifu anawachagamotisha Wakristo
kujitoa kimasomaso kuliinjilisha Jukwaa la Watumiaji wa Mitandao ya Kijamii.
Padre
Lombardi anasema, Baba Mtakatifu alikwisha onja mafanikio ya matumizi ya mitandao
ya kijamii wakati wa maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani iliyofanyika mjini Sydney,
vijana wengi walikuwa wanamtumia ujumbe mfupi wa maneno na kwamba, uwepo wake kwenye
mitandao ya kijamii, anapania kuwafikia watu wengi zaidi.
Ni mwaliko pia kwa
viongozi wengine wa Kanisa kuiga mfano huu kadiri ya uwezo wao. Kanisa halina budi
kuendeleza utambulisho wake kwamba, ni Jumuiya Kubwa yenye dhamana na wajibu wa kuwasiliana
na watu wengi zaidi; kujibu matarajio na matamanio ya watu wa ulimwengu wa sayansi
na teknolojia mintarafu Habari Njema ya Wokovu na Kweli za Kiinjili.
Vyombo
mbali mbali vya mawasiliano ya jamii vinavyomilikiwa na kuendeshwa na Vatican, kwa
miaka kadhaa sasa vinaendelea kutumia mitandao mbali mbali ili kufikisha ujumbe wake
kwa hadhira inayokusudiwa, kama njia ya kujenga na kuendeleza majadiliano na watu
kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Mawasiliano haya kama ambavyo Baba Mtakatifu Benedikto
alivyobainisha alipotembelea kwa mara ya kwanza Radio Vatican ni kutaka kujenga jukwaa
la majadiliano ya kina, kwa kuunda na kuimarisha familia inayowasiliana.
Padre
Federico Lombardi anasema, maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari na mawasiliano
yana matatizo na changamoto zake, Kanisa halina budi kuendelea kujifunza ili kuboresha
ujumbe unaotolewa kwenye mitandao hii.
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na
sita, katika umri wake anajifunza kutumia mitandao ya kijamii ni changamoto na mwaliko
kwa Kanisa kujifunga kibwebwe ili kuonesha uwepo wake endelevu na wenye mguso katika
Jukwaa la Mitandao ya Kijamii. Wasaidizi wake katika kuongoza, kufundisha na kuwatakatifuza
watu ambao wamekabidhiwa kwao wanachangamotishwa kuiga mfano huu kwa ajili ya mafao
na maendeleo ya Kanisa katika majadiliano ya kina.