2012-12-04 10:01:27

Unaweza kutwitter na Baba Mtakatifu kwa anuani ifuatayo: @pontifex


Askofu mkuu Claudio Maria Celli, Rais wa Baraza la Kipapa la Mawasiliano ya Jamii, Jumatatu, tarehe 3 Desemba 2012 ameongoza ujumbe wa wakuu wa idara mbali mbali za mawasiliano mjini Vatican katika uzinduzi wa matumizi ya Twitter kwa ajili ya Baba Mtakatifu benedikto wa kumi na sita; mtandao wa kijamii ambao utaanza kutumiza rasmi hapo tarehe 12 Desemba 2012, Kanisa litakapokuwa linaadhimisha Kumbu kumbu ya Bikira Maria wa Guadalupe.

Kuanzia sasa unaweza kutweet na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kwa kwa lugha nane: Kiingereza, Kihispania, Kiitaliani, Kijerumani, Kipolandi, Kiarabu na Kifaransa kwa kutumia anuani ifuatayo @pontifex.

Baba Mtakatifu anatarajiwa kuzindua rasmi matumizi haya kwa kujibu maswali kadhaa kuhusu Imani yatakayokuwa yameulizwa na watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Hii ni njia muafaka anasema baba Mtakatifu kwa Kanisa kufanya majadiliano ya kina na waamini wanaoishi katika ulimwengu wa mtandao ambao wanaonesha kiu na njaa ya kutaka kukutana na Mwenyezi Mungu.

Itakumbukwa kwamba, tangu mwaka 2009, Vatican ilianza pia kutumia mtandao wa Youtube na Baba Mtakatifu mwenyewe akaonesha umuhimu wa Kanisa kuviinjilisha vyombo vya mawasiliano ya jamii kwa kuvisaidia kupata tunu msingi za maisha ya kijamii na kiutu, ambazo zitatumiwa na wahusika katika kuboresha maisha yao.

Mwaka 2010, Baba Mtakatifu akawaalika Viongozi wa Kanisa na kwa namna ya pekee, Mapadre kushirikisha Neno la Mungu kwa njia ya mtandao, ili kuendeleza dhamana ya Mama Kanisa katika kutangaza Habari Njema ya Wokovu kwa kutumia pia maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari. Mitandao ya Kijamii inaendelea kuboresha maisha ya watu wengi licha ya changamoto na vikwazo vinavyojitokeza; lakini hata hapa Mama Kanisa lazima aendeleze utume wake wa Kuinjilisha.

Hili ni jukwaa la majadiliano ya kina kati ya Kanisa na watumiaji wa mitandao kuhusiana na Injili ya Kristo pamoja na Mafundisho Jamii ya Kanisa. Baba Mtakatifu anataka kuonesha njia ya kujadiliana na watu, kwa kutambua kwamba, Kanisa ni Mama anayesikiliza na kujali shida na mahangaiko ya watoto wake. Hii ni changamoto pia kwa viongozi wengine wa Kanisa kujiwekea utaratibu wa kuweza kujibu kiu na njaa ya watu katika hija ya maisha yao ya kiroho.

Uwepo wa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita katika mtandao wa kijamii ni kuwakilisha sauti ya mshikamano na viongozi wengine wa Kanisa. Ni mwaliko na changamoto kwa waamini pia kupaza sauti zao, kwa kuwashirikisha wengine utajiri wa Habari Njema ya Wokovu kwa njia ya majadiliano ya kina yanayogusa undani wa Imani, Matumaini na Mapenda, fadhila za Kimungu.

Mwanzoni mwa Mwezi Desemba, watumiaji wa mtandao wanaweza kuanza kumuuliza maswali Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita na majibu ya maswali haya yatatolewa wakati wa kuzindua rasmi mtandao wa twitter. Mwanzoni mwa matumizi ya mtandao huu, kutakuwa na mfumo wa maswali na majibu, kama kielelezo cha Mama Kanisa anayesikiliza na kujali wasi wasi na matumaini ya watoto wake.







All the contents on this site are copyrighted ©.