2012-12-03 07:32:06

Wanandoa jengeni uwiano mzuri kati ya kazi na familia!


Ndugu msikilizaji wa Radio Vatican, tunapoendelea na tafakari yetu kuhusu miito ya familia na kazi ni vizuri leo tukumbushane kuwa miito hii miwili tofauti haipaswi kufarakana bali kujenga mahusiano mazuri. RealAudioMP3
Jambo la kushangaza ni kuwa katika jamii yetu leo miito hii miwili iko kwenye mivutano sana na mara nyingi familia inaonekana sio muhimu kama kazi. Wengi wanajiuliza je ni sawa kubali mshahara kidogo ili nipokee wajibu wa uzazi au malezi ya watoto au afadhali kuahirisha uzazi na malezi nijiendeleze na kufanya kazi zaidi ili nipate mshahara mkubwa? Lile lililo jukumu msingi la familia yaani uzazi na malezi mahali pengi kwa sasa linahesabika kama kazi isiyo na ujira (Unpaid work)
Leo hii kazi inaonekana ndio wito pekee wenye thamani kubwa kuliko familia. Na jambo la ajabu zaidi ni pale kazi inapomgeuza mwanadamu kuwa chombo cha uzalishaji tu bila hata kujali utu wake. Kazi imegeuka kuwa bidhaa tena bidhaa adimu. Hata mwanamke ambaye umama wake hauwezi kubadilishwa na chochote leo hii wimbi la wakati linamkuta katika kudai haki sawa katika mishahara na ajiri. Haki sawa ni jambo jema lakini nafasi ya umama katika malezi haiwezi kuzibwa na mtu mwingine yeyote.
Mahali pengine familia imehesabika na kuonekana kama taasisi binafsi kama vile dini ambayo ni kwa ajili ya watu wachache na sio kwa jamii nzima. Ndugu msikilizaji kazi kama ilivyo familia inamhusu kila mwanadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu haina dini wala kabila.
Mwaliko wa kanisa kwa wakati wote ni kujenga uwiano mzuri kati kati ya familia na kazi. Ni lazima tutambue kuwa japo kazi na familia ni miito miwili tofauti lakini yote hutusaidia kudhihirisha upendo na kukua katika utakatifu. Ni Mungu huyo huyo aliyetoa amri ya kuzaa na kuongezeka yaani kujenga familia lakini ni huyo huyo anayempa mwanadamu amri ya kufanya kazi. (Mwanzo 1:27-28). Kilele chake ni pale Mungu anapokubali umwilisho katika familia nakuifanya kazi kwa wakati wote mpaka pale juu msalabani.
Ndugu msikilizaji, katika tafakari zetu toka waraka wa mwenye heri Yohane Paulo II (Familiaris Consortio) tulisema mwanamume ni mume kwa mkewe na baba kwa watoto wake, hivyo endapo kazi za kiuchumi zitamtenga na majukumu haya ya kifamilia basi familia yake iko hatarini. Tulisema mwanamke ni mke kwa mumewe, lakini, mama kwa watoto wake hivyo endapo kazi zake za kiuchumi zinamtenga na wajibu huu basi familia yake iko hatarini.
Tumalizie tafakari yetu ya leo kwa kurudia kuwa kinachotakiwa ni uwiano mzuri kati ya kazi na familia kwani yote ni muhimu na yanategemeana. Daima tukumbuke kuwa kazi chimbuko lake ni familia na kazi ni kwa ajili ya familia.
Kutoka Studio za Radio Vatican ni mimi ni Padre Raphael Mwanga, wa Jimbo Katoliki la Same, Taasisi ya Ndoa na Familia, Chuo Kikuu cha Kipapa Laterano- Roma.








All the contents on this site are copyrighted ©.