Kila Mwaka ifikapo tarehe 3 Desemba, Jumuiya ya Kimataifa inaadhimisha Siku ya Walemavu
Kimataifa, kwa kukazia haki zao msingi. Askofu mkuu Zygmunt Zimowski, Rais wa Baraza
la Kipapa la wahudumu wa Sekta ya Afya anasema katika ujumbe wake kwa maadhimisho
haya kwamba, hawa ni watu wenye thamani kubwa katika maisha ya kiimani, kwani wanashiriki
katika mateso na upendo wa Kristo kwa waja wake.
Utu na heshima yao vinapaswa
kulindwa na kuheshimiwa; walemavu kwa upande wao, wapokee hali yao ya maisha kwa imani
na matumaini. Wasikilizwe katika shida na mahangaiko yao ya ndani; washirikishwe katika
maisha na utume wa Kanisa, kwa kuwamegea ukarimu na kulinda haki zao msingi. Wapewe
huduma za tiba; miundo mbinu iwazeshe kuishi kwa ukamilifu zaidi, wakiendelea kusaidiwa
na Familia zao; daima mafao yao kama binadamu yapewe kipaumbele cha kwanza.
Mama
Kanisa anapenda kuonesha ukaribu wake kwa watu wenye ulemavu, kwa kuwashirikisha mwanga
wa Imani, matumaini, mapendo na mshikamano wa kweli. Walemavu ni watu wanaopaswa kupewa
tiba, lakini zaidi waonjeshwe upendo, watambuliwe, waheshimiwe na kushirikishwa katika
maisha ya jamii inayowazunguka.
Wasionekane kuwa ni kikwazo na kizingiti cha
maendeleo ya binadamu, kwani ni kielelezo makini cha Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka
kutoka katika wafu. Ni walimu wa upendo unaookoa na watangazaji wa Habari Njema ya
Wokovu ya upendo, mshikamano na ukarimu mintarafu mwanga wa Kristo.
Katika
Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, watu wenye ulemavu wajengewe pia uwezo wa kuwa ni vyombo
vya Uinjilishaji Mpya, kwa kustahimilia mateso na mahangaiko yao ya ndani pamoja na
kuwatendea vyema. Imani thabiti inamwezesha mwamini kuweza kuyapokea mateso na mahangaiko
yake kwa uvumilivu, matumaini na mapendo.
Askofu mkuu Zygmunt Zimowski anapenda
kuwahakikishia watu wenye ulemavu kwamba, Kanisa liko pamoja nao katika shida na mahangaiko
yao ya ndani na kamwe haliwezi kuwaacha pweke! Linasubiri kuona kwamba, hata wao wanashiriki
kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa.
Bikira Maria Mkingiwa dhambi
ya Asili, awasaidie waamini kutambua na kuonja ubinadamu uliojeruhiwa, ili kuwapokea
na kuwasaidia kutambua kwamba, hata wao wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu na kukombolewa
na yesu Kristo.