2012-12-03 15:07:17

Uelewa sahihi wa binadamu unapata chimbuko lake katika ufunuo na akili inayobainisha haki na wajibu wa binadamu


Baraza la Kipapa la Haki na Amani limefanya mkutano wake wa mwaka wakati huu Mama Kanisa anapoadhimisha Mwaka wa Imani, Jubilee ya Miaka 50 ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican pamoja na Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya. Bado muda kidogo Waraka wa Papa Yohane wa Ishirini na tatu: Amani Duniani, Pacem In Terris utakuwa unatimiza pia miaka 50 tangu ulipochapishwa. Yote haya ni matukio muhimu sana kwa maisha na utume wa Kanisa.

Mafundisho Jamii ya Kanisa ni sehemu muafaka ya dhamana ya Uinjilishaji inayotekelezwa na Mama Kanisa sehemu mbali mbali za dunia na ni chombo muhimu sana cha Uinjilishaji katika Mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo. Ni mwaliko kwa waamini kumpokea Yesu Kristo pamoja na kuendelea kumshuhudia katika medani mbali mbali za maisha; daima wakiwa na mwono sahihi wa binadamu, utu, uhuru na uwezo wake wa kufikiri. Ni mwono wenye mwelekeo katika maisha ya binadamu pamoja na kumpatia Mwenyezi Mungu nafasi anayostahili.

Ni sehemu ya hotuba ya Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, aliyoitoa Jumatatu tarehe 3 Desemba 2012 wakati alipokutana na Wajumbe wa Baraza la Kipapa la Haki na Amani ambao wamehitimisha Mkutano wao wa Mwaka hapa mjini Vatican. Baba Mtakatifu anasema, uelewa makini kuhusu binadamu unapata chimbuko lake katika Ufunuo sanjari na matumizi ya akili ya kawaida inayobainisha haki na wajibu wa binadamu, kama alivyopembua kwa kina na mapana Papa Yohane wa Ishirini na tatu.

Haki na wajibu ni chanda na pete kwani ni mambo yanayotegemeana pamoja na kujikita katika msingi wa maadili ambayo yameandikwa katika dhamiri ya mwanadamu na hivyo kupata mwelekeo sahihi wa mtu na jamii. Jamii nyingi zinaendelea kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu, lakini kwa bahati mbaya, kwa upande mwingine, kuna ubinafsi na sera za uchumi tenge ambazo zinazombeza mwanadamu.

Licha ya maendeleo ya mawasiliano ya jamii, lakini bado mwanadamu wa leo anajikuta akiogelea katika upweke; kinyume kabisa na asili yake ambayo ni kiini cha uhusiano kati yake na jirani zake pamoja na Mwenyezi Mungu. Mtu anajiona kuwa ni rasilimali na sehemu ya mchakato wa shughuli za uzalishaji na ununuzi; mambo yanayomdhalilisha utu na heshima yake.

Raha kupita kiasi na ubinafsi unaojionesha katika haki za kujamiiana, uzazi, mtaji unaojikita kwenye faida kubwa ni mambo ambayo yanaathari kubwa katika uchumi halisia. Mifumo hiii inamfanya mfanyakazi kuwa mtumwa wa kazi na kazi yake kuwa na mafao kidogo katika Jamii, hali inayohatarisha misingi ya maisha ya Familia. Binadamu katika asili yake, anaalikwa kuwaheshimu wengine, kulinda na kutunza mazingira kwani anatambua dhamana aliyo nayo kwake binafsi na kuhusiana na mazingira.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anasema kadiri ya Mafundisho ya Kanisa, kazi ni msingi wa maisha ya binadamu, kama mtu binafsi na jamii; sanjari na ushiriki wake katika kujenga familia, daima akitafuta mafao ya wengi pamoja na kukuza amani. Fursa za kazi ni jambo linalopaswa kupewa kipaumbele cha kwanza, hata wakati wa kuchechemea kwa uchumi wa kimataifa.

Uinjilishaji Mpya wa Jamii unaweza kumwibua mtu mpya mwenye kuthamini zaidi tamaduni na kutaka kuziendeleza. Ni mtu atakayesimama kidete kupambana na ubinafsi, malimwengu na teknolojia kwa kukuza na kudumisha udugu, hali ya kujitoa bila ya kujibakiza sanjari na mshikamano wa upendo; kwa kumwilisha Amri ya Upendo kwa Mungu na Jirani. Hii ndiyo siri ya mabadiliko katika Jamii kitaifa na Kimataifa.

Papa Yohane wa Ishirini na tatu aliichangamotisha Dunia, kujenga Jumuiya ya Kimataifa inayojikita katika upendo kwa ajili ya mafao ya Familia ya binadamu, kama anavyobainisha kwenye Waraka wake kuhusu Amani Duniani. Kanisa halina mamlaka ya kutoa mwelekeo wa kisheria na kisiasa kuhusu mwelekeo mpya wa Jumuiya ya Kimataifa, lakini linatoa mwono sahihi wa binadamu, maadili kwa ajili ya mafao ya wengi.

Hakuna uongozi bora unaojikita mikononi mwa watu wachache tu, wanaowatawala wengine pamoja na kuwanyonya maskini. Uongozi bora unajikita katika nguvu ya kimaadili, matumizi sahihi ya akili pamoja na kuwashirikisha wengine mintarafu uwezo na haki husika.

Baba Mtakatifu analishukuru Baraza la Kipapa la Haki na Amani pamoja na taasisi mbali mbali ambazo zimejitahidi kueneza ujumbe wa Waraka wake wa kichungaji, Upendo katika Ukweli, kama sehemu ya changamoto inayopania kuleta mabadiliko katika mfumo wa fedha kimataifa kama watakavyofanya wakati wa Semina ya Kimataifa kuhusu Waraka wa Papa Yohane wa Ishirini na tatu, Amani Duniani.

Mwishoni, Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, amehitimisha hotuba yake kwa kuwaweka wajumbe wa Baraza la Kipapa la Haki na Amani chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria, ili aweze kuwaongoza katika kutangaza na kushuhudia Mafundisho Jamii ya Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.