WAWATA ni matunda ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican; changamoto ya waamini walei
kuyatakatifuza malimwengu!
Ifuatayo ni risala ya Wanawake Wakatoliki Tanzania, WAWATA, wakati wa maadhimisho
ya maonesho ya Miaka 40 tangu ilipoanzishwa. Kwa ufupi, risala hii inagusia kwa ufupi:
historia ya WAWATA katika kipindi cha miaka 40 iliyopita, taswira, malengo pamoja
na utekelezaji wa utume wao ndani ya Kanisa na Jamii kwa ujumla.
Mwadhama Policarp
Kardinali Pengo Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Dsm na Rais wa SECAM, Mhashamu Askofu
Mkuu Francisco M. Padilla Balozi wa Baba Mtakatifu nchini Tanzania, Mhashamu Askofu
Desderius Rwoma –Mwenyekiti wa Idara ya utume wa Walei katika Baraza la Maaskofu Katoliki
Tanzania, Waheshimiwa Mapadri na Watawa wa Kike na Wakiume, Waheshimiwa Wageni
wetu kutoka nchi za nje Waheshimiwa Viongozi wote wa Halmashauri ya Walei Wageni
waalikwa, Wanawake Wakatoliki wote toka majimbo yote ya Tanzania. Mabibi na
Mabwana.
Kwa Upendo wa Kristo – Tutumikie na Kuwajibika!!
Kwa
heshima kubwa uongozi na Wanawake Wakatoliki Tanzania katika ujumla wetu , tunapenda
kuwasilisha Risala fupi itakayoonyesha maendeleo na changamoto mbalimbali tulizokutana
nazo katika kipindi cha miaka 40 tangu kuanzishwa kwake mwaka1972.
Awali ya
yote tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa baraka zake kwa WAWATA katika ngazi zote, tukianzia
ngazi ya Jumuiya ndogo ndogo, vigango, dekania, parokia, majimbo na hata Taifa zima
kwa ujumla. Tuna kila sababu ya kumtukuza Mungu katika kipindi hiki cha miaka 40 ya
uhai wa WAWATA katika Taifa letu.
Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Kwa namna
ya pekee tunakushukuru sana kwa kukubali kwako kutufungulia Maonesho haya baada ya
kuadhimisha nasi Misa ya ufunguzi hapo jana ambayo iliashiria kuanza rasmi kwa wiki
ya adhimisho la Kilele cha Miaka 40 ya WAWATA .
Aidha kwa nafasi ya sherehe
za Miaka 40 ya WAWATA ,tunawashukuru sana Baraza la Maaskofu ambao mwaka 1972 waliidhinisha
kuanzishwa kwa Chombo Hiki na kwa uongozi wao uliosaidia sana katika kuukuza umoja
huu hadi ukaenea majimbo yote ya Tanzania na kujulikana kimataifa .
Katika
vipindi mbalimbali Tumekuwa na Maaskofu wengi Wenyeviti wa Idara ya Utume wa Walei
pamoja na Makatibu wa Idara ya Utume wa Walei Baraza la Maaskofu wakiwemo mapadre
watawa na viongozi mbalimbali.Wote wamekuwa msaada mkubwa katika maendeleo ya WAWATA
katika ngazi mbalimbali. Pamoja na shukrani za dhati kwa hao wote WAWATA wanazidi
kuwaomba ushirikiano wao katika kipindi kipya cha Upendo kwa Vitendo.
Kwa
nafasi hii ya adhimisho la miaka 40 ya WAWATA na hasa kwa faida ya wageni na wale
wote ambao hawana picha ya hiki chombo kimeanzia wapi, ni vema tukaelezea kwa ufupi
sana WAWATA ni nini.
Wanawake Wakatoliki Tanzania (WAWATA) ni chombo cha Kanisa
Katoliki kilichoundwa kutokana na maazimio ya Mtaguso Mkuu wa pili wa Vatikano. Baada
ya azimio hili kutolewa katika Mtaguso huo, Kila nchi ilichukua na kuanza utekelezaji
kadiri muda na uelewa wa azimio hilo ulivyoruhusu na kuwafikishia waamini wake.
Kwetu
sisi Tanzania, umoja huu ulianza kuzama ndani ya mioyo ya watu mwaka 1972. Na nia
kuu ya kuanzishwa Umoja huu, ilikuwa kutoa fursa kwa Wanawake Wakatoliki kushiriki
na kushirikisha Utume wao katika Kanisa kama wanawake Wakristo kwa kutumia karama
na vipaji mbalimbali walivyojaliwa na Mungu kwa nia ya kulistawisha kanisa la Kristo
hapa duniani..
Taswira (vision): Taswira ya WAWATA ni kuona
kila mwanamke mkatoliki wa Tanzania anaelewa nafasi yake na wajibu wake wa Kikristo
kuanzia ngazi ya Familia, Jumuiya, Kanisa, jamii na Taifa kwa ujumla, pia wanakuwa
na maendeleo ya kiuchumi ili kukidhi mahitaji ya familia na michango ya maendeleo
ya Kanisa na Jamii, na kufanya maisha ya hapa duniani kuwa taa na nuru katika Ulimwengu
kama mawakili wa Yesu Kristo.
Malengo: Mwadhama Polycarp Kardinali
Pengo, Umoja huu ulipoanzishwa, ulijiwekea malengo ili kupata mwelekeo utakaotufikisha
mahali ambapo tunaweza kufanya tathmini ya Utume wetu katika kanisa na ukombozi mzima
wa mwanamke katika suala la kiroho, ujinga, umaskini na uwezo. Malengo yalikuwa kama
yafuatavyo:
Kumjenga mwanamke katika Imani thabiti ya Kikristo, aishi maisha
matakatifu, atakatifuze malimwengu.
Kumjengea uwezo
wa kujikomboa yeye na familia yake ili akomboe wengine wenye shida, yatima na wasiojiweza.
Kumwendeleza mwanamke kielimu na kiujuzi ili aondokane na giza la
kiroho, ujinga wa akili na aendeleze wengine
Kumwezesha
mwanamke katika maswala ya kiuchumi ili kutegemeza familia, kanisa na kuwategemeza
wengine.
Mafanikio na Changamoto: Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo,Wanawake
Wakatoliki Tanzania katika kipindi cha miaka 40,Tukitathmini tulivyoanza na sasa,
ni wazi kwamba tunamshukuru Mungu kwa hatua kubwa iliyofikiwa. Baadhi ya changamoto
tulizokabiliana nazo ni:
Kabla ya umoja huu kuanzishwa, kulikuwa hakuna
ushirikishwaji wowote wa utume wa wanawake katika Kanisa – Leo hii wanawake wanashirikishwa
katika kuinjilisha, mikutano ya kanisa, Uongozi wa kanisa na mambo mengi ya maamuzi
katika kanisa.
Umoja huu ulipoanza, mfumo wa uongozi
ulianzia Taifani, na kupatikana viongozi haikuwa rahisi, katika juhudi za kuwaelimisha
wanawake nafasi yao na wajibu wao katika Kanisa, uongozi uliingia katika ngazi ya
majimbo, pole pole maparokiani, vigangoni na sasa uongozi umepenya mpaka kwenye jumuiya
ndogo ndogo kuhakikisha kuwa Utume wa mwanamke mkatoliki katika kanisa unamfikia
kila mwanamke mbatizwa katika kanisa la mahali.
Swala
la malezi ya watoto na vijana, wanawake walizoea kulelea kwenye ngazi ya familia zaidi,
lakini leo hii, wanawake wameshika hatamu ya malezi kwenye Jumuiya ndogo ndogo, wanafadhili
seminari zetu, vituo vya watoto yatima na vituo vingine vya malezi kwa ushirikiano
mkubwa na watawa wa kike.
Swala la maendeleo ya jamii
na uchumi, wanawake walizoea zaidi kazi za nyumbani, kilimo na ufugaji lakini leo
pamoja na hizo, wanawake wamejikita katika ujasiriamali mdogo na mkubwa ambao umekuwa
kichocheo kikubwa cha maendeleo na uchumi wa nchi.
Leo katika maonesho
ya kazi za wanawake wakatoliki umeona juhudi walizo nazo katika majimbo yote katika
nyanja zote za Utume katika kanisa na maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.
Katika
Utume wa Kanisa:
Majimbo yameonesha uwajibikaji wa matendo ya huruma,
kufundisha watoto na vijana, ushiriki katika jumuiya ndogo ndogo, mafungo, hija mbalimbali,
makongamano, kutembelea vituo vya yatima, magereza na wagonjwa, kutegemeza seminari
zetu, kushiriki michango mbalimbali ya ujenzi wa makanisa pia kuwatia moyo vijana
wetu wanaopata madaraja ya kanisa na kuwekwa wakfu kwa kuwazawadia zawadi mbalimbali,
matoleo ya vipaji mbalimbali kwa ajili ya watumishi wa Mungu
Katika maendeleo
na Uchumi: Majimbo yameonesha: Mahudhurio ya vikao na mikutano ya maamuzi, uanzishwaji
wa mifuko ya kuweka na kukopa, ujenzi wa vituo vya mafunzo na shule za watoto wadogo,
miradi ya WAWATA kiparokia, kijimbo na kitaifa, aidha tunachukua fursa hii kuwashukuru
sana wafadhili wetu wa nje ya nchi, akiwemo Mr.Viliger ambaye yupo hapa leo kwa mbegu
ya ‘Revoling Fund’ waliotupatia ambayo kwa uhakika ilitupa hatua nzuri ya kuingia
katika ujasiriamali. Wanawake ambao hawakuwa na jinsi ya kujikwamua katika umaskini,
Mbegu hii ilikuwa ukombozi na leo hii wanawake wengi wana viwanda vyao, maduka, mashule
na biashara nyinginezo kwa kupitia msaada huu. Ijapokuwa wapo walioshindwa kutembea
na mfuko huu, lakini asilimia kubwa walifanikiwa na baadhi ya mafanikio umeyaona kwenye
maonesho yetu.
Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Maendeleo ya WAWATA katika
kipindi hiki cha miaka 40, si rahisi kuweza kuyaandika yote ila hatutasahau ushirikiano
tulio nao na vyama vingine vya kanisa na Serikali ambavyo vimekuwa kama daraja kuu
la kuwafikia wanawake wengi katika kanisa na makanisa na Taasisi mbalimbali ambazo
aidha wanatupatia huduma sisi au WAWATA wanapeleka huduma.
Mwadhama Polycarp
Cardinal Pengo,utayari wako wa kuwa nasi katika tukio hili muhimu unatutia moyo sana
moyo sana sisi WAWATA katika Utume wetu. Adhimisho hili la miaka 40 tulilizindua
rasmi Mwezi Septemba 2011 .Katika kipindi hiki adhimisho hili limefanyika nchi nzima
katika ngazi zote za kanisa katoliki Tanzania kwa mambo yafuatayo:
Tafakari
za Kiroho
Tafakari za kina za kiroho kuhusu kauli Mbiu ya adhimisho ambayo
ni “Upendo kwa Vitendo-love in action” kauli mbiu ambayo Wanawake Wakatoliki Dunia
nzima Tuliipitisha katika Adhimisho la Miaka 100 ya Umoja wa Jumuiya za Wanawake
Ulimwenguni lilifanyika huko Israel mwaka 2010 .Upendo ni Mhimili wa mafundisho ya
Bwana wetu Yesu Kristu na hakika binadamu tukiishi kwa Upendo Amani na maelewano vitajengeka.
Tunashukuru sana Kwamba Balozi wa Baba Mtakatifu amekubali Kufungua rasmi Tafakari
yetu ya kuhitimisha Miaka 40 siku ya Ijumaa tarehe 28/9/2012 itakayowawezesha WAWATA
kuandaa Mkakati wa Utekelezaji wa miaka mitano ijayowa kiongozwa na kauli Mbiu y a
Upendo kwa Vitendo. Aidha tunamshukuru sana Balozi wa Baba Mtakatifu nchini Tanzania
kwa kukubali kuadhimisha Misa ya kilele cha adhimisho letu kumshukuru Mungu na
kumtukuza Somo wetu Bikira Maria Msaada wa Wakristu itakayofanyika katika kanisa
kuu la Mt Yosefu siku ya Jumapili tarehe 30/9/2012.
Hija katika
sehemu Takatifu
Moja ya matukio muhimu katika sherehe za miaka 40 ya WAWATA
ni Hija za WAWATA sehemu mbalimbali takatifu nchini na nje ya nchi .Ofisi ya WAWATA
taifa ilifanikiwa kuratibu hija ambayo ilijumlisha maeneo matatu:Vatikano-Roma ambapo
mahujaji walionana na Baba Mtakatifu benedicto wa 16, Lurdis ambako Bikira Maria alimtokea
Mt.Bernadetta na Israel.Tunawapongeza WAWATA majimbo yote katik a ushiriki wao katika
hija mbalimbali
Matendo ya Huruma
Katika adhimisho
hili mwaka Mzima WAWATA walifanya matendo ya Huruma kuwasaidia wasijiweza katika jamii
nzima kwa hali na mali.Aidha walishiriki pia katika kufadhili seminari na vituo kadhaa
vya kanisa vinavyohudumia wahitaji.
Maonesho ya kazi ya Utume
wa WAWATA
Maonesho ya kazi za utume wa WAWATA kama ulivyojionea yanaainisha
kazi mbalimbali za WAWATA mathalani Miradi mbalimbali ya kumkomboa mwanamke katika
umaskini, Uinjilishaji ,Ushiriki wa Mwanamke Mkatoliki katika shughuli za kijamii
pamoja na Wanawake Wakatoliki wanavyoshiriki katika kulitegemeza kanisa na Taifa letu
kwa ujumla.
Ushiriki katika Kujadili katiba ya jamhuri
ya Muungano wa Tanzania
Uongozi wa WAWATA katika adhimisho hili utapata
fursa ya kujadili Katiba ya Nchi yetu ili kuwaandaa kushiriki kikamilifu fursa waliyopewa
ya kushiriki mchakato huo ili katiba yenye kukidhi matakwa ya watanzania na yenye
kuzingatia mpango wa Mwenyezi Mungu iweze kupatikana.
Hitimisho: Tunamshukuru
sana Mwenyezi Mungu kwa hayo yote aliyotujalia, tunaomba atusaidie kusiwepo na kurudi
nyuma bali tusonge mbele zaidi na zaidi tukizidi kuleta mshikamano wa wanawake wakatoliki
wote pia wanawake wa madhehebu ambako WAWATA ni moja katika umoja wa Wanawake wa Madhehebu
ya Kikristo kitaifa na majimboni .
Kwa namna ya pekee, tunakushukuru sana Mwadhama,Balozi
wa Baba Mtakatifu pamoja na Waandamizi mliofuatana nao kwa kuutoa muda wenu kwa ajili
yetu siku hii ya leo, tukijua wazi kuwa mna shughuli nyingi za Kichungaji. Mwenyezi
Mungu awabariki sana na kuwajalia maisha marefu yenye amani tele.
Tunawashukuru
watu wote,pamoja na wageni kutoka nchi za nje, Kenya, Uganda, Malawi na Zambia, walioacha
shughuli zao wakaja kuungana nasi katika tukio hili kuu la WAWATA kutimiza miaka 40.
Mungu awabariki sana. Wabarikiwe pia WAWATA wote waliojitoa kwa hali na mali katika
kufanikisha shughuli hii, Mungu awabariki na kuwafanikisha katika malengo yenu.
Tunawashukuru
sana Waasisi wa Umoja huu pamoja na Viongozi wote waliokwisha pitia katika ngazi
mbalimbali ambao leo tunasifu kazi zao na mafanikio kwa hii miaka 40. Mungu awazidishie
neema zake popote walipo.