2012-11-28 08:29:52

Maandalizi makini yanahitajika kabla ya kupokea Sakramenti za Kanisa


Mpendwa msilizaji wa Radio Vatican, karibu tena katika mfululizo wa vipindi vyetu vya Uinjilishaji wa kina tukiendelea bado kuchambua Mwongozo wa maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya. Juma hili tuendelee na sehemu ya mchakato mzima wa uinjilishaji katika kuwaingiza Watu wa Mungu katika Ukristo. RealAudioMP3

Uenezaji wa Imani katika ulimwengu unaobadilika kila siku unaleta changamoto nyingi katika ulimwengu wa Ukristu. Hali imepelekea katika Kanisa kuwepo kwa majadiliano ya Kina juu ya changamoto hizo jambo ambalo limepelekea kuitishwa kwa Sinodi maalum juu ya tema hii ya Uinjilishaji Mpya. Nyaraka zilizotolewa katika Mtaguso Mkuu wa pili wa Vatican sasa yametimia machoni pa Kanisa.

Sakramenti za kuingiza watu katika Ukristo yaani: Ubatizo, Kipaimara na Ekaristi Takatifu hivi sasa si Sakramenti tofauti tena miongoni mwa Waumini bali zimeunganishwa na kuwa hatu kuu tatu msingi za kumwingiza mtu katika Imani ya Kikristo. Hii ni hatua muhimu sana iliyofikiwa na Kanisa mahali ambapo Waumini wanazielewa barabara sakramenti hizi msingi katika maisha yao.

Katika mchakato huu, bado kuna kutofautiana katika maadhimisho ya sakramenti hizi pia kuna changamoto nyingi zitokanazo na umuhimu wa sakramenti hizi katika Kanisa kati ya Kanisa la Magharibi na lile la Mashariki. Pia bado kuna dukuduku hususan juu ya ubatizo wa watoto wadogo na uhuru wa mtu kuchagua imani anayoitaka.

Tofauti hizi zinatoa mwaliko kwa Kanisa kutoa majibu ya kufaa yanayokidhi haja ya wanafamilia ya Mungu kiulimwengu. Hivyo Kanisa linaalikwa kufanya upya tathmini ya namna ya kumwingiza mtu Ukristo likizingatia umoja wa Kanisa kiulimwengu. Bado pia kuna changamoto hata ya namna ya maadhimisho ya mafumbo na ibada za Kikristu mintarafu maswala ya Liturujia na lugha ya kutumia. Kuna mvutano kati ya wanafamilia ya Mungu ambao unahitaji tathmini na kutolea majibu ya wazi ya kiteologia, kiimani na kimapokea.

Ulimwengu wa leo bado unaleta changamoto nyingine kwa wanafamilia ya Mungu yaani pale wanapojitokeza watu wengine katika mijadala ya mambo ya Mungu. Wanafamilia ya Mungu, walio wengi wanashindwa kujibu maswali katika mijadala kama hii na kubaki kukaa kimya na kushindwa kabisa kuitetea imani yao hali ambayo imepelekea wengi kunaswa na madhehebu mengine kwa kufikiri kuwa kule wanapata majibu sahihi kuhusu imani yao.

Aidha, kukosekana kwa Katekesi ya kina mtu anapoingizwa Ukristo kumepelekea kuwa na wanafamilia ya Mungu wasiokomaa kiimani na mara wanaokumbwa na changamoto kimaisha na kiimani hubabaika na kurudi nyuma.

Hati hii imelitaka Kanisa kubuni mbinu itakayoliwezesha Kanisa kwajenga Waamini wake kiimani na pia kimafundisho. Utangazaji wa Neno la Mungu kwa mara ya kwanza kwa watu ambao hawajaisikia kabisa imani lazima ufuatane na Katekesi ya kina ili kuweza kuwakomaza kiimani watoto wapya katika Kanisa.

Katekesi mbali na utangazaji wa Neno itasaidia mchakato mzima wa wongofu wa mtu kumwelekea Mungu. Hivyo makanisa mahalia yamealikwa kupokea mwongozo utakaotolewa na Mababa wa Sinodi, na kuketi chini na kuona namna gani kulingana na hali na mazingira ya Kanisa mahalia wanaweza kufanya uenezaji wa imani uzae matunda yaliyokusudiwa.

Wakati umefika ambapo lazima Wanafamilia ya Mungu wazoee kwanza kabisa kuongea juu ya Imani yao mbele ya watu wengine wenye mtazamo kidogo tofauti na wao au hata kwa wenzao wenye njaa ya kutaka kujiimarisha zaidi kiimani. Tofauti na mtindo wa zamani kidoko ambapo Wachungaji tu ndio waliotegemewa kutoa majibu juu ya maswali ya kiimani sasa Kanisa lazima liwandae vema watoto wao kuweza kucheza kwa uhuru na watoto wengine bila kuwa na hofu.

Kwa upande wa Wanafamilia ya Mungu wakati umefika kufungua mioyo yao na kujikita moja kwa moja katika mchakato mzima wa uinjilishaji kwa wao wenyewe kujibidisha kufahamu fika angalau yale ya msingi ambayo kimsingi ndiyo yanayoulizwa na wengi mitaani.

Mpenzi msikilizaji wakati ukuta, ukishindana nao utaumia! Hadi hapa tumefikia mwisho wa makala yetu kwa siku ya leo. Nakutakia kila neema na Baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Kutoka Studio za Radio Vatican ni mimi mtayarishaji na msimulizi wako Padre George wa Bodyo.










All the contents on this site are copyrighted ©.