Mkutano wa Kimataifa kuhusu athari za mabadiliko ya tabianchi wafunguliwa mjini Doha,
Qatar
Wajumbe kutoka nchi mbali mbali wanakutanika mjini Doha, Qatar, kujadili kwa mara
nyingine tena, mikakati ya kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi duniani
kwa kuziwezesha Nchi zinazoendelea kukabiliana na majanga haya ambayo yameendelea
kuwa ni sababu ya umaskini kwa watu wengi duniani. Katika kipindi cha miaka zaidi
ya kumi, Jumuiya ya Kimataifa imekuwa ikijadili mikakati ya kupunguza athari za mabadiliko
ya tabianchi lakini bila mafanikio.
Juhudi hizi ziligonga mwamba wakati wa
mkutano wa Copenhagen, miaka mitatu iliyopita, wakagonga mwamba tena mwaka 2011, sasa
wamejipanga ili kuweza kufikia muafaka ifikapo mwaka 2015.
Mambo kadhaa yanapaswa
kupatiwa ufumbuzi, ikiwa ni pamoja na kujipanga kubeba gharama kubwa ili kupunguza
uzalishaji wa hewa ya ukaa kati ya nchi tajiri duniani na nchi maskini. Wajumbe wanaangalia
pia uwezekano wa kurefusha Itifaki ya Kyoto, kwa ajili ya nchi tajiri zaidi duniani
sanjari na kutafuta fedha zitakazotumika kwenye nchi changa duniani, kama njia ya
kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Lengo ni kuhakikisha kwamba,
dunia inakuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi hata kwa siku za usoni. Wanaharakati
na watunza mazingira wanabainisha kwamba, mazungumzo ya Umoja wa Mataifa kuhusu mikakati
ya kudhibiti athari za mabadiliko ya tabianchi yanakwenda mwendo wa "Kinyonga".
Mkutano
wa mabadiliko wa kudhibiti mabadiliko ya tabianchi umefunguliwa Jumatatu, tarehe 26
Novemba 2012. Mafuriko, vimbunga, ukame wa kutisha ni kati ya mambo ambayo yatakuwa
na athari kubwa katika maisha ya watu na harakati za maendeleo kwa ujumla, kama inavyojionesha
katika kipindi cha miaka ya hivi karibuni.
Nchi wanachama wa Jumuiya ya Ulaya
wanaounda asilimia kumi na tano ya wazalishaji wakubwa wa hewa ya ukaa, wanaonekana
kuunga mkono wazo la kuendeleza Itifaki ya Kyoto. Marekani ilipinga Itifaki ya Kyoto,
kwa vile China na India ambao pia ni wazalishaji wakuu wa hewa ya ukaa hawakuwekewa
masharti yoyote. Wao wanataka majadiliano kuhusu uthibiti wa hewa ya ukaa yawe katika
ngazi sawa sawa, ili kuweza kupitisha Itifaki mpya.
China na India inashikilia
msimamo wake kwamba, tatizo la uzalishaji wa hewa ya ukaa ambayo inatishia maisha
na usalama wa dunia ni matokeo ya uzalishaji mkubwa viwandani unaofanywa na Marekani
pamoja na nchi mbali mbali za Bara la Ulaya. Nchi hizi zinaomba kuruhusiwa kuendelea
kuzalisha hewa ya ukaa kwani ndiyo zinaanza kuchipukia katika masuala ya maendeleo
sanjari na kupania kuwainua watu wengi kutoka katika baa la umaskini.