2012-11-26 07:30:13

Jumuiya ya Kimataifa inapaswa kutoa haki msingi katika udhibiti wa athari za mabadiliko ya tabianchi


Mashirika mbali mbali ya Misaada na Maendeleo ya Kanisa Katoliki Kimataifa, yanasema kwamba, Mkutano wa Kimataifa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi unaoanza huko Doha, nchini Qatar, kuanzia tarehe 26 Novemba hadi tarehe 7 Desemba 2012, iwe ni fursa ya kuweka mikakati makini na endelevu ya kifedha inayolenga kuzisaidia nchi zinazoendelea kukabiliana kikamilifu na athari za mabadiliko ya tabianchi, ili hatimaye, kufikia muafaka wa Kimataifa, ifikapo mwaka 2015.

Wajumbe wanapaswa kuweka mikakati ya haki, usawa na inayotekelezeka pamoja na kutoa mbinu mkakati utakaotumiwa na Jumuiya ya Kimataifa, ili kufikia malengo yatakayokuwa yamefikiwa, vinginevyo ni kupoteza muda na rasilimali, wakati ambapo kuna maelfu ya watu wanaendelea kuathirika kutokana na mabadiliko ya tabianchi.

Udhibiti wa madhara haya ni jukumu la Jumuiya ya Kimataifa, lakini kwa namna ya pekee, Nchi zilizoendelea zinapaswa kuonesha mfano wa kuigwa kwa kupunguza uzalishaji wa hewa ya ukaa inayotoka viwandani mwao, ambayo imekuwa ni chanzo kikubwa cha athari ya mabadiliko ya tabianchi.

Mashirika ya Misaada na Maendeleo ya Kanisa Katoliki Kimataifa yanasema, hadi sasa Itifaki ya Kyoto ndicho chombo pekee kinachofanya kazi ya kudhibiti hewa ya ukaa, mwaliko kwa Jumuiya ya Kimataifa kujikita zaidi katika utekelezaji wa malengo ya Itifaki hii itakapokuwa inaingia katika Awamu ya Pili, hapo mwaka 2013.

Hadi sasa hakuna rasilimali wala utashi wa kisiasa unaotaka kulivalia njuga tatizo la athari za mabadiliko ya tabianchi, wakati ambapo kiwango cha nyuzi joto kinaendelea kuongezeka. Jumuiya ya Kimataifa haina budi kutekeleza maamuzi yake. Ili kudhibiti athari za mabadiliko ya tabia nchi, vinginevyo, majanga asilia yataendelea kusababisha umaskini, vurugu na kinzani za kijamii, kisiasa na kivita.








All the contents on this site are copyrighted ©.