Kanisa ni: Moja, Takatifu, Katoliki na la Mitume, linapata chimbuko na hija yake kwa
njia ya Umoja katika Fumbo la Utatu Mtakatifu
Kanuni ya Imani inayoungamwa na Waamini katika Liturujia ni muhtasari wa Imani ya
Kanisa ambayo kila mwamini anaipokea wakati anapobatizwa. Kwa kuiungama na kuilinda,
waamini wanaweza kuwa kweli ni wafuasi wa Kristo.
"Katoliki" ni neno linaloonesha
umuhimu wa Kanisa na utume wake, kwani ni Yesu mwenyewe kwa njia ya Roho Mtakatifu
anayeliwezesha Kanisa lake kuwa ni: Takatifu, Katoliki na la Mitume pamoja na utekelezaji
wake. Kanisa ni Katoliki kwani kwa njia yake, Yesu anawakumbatia binadamu wote katika
utume wake kwa njia ya mwanga wa Injili unaoyaunganisha mataifa yote katika Ufalme
wa Mungu. Huyu ndiye Mwana wa Daudi, lakini zaidi ni Mwana wa Mtu, kama anavyotambulikana
katika Maandiko Matakatifu.
Hivi ni vielelezo makini anavyovitumia Yesu kuonesha
utume wake wa kama Masiha wa ulimwengu wote. Kwa njia ya ubinadamu wake, anawavuta
wote kuungana na Mwenyezi Mungu kwa njia ya Kanisa ambalo ni kielelezo cha umoja na
mshikamano wa kweli.
Hii ni sehemu ya tafakari ya Baba Mtakatifu Benedikto
wa kumi na sita, aliyoitoa wakati wa kuwasimika Makardinali wapya sita katika Ibada
iliyofanyika Jumamosi, tarehe 23 Novemba, 2012 kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro
mjini Vatican. Yesu analituma Kanisa lake kwenda ulimwenguni kote, ili kuwaunganisha
watu katika kifungo cha imani na hatimaye, kuwa ni Watoto wa Mungu, kama wanavyobainisha
Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican. Watoto hawa wanapaswa kujenga na kuimarisha
umoja wao hadi pale utashi wa Mungu utakapokamilika.
Baba Mtakatifu anasema,
Ukatoliki wa Kanisa unapata chimbuko lake katika Mpango wa Kazi ya Ukombozi wa dunia,
hali ambayo ilijionesha kwa namna ya pekee, pale Roho Mtakatifu alipowashukia Wakristo
wa Kanisa la Mwanzo, ili Injili iweze kuwafikia watu wengi zaidi, ambao wangefanyika
kuwa ni Watoto wa Mungu, ndiyo maana hata Kanisa katika utume wake, linawakumbatia
wote na kila mtu anaielewa lugha yake kama walivyoshuhudia Mitume siku ile ya Pentekoste.
Utume wa Kanisa la Kiulimwengu unapania kuunda umoja wa Watu wa Mungu, huku
wakitoka kifua mbele kutangaza Habari Njema ya Wokovu, ili ufalme wa Mungu uweze kuwafikia
wote. Kwa njia ya Roho Mtakatifu anasema Baba Mtakatifu waamini wamekirimiwa Mapaji
ya Roho Mtakatifu, wakipewa wajibu na dhamana ya kumshuhudia kwa mataifa yote sanjari
na kujenga ufalme wa Mungu.
Tangu mwanzo wa Kanisa, mitume na wafuasi wao hawakutegemea
usalama katika nguvu za kibinadamu, bali waliongozwa na kutegemezwa na nguvu ya Roho
Mtakatifu, Injili na Imani, wakafanikiwa kuingia katika medani mbali mbali za maisha
ya mwanadamu, lakini Kanisa daima likabaki kuwa ni MOJA. Makanisa mahalia yakaanzishwa
na kuenea sehemu mbali mbali za dunia, lakini bado Kanisa likabaki kuwa ni Kanisa:
Moja, Takatifu, Katoliki na la Mitume, linalopata chimbuko lake la maisha na hija
yake kwa njia ya Umoja katika Fumbo la Utakatifu Mtakatifu.
Baba Mtakatifu
Benedikto wa kumi na sita, anasema, huu ndio mwelekeo wa Baraza la Makardinali, wanaoonesha
sura tofauti za Kanisa, lakini wote kwa pamoja wanaunda Kanisa la Kiulimwengu, ambalo
ni la waamini wote kutoka katika mabara yote, kielelezo cha Kanisa la Pentekoste,
linaloimba utenzi kwa Mungu aliye hai.
Baba Mtakatifu alitumia fursa hii pia
kuwasalimia wawakilishi kutoka sehemu mbali mbali za dunia, waliofika mjini Vatican
kushuhudia Makardinali wapya wakisimikwa rasmi, kielelezo cha mshikamano na ushirikiano
wa kibaba na kirafiki; tayari wakiwa makini kutoa huduma yao ya kichungaji kwa Makanisa
mbali mbali yaliyoko mjini Roma ili kuendelea kujenga na kuliimarisha Kanisa la Kristo,
kama walivyoapa katika kiapo cha utii kwa Khalifa wa Mtakatifu Petro.
Makardinali
wanapaswa kuendelea kuwa waaminifu kwa Kristo pamoja na Kanisa Takatifu. Wawe tayari
hata kuyamimina maisha yao, kama inavyojionesha kwa njia ya Kofia Nyekundu za Kikardinali
wanazovaa; lengo ni kueneza Imani ya Kikristo, kwa ajili ya kusimama kidete kuinda
na kutetea amani na utulivu wa Watu wa Mungu.
Pete ambayo Makardinali wamevishwa
na Baba Mtakatifu ni alama ya uaminifu na upendo wao kwa Kanisa; daima wakiwa wameungana
na Khalifa wa Mtakatifu Petro na kwa ajili ya huduma kwa watu wa Mungu, kwani Kanisa
la Roma ni kielelezo cha upendo wa Kanisa Katoliki. Watashirikiana kwa karibu zaidi
na Mabaraza mbali mbali ya Kipapa na kwa njia hii, wanakuwa ni wasaidizi wake wa karibu
katika kuchunga na kuliongoza kundi la Kristo kwa kuwa makini katika Mafundisho tanzu
ya Kanisa, Nidhamu na Maadili.
Kwa njia ya karama na mapaji mbali mbali waliyokirimiwa
Makardinali wapya, watachangia utajiri wa Kanisa la Kristo, daima wakijitahidi kutolea
ushuhuda amini wa imani na huduma yao kwa Kristo na Kanisa lake.