Juhudi za Serikali ya Tanzania katika maboresho ya mafunzo katika sekta ya afya
Rais Jakaya Mrisho Kikwete wa tanzania, Ijumaa Novemba 23, 2012 amepokea taarifa ya
maendeleo ya ujenzi wa Kampasi mbili za tiba ya afya vinavyojengwa katika Chuo Kikuu
cha Dodoma na Mloganzila huko Kisarawe, ambavyo pia vitatumika kama hospitali hapa
nchini. Kwanza Rais amepokea maendeleo ya ujenzi wa Kampasi ya Afya ya Chuo Kikuu
cha Dodoma kutoka kwa Mkurugenzi wa Mfuko wa Afya ya Jamii (National Health Insurance
Fund) NHIF Bw. Emmanuel Humba .
Ujenzi wa kampasi hii umeshaanza na kufikia
hatua ya juu na hospitali inatarajiwa kuanza shughuli zake rasmi mwaka 2015. Kulingana
na Bw. Humba, maandalizi ya kufanikisha uanzishaji wa Chuo/ Hospitali hiyo vimeshaanza
ambapo baadhi ya wataalamu wakiwemo Madaktari na watumishi wengine wako nchini na
nje ya nchi kwa ajili ya masomo na mafunzo mbalimbali. Chuo hicho kinatarajia kuwa
na vifaa vya kisasa vya tiba vinavyokidhi mahitaji ya Afya na Elimu ya Udaktari wa
kiwango cha Kimataifa.
Rais pia amepokea taarifa ya maendeleo ya ujenzi wa
Kampasi ya Mloganzila ambapo katika ujenzi na uanzishwaji wa Kampasi hizi zote, Rais
Kikwete amesimamia kuanzia hatua za awali. Kampasi ya Mloganzila ambayo ni sehemu
ya Hospitali kuu ya Muhimbili inajengwa kwenye eneo la ekari 3800 na itakua sehemu
ya kutolea mafunzo kwa wanafunzi wa udaktari na huduma za Afya, lakini pia itakua
sehemu ya kutolea matibabu ya maradhi yote makuu na ya kawaida nchini. Ujenzi wa
Hospitali hii unatarajiwa kuanza mwishoni mwa mwezi Januari, 2013 na unatarajiwa kukamilika
miaka miwili baada ya ujenzi.
Katika hafla hiyo Makamu Mkuu wa Chuo cha Afya
na Sayansi Shirikishi Muhimbili Prof. Ephata Kaaya ametumia nafasi hiyo kumkabidhi
Rais Kikwete Cheti cha Udaktari wa Public Health (Honoris Causa), kufuatia Shahada
aliyotunukiwa na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi, Muhimbili Disemba, 2010
kwa Kutambua mchango wa Rais Kikwete katika kuendeleza Sekta ya Afya nchini.
Akitoa
taarifa hiyo ya maendeleo kwa Rais Kikwete, Prof. Kaaya amesema tayari wataalamu na
wafanyakazi wanaotarajiwa kufanya kazi katika kampasi ya Mloganzila wameshaanza mafunzo.
Mara hospitali hiyo kubwa na ya kisasa itakapokamilika itakua na uwezo wa vitanda
vya kulaza wagonjwa mia sita (600). Rais Kikwete amewapongeza wataalamu wote kwa juhudi
zao na kuwa ahidi kuwa lengo lake ni kuhakikisha nchi inaondokana na adha ya kupeleka
wagonjwa nje ya nchi kwa ajili ya matibabu.
Rais amesema moja ya lengo kubwa
la serikali yake, ni kutoa kipaumbele katika sekta ya Afya ili kuhaklikisha watanzania
wanapata huduma bora, kupanua mafunzo ya Afya na kuongeza wataalamu watakaoweza kutibu
magonjwa yote makubwa hapa hapa nchini. Rais amewaahidi watendaji wa Kampasi zote
mbili kuwa atahakikisha ujenzi wa huduma hizi muhimu kwa Umma haukwami kwa sababu
ya ukosefu wa pesa kwani ni jambo ambalo amedhamiria.