2012-11-23 08:22:01

Nigeria tumieni vyema utajiri na urithi wenu wa kiimani kupambana na: ujinga, umaskini, maradhi, rushwa na ufisadi!


Kardinali mteule John Olorunfemi Onaiyekan wa Jimbo kuu la Abuja, Nigeria, Alhamsi tarehe 22 Novemba 2012 alipata nafasi ya kuzungumza na waandishi wa habari mjini Roma. RealAudioMP3

Pamoja na mambo mbali mbali aliyoyazungumzia kuhusu maisha na utume wa Kanisa nchini Nigeria, ametumia fursa hii kumshukuru Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwa kuendelea kuthamini ukomavu wa Kanisa Barani Afrika.

Hii ni changamoto kubwa kwa Kanisa Barani Afrika kuhakikisha kwamba, waamini wanajenga na kuimarisha Kanisa ambalo limekita mizizi yake katika Imani na ushuhuda wa maisha unaomwilishwa katika medani mbali mbali mintarafu kweli za Kiinjili.

Kardinali mteule Onaiyekan anasema, Injili ya Kristo inasimikwa katika misingi ya haki, amani na upendo. Huu ndio ushuhuda unaopaswa kumwilishwa katika sekta mbali mbali za maisha na utume wa waamini Barani Afrika; kwa kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa.

Akizungumzia kuhusu hali tete nchini Nigeria, Kardinali mteule Onaiyekan anabainisha kwamba, usalama wa raia na mali zao ni kati ya changamoto pevu nchini Nigeria. Hii inatokana na ukweli kuhusu mashambulizi ya kinyama yanayofanywa na Kikundi cha Boko Haram, ambayo kwa namna moja au nyingine yanafumbatwa katika masuala ya kidini. Hata katika mazingira hatarishi kama haya Injili ya Kristo haina budi kutangazwa.

Ikumbukwe kwamba, tangu mwanzo wa kuanzishwa kwa Kanisa limekumbana daima na madhulumu na kwamba, damu ya Wakristo imekuwa ni chachu ya kukua na kukomaa kwa Kanisa ambalo linaendelea kufuata nyayo za Muasisi wake, Yesu Kristo, aliyekabiliana na kifo uso kwa uso.

Dhuluma ni nyenzo inayosaidia kukuza na kuliimarisha Kanisa, kumbe si bure hata kidogo! Jambo la msingi ni kuhakikisha kwamba, katika kipindi hiki cha mpito Wakristo wanakuwa na Imani thabiti na sahihi na wahakikishe kwamba, wanaishuhudia mahali popote pale walipo.

Kardinali mteule anapenda kukazia: umoja, upendo, amani na mshikamano wa kitaifa na udugu, miongoni mwa wananchi wote wa Nigeria. Licha ya tofauti zao za kidini, lakini kama raia wa Nigeria kuna mambo mengi ambayo yanawaunganisha kwa pamoja, huku wakiendelea kuchota utajiri na fadhila za kidini; ili wote kwa pamoja, waweze kusimama kidete kupinga: ujinga, umaskini, maradhi na utawala mbaya; daima wakipania kutafuta mafao ya wengi.







All the contents on this site are copyrighted ©.