2012-11-23 08:02:56

Maaskofu walaani vita na dhuluma inayoendelea nchini DRC


Maaskofu Katoliki kutoka sehemu mbali mbali za Kanisa Barani Afrika katika mkutano unaozungumzia utambulisho wa Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki, Caritas, katika ujumbe wao kwa Jumuiya ya Kimataifa wanasema kwamba, wanasikitishwa na mahangaiko ya watu wanaokabiliana na vita mjini Goma, DRC na kwamba, kwa kauli moja wanalaani vita hii ambayo haina tija wala mafao kwa wananchi wa DRC.

Vita hii imepelekea watu wengi kuyakimbia makazi yao na hivyo kukabiliana na hali mbaya ya hewa, njaa na udhalilishaji wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto pamoja na kuwateka watoto ili kuwapeleka mstari wa mbele kinyume cha sheria na kanuni za kimataifa. Vitendo vyote hivi vinadhalilisha utu na heshima ya watu hawa ambao wamumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Caritas Goma inakisia kwamba, kuna zaidi ya watu laki moja ambao wamelazimika kuyakimbia makazi kwa kuhofia usalama wa maisha yao.

Maaskofu kutoka Afrika wanasema, huu si muda wa kupigana vita, bali kujenga mshikamano na ushirikiano wa dhati miongoni mwa wananchi, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wote wa DRC, kila mtu akiheshimiwa na kulindwa. Inasikitisha kuona kwamba, utajiri wa maliasili badala ya kuleta mafao kwa wengi, umekuwa ukitumiwa na watu wachache kwa ajili ya mafao yao binafsi.

Maaskofu wanasema, umefika wakati wa kuhakikisha kwamba, kunakuwepo na usawa, haki na, ukweli na uwazi katika matumizi ya maliasili ya taifa, ili iweze kuwa ni kikolezo cha maendeleo. Maaskofu wanaiomba Jumuiya ya Kimataifa kuhakikisha kwamba, pande zinazosigana nchini humo zinajikita katika majadiliano ili kusitisha na hatimaye kukomesha kabisa vita nchini DRC na wahusika wafikishwe kwenye mkondo wa sheria.







All the contents on this site are copyrighted ©.