2012-11-23 08:58:40

Hii ndiyo Imani Yetu inayosimikwa kwa Kristo na Kanisa lake!


Kardinali Jaime Ortega Alamino, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Havana Cuba, katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani, ameandika barua kwa Familia ya Mungu Jimbo kuu la Havana, akionesha umuhimu wa Imani. Anapembua kwa kina na mapana mwelekeo wa imani nchini Cuba kwa kuwataka waamini kujikita katika kuifahamu, kuishuhudia na kuitetea imani yao kwa Kristo na Kanisa lake.

Anasema, katika ulimwengu wa utandawazi, watu wanaendelea kuonja mtikisiko wa maadili na utu wema; watu wanatake kuishi kana kwamba, hakuna Mungu; wakiongozwa na kusukumwa na mawazo mepesi mepesi bila ya kufanya rejea kwa Mwenyezi Mungu ambaye ni muumbaji wa vile vinavyoonekana na vile visivyoonekana. Walimwengu wanajidai kutaka kuanzisha mchakato mpya wa kanuni maadili, usiotaka kumshirikisha Mwenyezi Mungu asili ya wema na utakatifu wa maisha; wanataka kumnyamazisha Mungu kutoka katika undani wa dhamiri zao.

Kardinali Jaime Ortega Alamino anakazia kwamba, katika mazingira kama haya, kuna haja kwa waamini kusimama kidete kuiungama Imani ambayo inarutubishwa kwa akili, vinginevyo, imani hiyo inaweza kugeukwa kuwa ni vionjo na hali ya mtu kujisikia; matokeo yake ni imani kupoteza dira na mwelekeo na kuanza kuwa ni chanzo cha kero na vurugu ndani ya Jamii, kama inavyojionesha katika baadhi ya makundi ya waamini wa dini mbali mbali duniani. Hii ni imani inayounda makundi ya waamini wenye siasa kali, wanaosukumwa na vionjo zaidi kuliko kutumia akili zao barabara.

Nchini Cuba, Wakristo, wamenyanyasika, wakadhulumiwa na kunyamazishwa; mambo ambayo yanawafanya wananchi hao hadi leo hii, kuendelea kuishi katika hali ya wasi wasi na kuchanganyikiwa. Imani yao kwa Kristo iwajengee uwezo wa kukutana na Mwenyezi Mungu katika hija ya maisha yao ya kila siku. Ni mwaliko wa kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa katika mchakato mzima wa kuyatakatifuza malimwengu; kila mwamini akijitahidi kuchangia katika ujenzi wa Jamii, ili kupata mahali pazuri zaidi pa kuishi.

Ili kufanikisha azma hii, hakuna haja ya kufanya ugunduzi mkubwa wa kisayansi wala kwenda kuvinjari angani kwa ajili ya kutosheleza vionjo na hisia za mwanadamu, bali ukuaji na ukomavu wa maisha ya kiroho; unaothubutu kubainisha maana ya maisha, kwa kujikita kutafuta na kudumisha misingi ya haki na matumaini kwa wale waliokata tamaa ya maisha. Anawaalika Wakristo nchini Cuba kujibidisha katika azma ya Uinjilishaji Mpya, changamoto inayotolewa na Mababa wa Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya sanjari na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani.

Waamini daima wajitahidi kufanya rejea ya Imani yao kwa Kristo na Kanisa lake. Hii ni Imani ambayo mara nyingi, haikueleweka, imefutwa katika historia ya familia na watu wengi kutokana na kumezwa mno na malimwengu; kwa kutangaza tanga katika madhehebu mbali mbali ya Kikristo; kwa kuwa na misimamo mikali ya kiimani bila kusahau mifano mibaya ambayo imetolewa hata na Wakristo wengine.

Kardinali Jaime Ortega Alamino anasema, mtu akibahatika kukutana na Yesu katika hija ya maisha yake, kwa hakika, huyo atabadilika tu! Ni mtu ambaye atafanikiwa kuwa na mwelekeo na mawazo mapya, atakuwa na kukomaa, tayari kushuhudia mshikamano huo na Kristo pamoja na Kanisa lake.







All the contents on this site are copyrighted ©.