Waislam na Wakristo wanapaswa kushirikiana na kushikamana ili kudumisha haki ndani
ya Jamii
Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini kwa kushirikiana na Taasisi ya Kiislam ya
Majadiliano ya Kidini, kuanzia tarehe 19 hadi 21 Novemba 2012 walifanya mkutano wa
nane uliokuwa unajadili kuhusu ushirikiano kati ya Waislam na Wakatoliki katika kudumisha
amani ulimwenguni.
Mada hii iligawanywa tena katika vipengele vilivyojadili
kuhusu: dhana ya haki, haki mintarafu maisha ya mwanadamu, haki katika medani mbali
mbali za maisha ya kijamii pamoja na kuangalia haki kwa ajili ya Familia ya binadamu.
Ujumbe
wa Vatican katika mkutano huu uliokuwa unafanyika hapa mjini Vatican uliongozwa na
Kardinali Jean Lous Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya kidini na upande
wa Taasisi ya Kiislam ya Majadiliano ya kidini, ujumbe wake uliongozwa na Dr Mohammad
Bagher Korramshad, Rais wa Taasisi hii.
Katika tamko lao la pamoja, wajumbe
wanasema kwamba, mkutano huu umefanyika katika hali ya kirafiki, jambo lililowawezesha
wajumbe kushirikishana mawazo kuhusiana na changamoto zinazoendelea kujitokeza katika
ulimwengu mamboleo: hasa zaidi: athari za myumbo wa uchumi kimataifa, utunzaji bora
wa mazingira, sera zinazoendelea kudhohofisha misingi ya maisha na familia bora pamoja
na vitisho dhidi ya amani duniani.
Wajumbe wanatambua tofauti zao za kidini,
lakini wanafahamu fika kwamba, kuna mambo ambayo yanawaunganisha kwa pamoja nayo ni:
Imani katika Mungu mmoja, Muumbaji anayetoa fursa ya kufahamu misingi ya haki inayoweza
kutekelezwa katika ngazi ya mtu binafsi, Jumuiya; katika maisha ya kijamii, kisiasa,
kiuchumi na kimahakama.
Haki ni fadhila inayojikita katika utu na heshima
ya binadamu inayohitaji matumizi sahihi ya akili inayoangaziwa na Mwenyezi Mungu.
Kila mtu anawajibu wa kutambua na kuheshimu uhuru wa dhamiri, kwani hii ni misingi
thabiti inayopania kudumisha haki ndani ya Jamii. Uelewa makini wa dhana ya haki,
inawasaidia waamini wa dini hizi kuweza kukabiliana na changamoto mbali mbali zinazojitokeza
katika ulimwengu mamboleo.
Ni wajibu wa kimaadili kwa viongozi kupinga aina
zote za ukiukwaji wa haki na kwamba, wanachangamotishwa kusimama kidete kukuza na
kuendeleza haki sehemu mbali mbali za dunia. Viongozi hawa wa kidini wanabainisha
kwamba, wanazo nyenzo za kutosha, zinazoweza kutumika ili kutekeleza misingi ya haki
na amani katika uhalisia wake. Waamini wa dini hizi mbili wanapaswa kuendelea kufahamiana
na kushikamana kwa karibu zaidi ili kukuza majadiliano ya kidini na ushirikiano.
Wajumbe
kwa pamoja wameahidi kuhakikisha kuwa matunda ya mkutano huu yanatangazwa kwa waamini
wa Jumuiya na Jamii wanamoishi, ili kuleta mabadiliko duniani. Wanamshukuru kwa namna
ya pekee, Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, aliyewapokea na kuzungumza nao
mara baada ya Katekesi yake, Jumatano tarehe 21 Novemba 2012. Mkutano mwingine unatarajiwa
kufanyika nchini Tehran, katika kipindi cha miaka miwili ijayo, lakini utatanguliwa
na kamati ya maandalizi.