2012-11-22 15:04:46

Magereza iwe ni shule ya mafunzo endelevu na fursa ya kuonja ushindi wa Kristo kwa njia ya Fumbo la Pasaka dhidi ya dhambi na uovu!


Athari za myumbo wa uchumi kimataifa zinaendelea kusababisha matabaka ya kijamii na ubinafsi mambo ambayo yanachochea kwa kiasi kikubwa tabia ya makosa ya jinai, mada ambayo inapaswa kujadiliwa katika mapana yake si kwa kuwaachia tu watunga sheria, bali kuangalia pia jinsi ambavyo sheria inatekelezwa katika utoaji wa adhabu.

Haki inapaswa kuzingatia na kuheshimu utu na haki msingi za binadamu, mambo ambayo bado hayatekelezwa kikamilifu katika nchi nyingi duniani, kwani haki msingi za mtu binafsi zinaendelea kuvunjwa mara kwa mara, changamoto ya kuwa na mwelekeo mpya ili magereza yawe kweli ni mahali pa kurekebisha tabia, ili mfungwa anapomaliza adhabu yake, aweze kupokelewa tena katika Jamii, huku akionesha ukomavu na kwamba, sasa yuko tayari kutafuta mafao ya wengi ndani ya Jamii.

Ni sehemu ya hotuba ya Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwa wajumbe wa mkutano wa kumi na saba wa Viongozi wakuu wa magereza Ulaya, walipokutana naye Alhamisi, tarehe 22 Novemba 2012 mjini Vatican. Anasema, katika miaka ya hivi karibuni kumekuwepo na maboresho makubwa katika maisha ya wafungwa, lakini bado kuna njia ndefu inayopaswa kufuatwa. Hapa si suala la fedha, bali ni pamoja na kuhakikisha kwamba, wafungwa wanaishi katika mazingira bora yanayoheshimu na kuthamini utu wao kama sehemu ya majiundo ya wafungwa.

Kuna umuhimu wa kubadili mawazo, ili kuheshimu na kuthamini haki msingi za wafungwa na jinsi ya kutekeleza adhabu kutokana na makosa waliyotenda. Lengo la adhabu liwe ni kumwelimisha mfungwa, ili aweze kutenda haki; wasaidiwe kuwa ni watu wema wanapokuwa wanatumikia vifungo vyao, kwa kuhakikisha kwamba, wanatendewa haki. Inasikitisha kuona kwamba, magereza badala ya kusaidia kubadili tabia na mwenendo wa wafungwa, yanachochea ukatili na uvunjifu wa sheria.

Baba Mtakatifu anawakumbusha wakuu wa magereza kwamba, wanaweza kutekeleza wajibu wa kusimamia haki kwa kuwamegea wengine upendo unaojishikamanisha na utu wa mwanadamu. Ni viongozi ambao wamekabidhiwa dhamana inayowataka kuwa makini sana, kwani kazi yao ni nyeti, kwani inamgusa mtu aliyekosa, anayetekeleza adhabu ya makosa yake, lakini anahitaji pia kuheshimiwa na kuthaminiwa kama binadamu, bila kudhalilishwa wala kubezwa.

Huu ndio utume uliotekelezwa na Yesu kwa kutambua kwamba, wadhambi walikuwa ni watu ambao walikuwa na nafasi kubwa ya kupokea huruma ya Mungu katika maisha yao na kwamba, kila mtu anaalikwa kuwa ni mwangalizi wa ndugu yake. Kama wakuu wa magereza, wanapewa dhamana ya kuwatunza wafungwa, ambao wanakabiliwa na hatari kubwa ya kutokutambua maana ya maisha, utu na heshima yao, matokeo yake ni kukata tamaa.

Kuna haja kwa Jamii kuwaheshimu wafungwa na kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya majiundo yao makini, ili magereza yageuke na kuwa ni Jumuiya inayoelimisha. Wafungwa kutoka nchi za nje ni jambo ambalo linaendelea kusababisha ugumu na kuwa ni hatari zaidi.

Wafungwa wanapaswa kuonesha utashi wa kufanya mabadiliko na mageuzi katika maisha yao, kwa kushiriki kikamilifu katika mikakati inayotolewa kwa ajili ya lengo hili. Wafungwa wapewe pia huduma za maisha ya kiroho, kwa kutambua kwamba, ndani mwao wanayo chapa ya sura na mfano wa Mungu ambayo kamwe haiwezi kufutika hata wanapokuwa gerezani.

Ni matumaini ya Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kwamba, magereza yatakuwa kweli ni mahali pa mafunzo endelevu na fursa ya kuonja ushindi wa kazi ya ukombozi iliyofanywa na Kristo kwa njia ya Fumbo la Pasaka, yaani: mateso, kifo na ufufuko wake. Kwa Fumbo la Pasaka akaonesha ushindi dhidi ya uovu na nguvu za giza.







All the contents on this site are copyrighted ©.