2012-11-21 08:03:42

SECAM yaanza semina kuhusu imani, utamaduni na maendeleo Jijini Dar Es Salaam


Baraza ka Kipapa la Utamaduni kwa kushirikiana na Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM, wanaendelea na semina inayojadili kuhusu imani, utamaduni na maendeleo. Semina hii imefunguliwa rasmi hapo tarehe 20 Novemba na inatarajiwa kuhitimishwa tarehe 24 Novemba 2012 na inawashirikisha wawakilishi sabini kutoka katika Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar.

Mada zinazojadiliwa kwa sasa ni pmoja na umuhimu wa kuwa na miundo mbinu itakayosaidia mchakato wa majadiliano kati ya Kanisa Barani Afrika na tamaduni na maendeleo endelevu kwa kuwashirikisha viongozi wa Kanisa, wanataalimungu, waamini na Waafrika ambao wanaishi uhamishoni. Lengo ni kuendeleza dhamana ya Kanisa katika Uinjilishaji sanjari na utamadunisho kwa kuangalia fursa, changamoto na matarajio kwa siku za usoni.

Wajumbe wanapembua kwa kina na mapana kuhusu utamaduni wa Mwafrika na Maendeleo endelevu barani Afrika wakati wa utandawazi; umuhimu wa kujenga na kuimarisha utawala bora pamoja na sera za Afrika kuhusu maendeleo. Ni siasa zipi ambazo zinafumbatwa katika kuchanganua mikakati ya maendeleo Barani Afrika.

Ni wakati kwa nchi wanachama wa SECAM kuanzisha jukwaa la imani, utamaduni na maendeleo, kama sehemu ya utekelezaji wa Nyaraka za Kichungaji: Kanisa Barani Afrika na Dhamana ya Afrika zilizotolewa na Kanisa baada ya maadhimisho ya Sinodi za Maaskofu Barani Afrika.

Semina hii inachukuliwa kama fursa muhimu kwa Kanisa Barani Afrika kama Familia ya Mungu inayopania kuendeleza mchakato wa kukusanya na kuunganisha mambo yatakayosaidia kukuza na kuimarisha imani, utamaduni na jukwaa na maendeleo Barani Afrika.

Semina hii imetanguliwa na Kikao cha Kamati tendaji ya SECAM chini ya uongozi wa Kardinali Polycarp Pengo, Rais wa SECAM. Kamati tendaji imejadili pamoja na mambo mengine sera na mikakati inayopaswa kufanyiwa kazi kwa wakati huu pamoja na kufanya tathmini ya mradi wa utawala bora unaoendeshwa na SECAM kwa kushirikiana na Shirika la Misaada la Baraza la Maaskofu Katoliki Ujerumani, Misereor, mradi ambao ulizinduliwa tangu mwaka 2006.







All the contents on this site are copyrighted ©.