Neno la Mungu na maadhimisho ya Sakramenti za Kanisa ni vyombo madhubuti vya kurithisha
Imani ya Kikristo
Mpendwa msikilizaji wa Radio Vatican, karibu tena katika idhaa yetu ya Kiswahili.
Hewani ni kipindi chetu cha uinjilishaji wa kina ambapo tunaendela bado kuchambua
hati ya Baba Mtakatifu Benedikto XVI kwa ajili ya maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu
juu ya Uinjilishaji Mpya iliyohitimishwa hivi karibuni hapa Vatican.
Juma hili
karibu tuchambue neno la Mungu, uenezaji wa Imani, mawakala wa uinjilishaji, maisha
ya ushuhuda na matunda ya uinjilishaji mpya.
Baba Mtakatifu Benedikto XVI
anaanza kwa kubainisha kuwa tangu Mtaguso Mkuu wa pili wa Vatican, Kanisa Katoliki
limegundua kuwa uenezaji wa Imani ni makutano ya ana kwa ana na Kristu mwenyewe kupitia
Neno lake na Mapokeo ya Kanisa kwa maongozi na msaada wa Roho Mtakatifu. Kila kizazi
na kila zama zimeendelea kukutana na Kristo katika Imani Katoliki kwa njia ile ile
na hivi Kanisa linaendelea kuwa hai likitimiza utume wake lililokabidhiwa na Kristo
Mwenyewe licha ya changamoto mbali mbali za mabadiliko ya nyakati na mazingira.
Ekaristi
Takatifu imebaki daima kuwa kiungo cha mapendo kinachowaunganisha wanafamilia ya Mungu
kutoka pande zote za dunia kwa kuumega mkate mmoja katika Kristo na hivi kuwa mwili
mmoja na Roho moja.
Hivyo Baba Mtakatifu amelitaka Kanisa kutafakari kwa makini
namna litakavyojizatiti kutangaza Neno la Mungu kwa vizazi vijavyo. Mazingira yanaonesha
kwamba kuna hamu na hamasa miongoni mwa vijana kulisikia Neno la Mungu na kumjua Yesu.
Hivyo kuna haja kwa Kanisa kujifunga kibwebwe na kujitoa kimaso maso kuliweka wazi
Neno hili mbele ya vijana.
Kuna haja ya kuwasaidia vijana kujipa moyo na kulisoma
na kulitafakari Neno la Mungu bila kuogopa ili kwa Neno hilo wakapate kutambua nafasi
yao katika ulimwengu huu na katika Kanisa na hivyo kukua kiimaadili na uchaji wa Mungu.
Lakini vijana wanahitaji ushuhuda wa Neno la Mungu na maisha ya Imani hai kutoka kwa
Kanisa yaani wazazi, jumuiya na wachungaji. Makundi haya lazima yajipange kuwa na
vijana ili wajinze kutoka ushuhuda wao.
Kufanikisha hilo Baba Mtakatifu Benedikto
XVI amesisitiza umuhimu wa Katekesi ya Kina. Vijana wapewe mafundisho msingi ya Imani
wakati wa maandalizi kupokea masakramenti, lakini pia katika ngazi mbali mbali Katekesi
iendelee katika vikundi vya vijana hata baada ya kupokea masakaramenti. Kwa maneno
mengine kuwepo kwa Katekesi endelevu katika marika yote ya jamii.
Sambamba
na hili waalimu wa Katekesi waandaliwe vizuri ili waweze kutoa majibu kwa maswali
mengi ya vijana kuhusu mambo ya Imani. Kazi hii pengine wasiachiwe Maketekista tu
bali kila mmoja na hasa Mapadre na Watawa wahusike moja kwa moja katika mafundisho
ya Katekesi. Baba Mtakatifu Benedikto XVI ni mfano halisi wa Walimu wa Katekesi kwa
wale wanaosikiliza mafundisho yake ya kila Jumatano katika Basilika la Mtakatifu Petro.
Baba
Mtakatifu ameyataja Makanisa mahalia kuwa wakala wakuu wa utangazaji, uenezaji na
mashahidi wa imani katika Kanisa. Kwa msingi huo Kanisa zima linahusika katika utume
huu wa kimissionari. Baba Mtakatifu amenukuu mafundisho ya Mtaguso Mkuu wa pili wa
Vatican kuwa Roho Mtakatifu huwakusanya waumini katika vikundi ambavyo huishuhudia
imani ambayo hujionesha katika kulisikiliza Neno la Mungu, kushirikishana mang’amuzi
kadiri kila mmoja anavyoangaziwa na Roho, kusaidiana kidugu na kuuishi upendo wa Mungu
kama unavyoainishwa na Kristu mwenyewe.
Kumbe, kuna haja ya kuimarisha jumuiya
ndogondogo na vikundi mbali mbali katika Kanisa kwa madhumuni haya ya uinjilishaji.
Vikundi hivi ni uwepo halisi wa Kanisa vikiungana na Wachungaji wake ndani ya Kanisa.
Kulingana
na mazingira yaliyopo Makanisa mahalia yanaalikwa kuwajibika na kuhusika moja kwa
moja na uinjilishaji kwa kujiaminisha kabisa kwa Roho Mtakatifu anayeliongoza Kanisa
daima kiasi kwamba makanisa haya yaweze kwa nguvu, kasi na ari mpya kuendeleza utume
wa Kanisa. Wakristu katika ujumla wao wajisikie kutoka ndani kuhusika kuitikia wito
wa Kristo wa kumtangaza kwa mataifa yote kila mmoja kwa maisha yake aliyoitiwa: kama
mwanafamilia, katika fani mbali mbali, maisha ya wakfu n.k.
Mpendwa msikilizaji,
wakati ukuta. Hadi hapa, tumefikia mwisho wa uchambuzi wetu kwa juma hili. Naomba
nikuage nikikutakia kila heri na baraka kutoka kwa Mungu. Kutoka studio za Radio Vatican
ni mimi mtayarishaji na msimulizi wako Padre George wa Bodyo.