Maaskofu wa Caritas Afrika wanakutana Kinshasa, DRC. kujadili utambulisho wa Caritas
Barani Afrika
Kardinali Robert Sarah, Rais wa Baraza la Kipapa linaloratibu misaada ya Kanisa Katoliki,
Cor Unum, kwa kushirikiana na Maaskofu wa Afrika wanaosimamia na kuratibu Mashirika
ya Misaada ya Kanisa Katoliki Barani Afrika, Caritas, kuanzia tarehe 20 Novemba hadi
22 Novemba 2012 wako Kinshasa, DRC kujadili kuhusu utambulisho wa Kanisa Katoliki
Barani Afrika, mintarafu Waraka wa kichungaji wa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi
na sita, Mungu ni Upendo, Deus Caritas est!
Hii ni fursa makini kwa Maaskofu
wa Afrika kupembua kwa kina na mapana dhamana ya Caritas kama kielelezo cha mshikamano
na Makanisa mahalia. Mkutano huu unahudhuriwa pia na Kardinali Oscar Andrès Rodrìguez
Maradiaga, Rais wa Shirikisho la Kimataifa la Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki.
Utambulisho
wa mashirika ya misaada yanayosimamiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki imekuwa ni
mada ambayo inafanyiwa kazi na Kanisa katika ujumla wake. Hii inatokana na ukweli
kwamba, Caritas Barani Afrika, limekuwa ni Shirika ambalo liko mstari wa mbele katika
kuwahudumia watu wanaokabiliana na hali ngumu ya maisha hasa zaidi kutokana na umaskini,
ujinga na maradhi, matatizo ambayo yakivaliwa njuga na kila mtu akatekeleza wajibu
wake ni mambo yanayoweza kutoweka kabisa kama si kupungua kwa kiasi kikubwa Barani
Afrika.
Caritas Barani Afrika inapenda kupembua mikakati ya shughuli za kichungaji
inayopania kumhudumia mtu mzima: kiroho na kimwili. Itakumbukwa kwamba, mada hizi
zimekwisha wahi kufanyiwa kazi kunako mwaka 2002, Kigali, Rwanda na 2006 kule Libreville,
Congo. Upendo kwa Mungu na jirani ni kiini cha utekelezaji wa majukumu na mipango
ya Caritas kadiri ya mabadiliko makubwa yaliyofanywa na viongozi wa Kanisa katika
kipindi cha miaka michache iliyopita.
Shirika la Caritas linatekeleza utume
wake chini ya uongozi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro na katika ngazi ya Makanisa mahalia,
liko chini ya Maaskofu mahalia. Ni Shirika ambalo linapaswa kutekeleza wajibu wake
unaojikita katika kweli za Kiinjili, uelewa wa kitaalimungu, maisha ya kiroho; kwa
kutambua kwamba, hii ni dhamana ya Kanisa zima, inayoihusisha pia Familia ya Mungu.
Kila mwamini anachangamotishwa na Mama Kanisa kuhakikisha kwamba, anazima
kiu ya upendo kwa jirani yake, hasa kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa
jamii, kwa njia ya Neno la Mungu na matendo ya huruma. Hiki ni kielelezo cha mshikamano
unaoongozwa na kanuni auni. Maaskofu wanatumia fursa hii kuimarisha utambulisho wa
Caritas Barani Afrika pamoja na changamoto mbali mbali zinazoendelea kuibuliwa Barani
Afrika dhidi ya utume na dhamana ya Kanisa.
Caritas inapaswa kuimarisha uhusiano
wake na Maaskofu mahalia na kwamba, hili si shirika linalojitegemea bali ni kwa ajili
ya maisha na huduma ya Kanisa kwa Familia ya Mungu, kumbe kuna haja ya kutumia vyema
rasilimali inayopatikana kwa ajili ya mafao ya wengi.