2012-11-20 08:29:32

Kanisa linapania kutangaza Injili ya Upendo kwa vitendo!


Myumbo wa uchumi kimataifa umepelekea kuibuka kwa kundi kubwa la watu wasiokuwa na fursa za ajira, kumong'onyoka kwa maadili na utu wema pamoja na kuongezeka kwa baa la umaskini na ujinga duniani, hali inayotishia mustakabali wa familia nyingi. RealAudioMP3

Askofu Beatus Kinyaiya wa Jimbo Katoliki Mbulu, katika mahojiano na Radio Vatican anabainisha kwamba, Kanisa limeendelea kuonesha mshikamano wake wa dhati na maskini pamoja na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii kwa kuwatangazia Injili ya Upendo, inayopania kuwajengea uweze wa kupambana na hali ngumu ya maisha kwa kuwekeza katika miradi ya elimu, uchumi na kijamii, dhamana inayotekelezwa kwa namna ya pekee na Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki, Caritas katika ngazi mbali mbali.

Caritas kwa kushirikiana na Wanawake Wakatoliki Tanzania imeweza kutoa mikopo midogo midogo kwa vijana, wanawake na wakulima ili kuwajengea uwezo wa kiuchumi na kusaidia maboresho ya kilimo chao, ili kiweze kuwa ni bora na endelevu.

Katika mwelekeo huo, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania lilianzisha Benki ya Mkombozi ili kutoa mikopo kwa wafabiashara na wakulima ili kuinua hali yao ya kiuchumi na kijamii. Hizi ni jitihada za Mama Kanisa nchini Tanzania kutangaza Injili ya Upendo kwa vitendo!







All the contents on this site are copyrighted ©.