2012-11-19 11:31:13

Utume wa bahari ni muhimu sana kwa mabaharia, wavuvi na familia zao


Kardinali Antonio Maria Vegliò, Rais wa Baraza la Kipapa la huduma za kichungaji kwa wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum, Jumatatu tarehe 19 Novemba 2012 amefungua Kongamano la ishirini na tatu la utume wa bahari, linalowajumuisha wajumbe mia nne kutoka katika nchi sabini wanaounda Familia ya Utume wa Bahari.

Hili ni kongamano kubwa kuwahi kuandaliwa na Baraza la kipapa. Itakumbukwa kwamba, makongamano mengine yamefanyika nchini Poland kunako mwaka 2007, Brazil 2002, Ufilippini 1997, Marekani 1992. Wajumbe wanarudi tena mjini Vatican baada ya kupita takribani miaka thelathini walipokutanika hapa kwa mara ya kwanza, katika maadhimisho ya kumbu kumbu ya miaka tisini tangu hati juu ya Utume wa Bahari ilipopitishwa na Papa Pio wa kumi na moja. Ni utume ambao ni muhimu sana kwa mabaharia, wavuvi pamoja na familia zao.

Makleri, watawa na waamini walei wamekabidhiwa dhamana ya kuinjilisha kwa njia ya utume wa bahari, changamoto inayokwenda sanjari na maadhimisho ya Mwaka wa Imani na agizo lililotolewa na Mababa wa Sinodi juu ya Uinjilishaji Mpya, iliyohitimishwa hivi karibuni hapa mjini Vatican.

Lengo ni kutaka kuhakikisha kwamba, kila mwanadamu anapata fursa ya kusikiliza Habari Njema ya wokovu ikitangazwa kwake, licha ya umbali na vikwazo vinavyoweza kujitokeza. Maendeleo ya sayansi na teknolojia ya sekta ya safari za majini na uvuvi yameleta athari na changamoto katika maisha na kazi kwa mabaharia na wavuvi, lakini zaidi wakati huu wa myumbo wa uchumi kimataifa. Licha ya magumu na changamoto hizi, lakini ubaharia ni fursa nyingine inayoweza kutumiwa na Mama Kanisa katika Uinjilishaji, anasema Kardinali Vegliò.

Vyombo vya usafiri majini vinabeba si tu mizigo na bidhaa, bali watu kutoka katika kila lugha, jamaa na taifa, watu ambao wanalazimika kuwa mbali na Familia na Jumuiya zao za Kikristo bila hata ya kupata lishe ya imani yao. Uinjilishaji Mpya sanjari na maadhimisho ya Mwaka wa Imani, yawawezeshe wahudumu wa utume wa bahari kuboresha imani yao, kwa kuamini Habari Njema ya Wokovu, tayari kutoka kifua mbele ili kutangaza Injili ya Kristo kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao ya Kikristo unaojidhihirisha katika uwepo, huduma na mshikamano endelevu.

Huduma ya upendo haina budi kuwakumbatia mabaharia wote bila ya ubaguzi wa aina yoyote, kwani ushuhuda wa upendo kwa mabaharia wanaoteseka na kunyanyasika ni kielelezo makini cha mshikamano wa Kristo kwa wote. Kanisa linawapongeza kwa mchango na majitoleo yao. Kongamano hili ni fursa ya kusikiliza, kushirikishana na hatimaye, kutekeleza dhamana hii nyeti kwa moyo wa upendo na mshikamano.

Kardinali Antonio Maria Vegliò anawashukuru wafadhili na viongozi mbali mbali ambao wameendelea kuwa ni mfano bora wa kuigwa katika utoaji wa huduma kwa mabaharia. Amehitimisha hotuba yake ya ufunguzi kwa sala iliyotolewa na Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili katika Waraka wake wa kichungaji, Kanisa Oceania.







All the contents on this site are copyrighted ©.