Uharibifu wa tabaka la Ozone una madhara makubwa kwa binadamu
Askofu mkuu Silvano Maria Tomasi, mwakilishi wa kudumu wa Vatican kwenye ofisi za
Umoja wa Mataifa zenye makao makuu yake mjini Geneva, hivi karibuni ameshiriki katika
mkutano wa ishirini na nne wa nchi wanachama, uliokuwa unajadili mambo yanayochangia
kuharibika kwa Tabaka la Ozone, kama sehemu ya utekelezaji wa itifaki ya Montreal,
inayoadhimisha kumbu kumbu ya miaka ishirini na mitano tangu ilipotiwa sahihi na nchi
wanachama.
Askofu mkuu Tomasi anabainisha kwamba, kipindi cha miaka ishirini
na mitano ni muda muafaka kabisa wa kuweza kufanya tafakari ya kina kuhusu maendeleo
yaliyokwishafikiwa tangu Itifaki ya Montreal ilipotiwa sahihi, ili kulinda Tabaka
la Ozone lenye umuhimu sana katika maisha ya mwanadamu na utunzaji wa mazingira. Uharibifu
wa Tabaka la Ozone unaweza kuwa na madhara makubwa katika maisha ya mwanadamu, jambo
linalohitaji uwajibikaji wa pamoja, wa ajili ya mafao na maendeleo ya kizazi hiki
na kile kijacho.
Kuna haja kwa nchi wanachama wa Itifaki ya Montreal kushirikiana
na wadau wengine katika mchakato wa kulinda na kutunza mazingira, kwa kushikamana
pamoja ili kuzisaidia nchi zinazoendelea duniani ili kukabiliana na changamoto zinazotokana
na mabadiliko ya tabianchi, ili kwa pamoja ziweze kuchukua hatua madhubuti katika
kutunza mazingira.
Dhamana ya kulinda na kutunza mazingira inakwenda sanjari
na haki msingi za binadamu, kwani madhara yake ni makubwa kwa afya za wananchi walio
wengi. Kwa nchi changa duniani, itakuwa ni vigumu kwao kuweza kupata tiba ya magonjwa
yanayosababishwa na uharibifu wa Tabaka la Ozone kutokana na gharama za matibabu haya
kuwa ni kubwa. Ikumbukwe kwamba, kuongezeka kwa kina cha maji baharini kumepelekea
mamillioni ya watu kuyakimbia makazi yao pamoja na kudumaza uchumi wa maeneo husika.
Utunzaji wa Tabaka la Ozone kiwe ni kielelezo cha mshikamano kwa kizazi hiki
na kile kijacho. Katika kipindi cha miaka ishirini na mitano iliyopita, kumekuwepo
na mafanikio ya kuridhisha katika kutunza na kuhifadhi Tabaka la Ozone, kutokana
na Serikali kushirikishana maendeleo ya sayansi na teknolojia, kwa kupashana habari
pamoja na kukazia elimu ya utunzaji bora wa mazingira., lengo ni kuwajibika kikamilifu
katika utunzaji wa kazi ya uumbaji ambayo mwanadamu amekabidhiwa kuifanya kwa hekima
na busara.
Ujumbe wa Vatican katika mkutano huu unabainisha kwamba, Kanisa
limeendelea kuwa mstari wa mbele kuhimiza utunzaji bora wa mazingira kwa kukazia elimu
ya mazingira, kanuni za maadili, matumizi bora ya vitu kwa kuepuka ulaji wa kupindukia
kwa kutambua kwamba, mazingira ni zawadi kubwa kwa maisha na ustawi wa mwanadamu,
yanapaswa kulindwa na kutunzwa vyema.
Binadamu ajenge utamaduni wa kutunza
na kuhifadhi mazingira kwa ajili ya mafao yake; juhudi hizi zijioneshe kwa kuwa na
sera na sheria makini zinazoheshimiwa na kutekelezwa.
Askofu mkuu Silvano Maria
Tomasi anahitimisha mchango wake kwa kusema kwamba, utunzaji bora wa mazingira ni
wajibu fungamanishi kwa familia nzima ya binadamu, unapania kukuza na kudumisha maendeleo
yake, kwa sasa na kwa wakati ujao.