Onesheni ukomavu na uzalendo kwa kukubali matokeo ya uchaguzi mkuu
Baraza la Maaskofu Katoliki Ghana katika mkutano wao wa mwaka uliohitimishwa hivi
karibuni linawaalika wananchi wa Ghana kushiriki kikamilifu katika uchaguzi mkuu nchini
humo utakaofanyika tarehe 7 na tarehe 28 Desemba 2012, ili kumchagua rais pamoja na
wabunge, watakaopewa dhamana ya kuiongoza nchi ya Ghana.
Maaskofu wanawaomba
wagombea urais na ubunge pamoja na mashabiki wao, kuhakikisha kwamba, wanadumisha
misingi ya haki, amani, utulivu na umoja wa kitaifa. Upande utakaoshindwa uoneshe
ukomavu na uzalendo wa kukubali matokeo kwa heshima na taadhima, kwani katika mashindano
yoyote kuna kushinda na kushindwa.
Wagombea nafasi za uongozi wawaelimishe
wananchi madhara yanayoweza kujitokeza ikiwa kama uchaguzi hautazingatia: sheria,
kanuni na maadili mema. Wapiga kura wajiepushe na vitendo vya kudanganya pamoja na
kuwapigia kura hata wale waliokwisha kufariki, kwani vitendo vya namna hii vinaweza
kulitumbukiza taifa katika maafa makubwa. Wale watakaoshinda waupokee ushindi wao
kama heshima na dhamana kutoka kwa wananchi wa Ghana na wale watakaoshindwa waoneshe
uzalendo kwa kukubali matokeo kwa heshima na taadhima wanasema Maaskofu, ikiwa kama
uchaguzi utakuwa ni huru na wa haki.
Wabunge watakaochaguliwa kutoka katika
vyama vya upinzani, hata katika uchache wao, lakini watambue kwamba, wanayo dhamana
kubwa kuchangia mawazo chanya katika uendeshaji wa shughuli za Serikali. Wabunge wote
kwa pamoja watambue kwamba, lengo la kuu ni kwa ajili ya kutafuta mafao ya wa wananchi
wa Ghana katika ujumla wao na hivyo wawe tayari kupokea tamko rasmi kutoka katika
Tume ya Uchaguzi Ghana.
Baraza la Maaskofu Katoliki Ghana, linavitaka vyombo
vya habari na vyama vya siasa kutoa nafasi kwa Tume ya Uchaguzi Ghana kutekeleza wajibu
na dhamana yake kwa kutangaza kwa wakati muafaka wale watakaoibuka washindi baada
ya uchaguzi, vinginevyo wanaweza kusababisha vurugu na ghasia zisizo na msingi wala
tija kwa wananchi wa Ghana. Pale ambapo sheria, kanuni na taratibu za uchaguzi hazikufuatwa
kikamilifu, vyama vya siasa na mashabiki wao, watumie sheria za nchi kutafuta haki
yao msingi bila kukimbilia vurugu na fujo.
Maaskofu wa Ghana wanasema, mara
baada ya washindi kutangazwa, wananchi wanapaswa kuachana na tofauti zilizowagawa
wakati wa mchakato wa kupiga kura, ili kushikamana kwa pamoja kujenga na kuimarisha
misingi ya mshikamano kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Ghana. Wananchi wajenge
umoja na mshikamano wa kitaifa.