2012-11-19 10:16:07

Kanisa ni sauti ya Kinabii inayotangaza Kweli za Kiinjili ili kukabiliana na changamoto mbali mbali zinazojitokeza ndani ya Jamii


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, tarehe 17 Novemba 2012 alikutana na kuzungumza na Kundi la Pili kutoka Baraza la Maaskofu Katoliki Ufaransa, lililohitimisha hija yao ya kitume inayofanyika kila baada ya miaka mitano hapa mjini Vatican.

Baba Mtakatifu anasema, Kanisa ni mjumbe wa Neno la Kristo lenye mguso na utambulisho wa kidini, lakini linafumbata ndani yake hekima ya Kimungu inayoweza kusaidia kupata ufumbuzi wa matatizo na changamoto mbali mbali zinazoikumba Jamii katika ulimwengu wa utandawazi. Wakristo wanaalikwa kuwashirikisha jirani zao sauti ya matumaini, inayosubiriwa kwa hamu kubwa.

Baba Mtakatifu anasema, Ufaransa ina historia yenye utajiri mkubwa ambayo kamwe haiwezi kubezwa wala kutwezwa. Kanisa lina dhamana na wajibu wa kuhakikisha kwamba, sauti yake inasikika, hata kama Kanisa na Serikali inatekeleza wajibu na dhamana yake katika ngazi mbili tofauti zinazopaswa kuheshimiwa, lakini ikumbukwe kwamba, Kanisa lina dhamana ya kutangaza Ukweli unaokomboa na kujaza mioyo ya watu matumaini na mapendo ya dhati.

Baba Mtakatifu anawaalika Waamini walei wanaotekeleza utume wao katika maisha ya hadhara kuendelea kushirikiana na Maaskofu kusimama kidete dhidi ya sheria zinazoweza kuhataraisha misingi ya maisha ya ndoa na familia inayoundwa kati ya Bwana na Bibi. Ni wajibu wao kutangaza Injili ya Uhai tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake hadi mauti inapomfika kadiri ya mpango wa Mungu.

Baba Mtakatifu anaungana na Maaskofu Katoliki Ufaransa kuonesha wasi wasi wake unaojikita katika urithishaji wa imani kwa vijana wa kizazi kipya; changamoto zinazoendelea kuzikabili familia nyingi ambazo kimsingi zinahitaji kupatiwa msaada ili kukabiliana na changamoto wanazokabiliana nazo.

Kuna baadhi ya watu wanataka kudhalilisha dhamana na utume wa Kanisa, ili uonekane kuwa ni jambo binafsi; changamoto kwa waamini kutolea ushuhuda wa imani yao kifua mbele, daima wakisukumwa na ujasiri, uaminifu na mafundisho adili ya Kanisa. Hii ndiyo changamoto endelevu katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani. Wazazi watekeleze wajibu wa malezi kwa watoto wao na kwa ajili ya mafao ya wengi.







All the contents on this site are copyrighted ©.