2012-11-17 09:35:24

"Sitisheni mashambulizi ya Makombora kwa ajili ya mafao ya pande hizi mbili"


Dr. Olav Fykse Tveit, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni, ameonesha masikitiko yake makubwa kutokana na mgogoro wa kivita unaoendelea kufuka moshi kwenye Ukanda wa Ghaza na Israel. Anazitaka pande zote mbili kuacha uhasama na kuhakikisha kwamba, wanatoa ulinzi na usalama kwa raia na mali zao.

Mgogoro wa kivita katika maeneo haya unaendelea kusababisha vifo na mateso kwa watu wasiokuwa na hatia. Kuna idadi kubwa ya watu ambao wamejeruhiwa vibaya sana, wengi wao ni wanawake na watoto. Baraza la Makanisa Ulimwenguni linafuatilia kwa umakini mkubwa mwenendo mzima wa mgogoro huo ambao umeibuka kwa kasi kubwa na kutaka pande zote mbili kusitisha mara moja mapigano ili kuokoa maisha ya watu.

Binadamu ana thamani kubwa machoni pa Mwenyezi Mungu na kwamba, mauaji ya watu wasiokuwa na hatia, hayawezi kukubalika kama malipo kutokana na migogoro na kinzani na migogoro ya kisiasa na kivita ambayo bado haijapata ufumbuzi wake.

Baraza la Makanisa Ulimwenguni linaliomba Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa pamoja na Shirikisho la Nchi za Kiarabu kutafuta suluhu ya haraka ili kuhakikisha kwamba, vita hii inasitishwa kwa ajili ya mafao ya pande zote mbili.

Dr. Tveit anasema kuwa, ni jambo ambalo halikubaliki kuona wananchi wanaoishi Israel wakishambuliwa na makombora kutoka Ukanda wa Ghaza, kwani mwelekeo huu unaweza kuhatarisha harakati za Palestina kutaka kutambuliwa na Jumuiya ya Kimataifa kama Nchi huru.







All the contents on this site are copyrighted ©.