2012-11-16 15:12:13

Rais Alassane Ouattara akutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu mjini Vatican


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Ijumaa tarehe 16 Novemba amekutana na kuzungumza na Rais Alassane Ouattara wa Pwani ya Pembe mjini Vatican. Viongozi hawa wawili wamezungumzia uhusiano mwema uliopo kati ya Vatican na Pwani ya Pembe, sanjari na mchango wa Kanisa Katoliki katika mchakato wa maendeleo endelevu nchini humo.

Wamesema, Kanisa bado linaweza kuchangia zaidi katika kuimarisha na kusimamia misingi ya haki, amani, majadiliano ya kidini na kiekumene pamoja na upatanisho wa kitaifa, chachu muhimu sana katika jitihada za wananchi kujiletea maendeleo yao.

Baba Mtakatifu pamoja na Rais Outtara wanasema, kuna haja kwa Kanisa na Serikali kuendelea kushirikiana kwa karibu zaidi hususan katika utoaji wa huduma katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu. Viongozi hawa kwa pamoja wameonesha nia ya kutiliana sahihi mkataba wa ushirikiano baina ya nchi hizi mbili.

Katika mazungumzo yao, viongozi hawa wawili wamegusia pia changamoto zinazojitokeza Barani Afrika, kwa kuzingatia kwamba, kwa sasa Rais Ouattara ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Ushirikiano wa Kiuchumi Afrika Magharibi, ECOWAS.

Rais Ouattara na ujumbe wake, walikutana na ujumbe wa Vatican uliokuwa unaongozwa na Kardinali Tarcisio Bertone, Katibu mkuu wa Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.