Mama Kanisa kumtangaza Mtumishi wa Mungu Maria Crescencia kuwa Mwenyeheri hapo tarehe
17 Novemba 2012
Mtumishi wa Mungu Maria Crescencia Pèrez aliyeishi kati ya Mwaka 1897 hadi mwaka 1932
ni kutoka katika Shirika la Mabinti wa Bikira Maria wa Orto. Kutangazwa kwake kuwa
Mwenyeheri ni furaha isiyokuwa na kifani kwa Kanisa zima, lakini kwa namna ya pekee,
kwa Familia ya Mungu nchini Arjentina, inayoshuhudia Binti yao akiandikwa kwenye Kitabu
cha Watakatifu wa Mungu.
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, akatika
Barua yake ya kichungaji kwa ajili ya kumtangaza Mtumishi wa Mungu Maria Crescenzia
Pèrez kuwa Mwenyeheri anasema kwamba, ni mtawa ambaye amejitahidi katika hija ya maisha
yake hapa duniani kumwilisha Injili ya Upendo katika hali ya kawaida, kwa unyenyekevu
na upendo usiokuwa na makuu.
Ni mtawa aliyekuwa na utulivu wa ndani na furaha
ya kweli katika hija ya maisha yake, ndiyo maana watu wengi hadi leo hii wanamwita
“Sista Mpendelevu” “Sor Dulzura”. Mashahidi wengi wanasema, kwa hakika watawa wote
walikuwa ni wema, lakini Sista Maria Crescencia Pèrez alikuwa ni mwema zaidi kuliko
wengine wote. Ni mtawa aliyekuwa na utashi thabiti, mvumilivu, mwema, mwenye furaha
na mpendelevu.
Tabia hii iliboreshwa zaidi kwa njia ya Imani hai, isiyotetereka;
Imani ambayo ilimwilishwa katika matendo na uhalisia wa maisha ya kila siku. Shughuli
zake za kichungaji na kitume zilipata chimbuko lake katika Imani, kiasi kwamba, alionekana
kana kana kwamba, ni mtu ambaye aliishi hapa duniani, lakini moyo wake ulikuwa mbinguni,
kama anavyosimulia moja wa mashahidi wake.
Upendo wake, anasema Kardinali Angelo
Amato, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa lenye dhamana ya kuwatangaza Watakatifu na Wenyeheri,
aliyekabidhiwa dhamana ya kumwakilisha Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika
Ibada ya kumtangaza kuwa Mwenyeheri kwamba, ni mtawa ambaye upendo wake, ulijionesha
kwa namna ya pekee, kwa Mungu na jirani.
Alijitoa bila ya kujibakiza kwa ajili
ya kuwasaidia maskini na wote waliokuwa wanasukumizwa pembezoni mwa jamii, si tu kwa
maneno matupu, bali kwa jasho na bidii ya kazi ya mikono yake, kwa kuwalipia wale
waliokuwa hawana mavazi, watoto wagonjwa ambao wazazi wao walishindwa kulipia gharama
za dawa.
Alitoa maziwa kwa wagonjwa, akiwaonesha upendo mkamilifu. Kwa watoto
waliokuwa wanapokea Ekaristi Takatifu kwa mara ya kwanza, alihakikisha kwamba, kila
mtoto anafurahia kwa kuwa na nguo nzuri, kwa kuwapatia vitabu vya kumbu kumbu na rozari,
ili kila mtoto aweze kweli kuifurahia siku hii ambayo alikuwa anakutana na Yesu wa
Ekaristi katika maisha yake.
Daima alisikika akisema kwamba, Yesu Kristo anajidhihirisha
kwa namna ya pekee miongoni mwa maskini, wagonjwa na wote wanaosukumizwa pembezoni
mwa Jamii, hawa wanapaswa kupendwa, kuheshimiwa na kuthaminiwa.
Kardinali Angelo
Amato anasema, kutangazwa kwa Mtumishi wa Mungu Maria Crescencia Pèrez kuwa Mwenyeheri,
ni mwaliko kwa waamini kukuza na kuimarisha imani yao kwa Mwenyezi Mungu kwa njia
ya maisha yao pamoja na kuwashirikisha wengine bila woga wala makunyanzi. Ni changamoto
ya kuchuchumilia utakatifu wa maisha, kwa kukuza na kudumisha ari na moyo wa sala,
huduma kwa wagonjwa na maskini; kwa watoto na wenye kuhitaji.
Ni mtawa anayehimiza
tafakari ya kina kuhusu Fumbo la Utatu Mtakatifu; upendo wa kidugu na furaha inayobubujika
kutoka katika Imani. Mtawa huyu ni kielelezo bora cha utu wema, utulivu na amani ya
ndani; furaha na upendo mkamilifu. Ni cheche ya upendo wa Mungu inayoburudisha moyo
wa mwanadamu na kumsukuma kutafuta lililojema zaidi.