2012-11-15 14:37:48

Viongozi waandamizi simamieni kikamilifu miradi ya maendeleo ili kuleta tija


WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amewataka Wakuu wa Mikoa na Wilaya waachane na dhana ya “Eyes on Hands Off” kama kweli wanataka kusukuma mbele maendeleo ya nchi hii kwani dhana hiyo imechangia mambo mengi kukwama.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo Alhamisi, Novemba 14, 2012) wakati akifungua Mkutano Maalum wa Kazi wa siku tatu kwa Wakuu wa Mikoa na Wilaya na Makatibu Tawala wa Mikoa ulioanza leo kwenye ukumbi wa Pius Msekwa mjini Dodoma.

“Ninatoa rai kwenu kujaribu kuondokana na tafsiri isiyokuwa sahihi ya dhana ya “Eyes on Hands Off” kuwa Mkuu wa Mkoa au Mkuu wa Wilaya hatakiwi kuingilia utendaji wa walio chini yake hata kama hawatekelezi vema wajibu wao na hivyo kusababisha mambo kutokwenda”, alisema.

“Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya wewe ndiwe Rais amekuteua na kukukabidhi madaraka ya kusimamia eneo lako. Kauli hii isiwaondolee jukumu la kusimamia miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika maeneo yenu. Ni lazima mkaitembelee na kujua kinachoendelea,” alisema huku akishangiliwa.

Waziri Mkuu alisisitiza kwamba: “Hii ni dhana potofu lazima sasa tuachane nayo. Lazima tufanye kazi kwa karibu na kuhakikisha miradi yote ya maendeleo katika maeneo tunayoyasimamia inatekelezwa kwa ukamilifu.”

Aliwakumbusha viongozi hao kwamba Serikali imeandaa Mpango wa Taifa wa Maendeleo muda mrefu na Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2011 -2016) ambao imeanza kuutekeleza.

“Viongozi mliopo hapa ni chachu muhimu sana ya kusimamia utekelezaji wa mipango hiyo. Tunahitajika kuandaa kwa kina na kusimamia utekelezaji wa mipango yetu kwa kuanisha wajibu wa kila mmoja katika utekelezaji... tunatakiwa kupanga na kusimamia matumizi ya fedha zinazotolewa kwa kuzingatia vipaumbele vichache tunavyokubaliana. Hatua hii itaonesha haraka matokeo mazuri na makubwa kwa maeneo ya kipaumbele na hatimaye kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi wetu,” alisema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu aliwaeleza viongozi hao kwamba Serikali kwa sasa ina mkakati mzuri wa kutambua mchango wa wabunifu na wagunduzi katika kuendeleza sayansi na teknolojia. “Tumepitisha sheria ya kuwatambua wagunduzi hivi karibuni, hivyo, tuna sehemu ya kuanzia,” aliongeza.

Aliwataka Wakuu hao wa Mikoa na Wilaya pamoja na Makatibu Tawala wa Mikoa wafanye kazi ya kuwabaini na kuwaendeleza wagunduzi wanaopatikana katika ngazi za Mikoa na Wilaya, ili kazi zao zisaidie kuendeleza uchumi wa Tanzania.

Akifafanua, Waziri Mkuu alisema Tanzania itakuwa mwenyeji wa Mkutano wa Kimataifa ujulikanao kama “Global 2013 Smart Partnership Dialogue” ambao utafanyika jijini Dar es Salaam Mei 24 – 28, 2013 ikiwa ni utekelezaji wa ahadi aliyoitoa Rais Jakaya Kikwete wakati akihudhuria mkutano kama huo huko Petrojaya, Malaysia, Juni 2011.

“Kwa kutambua kazi kubwa iliyoko mbele ya maandalizi ya mkutano huo mkubwa, jukumu lenu kubwa ni kusimamia mchakato mzima wa maandalizi ya Mkutano wa kitaifa kuanzia ngazi ya Wilaya na Mikoa,” alisisitiza.

Alisema wao ni Wenyeviti wa Mabaraza ya Biashara katika ngazi za mikoa na wilaya. Hivyo, baada ya mkutano huo wanatakiwa kuitisha mikutano ya mabaraza na kuendesha kwa kina midahalo muhimu katika ngazi zenu ili matokeo ya midahalo hiyo itumike kwenye mdahalo wa kitaifa ifikapo Januari 2013.

“Tujitahidi kati ya sasa na Januari 2013 tuwe tumekusanya maoni ya kutuwezesha kushiriki kwenye Mkutano huo. Jukwaa hili la Kimataifa liwe sehemu ya kupanua ushirikiano wa kimataifa katika nyanja ya teknolojia na ubunifu. Wanachotaka kwetu sisi kabla ya kwenda kwenye mkutano huo lazima tuwe na makundi tayari ya kuchangia” alisisitiza.

Mikutano ya “International Smart Partnership Dialogue” huandaliwa na nchi mwenyeji ikishirikiana na Taasisi ya Jumuiya ya Madola iitwayo Commonwealth Partnership for Technology Management – CPTM yenye makao yake jijini London, Uingereza. Mikutano hii ambayo hufanyika kila baada ya miaka miwili, ilianza kufanyika mwaka 1995, na ilipewa msukumo mkubwa na Waziri Mkuu Mstaafu wa Malaysia, Dkt. Mahathir Mohammed.

Mikutano hii huendeshwa kwa ushirikiano kati ya Malaysia na Nchi za Kusini mwa Afrika zikiwemo Zimbabwe, Zambia, Botswana, Msumbiji, Swaziland na Lesotho. Uganda imekuwa mwenyeji wa mikutano hii mara mbili mwaka 2001 na 2009.

Mikutano ya “Smart Partnership Dialogue” tofauti na mikutano mingine ni jukwaa la majadiliano kati ya Serikali na jumuiya mbalimbali za wananchi kuhusu jambo lo lote lenye manufaa kwao na ambalo litachangia kuleta maendeleo yao kijamii na kiuchumi. Viongozi mbalimbali wa Serikali wakiwemo wa ngazi za juu hukaa pamoja kama watu wa ngazi sawa na jumuiya za wananchi, zikiwemo za vijana, wasomi, wafanyakazi, wafanyabiashara, waandishi wa habari, wanasanaa na utamaduni, wanasiasa na madhehebu ya dini.

Naye Prof. Lucien Msambichaka wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) akitoa mada kuhusu ushirikiano kwa manufaa ya wote (Smart Partnership Dialogue) alisema hapa nchini kuna wabunifu na wagunduzi wenye vipaji mbalimbali ambao wanapaswa kuendelezwa ili kuharakisha maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Aliwataja baadhi yao kuwa wapo waliobuni ndege (Arusha), trekta (Ruvuma), incubator (Dar es Salaam), antenna za tubelight (Temeke-DSM), madish ya televisheni (Mbeya), na na kusisitiza kuwa wote hawa wanahitaji kuwezeshwa kiteknolojia ili kuboresha viwango vya vifaa walivyovibuni. “Wakipatiwa nguvu ya teknolojia, itawasaidia katika kuwezesha ukuaji shirikishi wa kijamii na kiuchumi,” alisema Prof. Msambichaka.

Akizungumzia kuhusu ukuaji wa kiuchumi, aliwataka Wakuu wa Mikoa na Wilaya ambao wanashiriki mkutano huu wasimamie maendeleo katika maeneo yao ili Tanzania iweze kweli kufikia malengo yake ya kuwa ni Taifa lenye uchumi wa kati (middle income country) ifikapo mwaka 2025.

Mada nyingine zitakazowasilishwa kwenye mkutano huo wa siku tatu ni Hali ya Usalama wa Nchi; Usimamizi na Ufuatiliaji wa shughuli za Serikali hususan Miradi ya Maendeleo; Usimamizi wa Mapato na Matumizi ya Fedha za Serikali za Mitaa na Usimamizi na Ufuatiliaji wa shughuli za Serikali za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa. Mada nyingine ni Migogoro ya Ardhi; Maandalizi ya Msimu wa Kilimo 2012/2013; Hali ya Lishe Nchini pamoja na Umuhimu Bima ya Afya kwa Wananchi.









All the contents on this site are copyrighted ©.