Ubadhirifu wa mali ya umma na wizi wa fedha vinavyowatesa watanzania!
HOJA BINAFSI YA KABWE ZUBERI ZITTO(MB) KUHUSU KULITAKA BUNGE KUCHUNGUZA NA KUILEKEZA
SERIKALI KUCHUKUA HATUA DHIDI YA RAIA WA WATANZANIA WALIOFICHA FEDHA NA MALI HARAMU
NJE YA NCHI
[Chini ya Kanuni ya 54(1) na (2)]
UTANGULIZI: Mheshimiwa
Spika, Mnamo tarehe 2 Novemba 2012 niliwasilisha barua ya kusudio la kuwasilisha
Bungeni Hoja binafsi kuhusu suala hilo hapo juu. Lengo la Hoja binafsi hiyo ni kuitaka
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuwasiliana na Taasisi ya Benki ya Dunia
kupitia kitengo cha ‘Assets Recovery’ kurejesha fedha haramu zilizofichwa na Raia
wa Tanzania katika mabenki huko nchini Switzerland. Ofisi yako ilinitaka nilete maelezo
ya ziada kuhusu hoja hiyo ili ipatiwe nafasi ya kupangwa kwenye ratiba za Bunge. Baada
ya kuleta maelezo hayo Ofisi yako imenipa nafasi kuwasilisha hoja hii mbele ya Bunge
lako tukufu. Kwa heshima na taadhima ninawasilisha mbele ya Bunge lako tukufu hoja
hii muhimu sana katika kuhakikisha kwamba Taifa letu linaziba mianya ya ufisadi na
hususani utoroshwaji wa fedha za kigeni za Tanzania.
Mheshimiwa Spika, Mwezi
Juni mwaka 2012, Benki Kuu ya Switzerland (National Bank of Switzerland) ilitoa taarifa
kwa umma kuhusu raia wa mataifa mbalimbali duniani wenye dhamana kwenye mabenki nchini
humo. Benki hiyo ilitangaza kwamba Jumla ya dola za Kimarekani milioni 196 (milioni
mia moja tisini na sita) zilikuwa zimehifadhiwa kwenye akaunti za mabenki mbalimbali
nchini humo na kwamba wenye fedha hizo ni Raia wa Tanzania. Fedha hizo ni zaidi ya
shilingi bilioni 314 (mia tatu kumi nanne bilioni) ukizibadilisha kwa thamani ya fedha
za Tanzania.
Mheshimiwa Spika, Mazungumzo yangu ya mwisho niliyoyafanya
jana usiku na wachunguzi waangu binafsi yameongeza taarifa ya ziada muhimu. Kwanza,
kiwango cha fedha kinacho milikiwa na watanzania nchini Switzerland peke yake ni takribani
mara 20 ya kiwango kilicho tangazwa na Benki ya Tanifa ya nchi hiyo. Kwa mfano, Benki
ya UBS peke yake ina maofisa 240 wanaohusika na Tanzania peke yake. Kila ofisa mmoja
husimamia mteja mwenye kiwango kisicho pungua dola za marekani milioni 10.
Fedha
hizi ni sehemu tu ya fedha ambazo watanzania wanazificha katika mabenki mbalimbali
ya nje ya nchi, na ndani ya hesabu hizi hamna fedha zilizo nchi nyingine,kama visiwa
Jersey, Mauritius na Cayman Islands maana nchi nyingine hazina utaratibu huu wa kuweka
wazi kama ilivyo kwa nchi ya Swistzerland kwa mwaka huu.
Mheshimiwa Spika, Gazeti
la The Guardian On Sunday la tarehe 23 Juni 2012 lilimnukuu Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi
ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa ndugu Edward Hosea akisema kwamba siku ya jumatatu
tarehe 24 Juni mwaka 2012 angeandika Barua kwenda Mamlaka za Switzerland kutaka kupewa
orodha ya majina ya raia wa Tanzania wenye fedha katika akaunti zilizotajwa. Hata
hivyo mpaka ninaleta maelezo haya umma wa Watanzania haujalezwa kama barua hiyo iliandikwa
na majibu yake yalikuwa ni nini. TAKUKURU ndio mamlaka pekee hapa nchini ambayo inaweza
kupata orodha ya majina ya watu wenye mabilioni haya kwa njia za halali na hasa kwa
watu ambao ni ‘Politically Exposed Persons’ kama Wabunge na waliowahi kuwa wabunge,
Mawaziri na waliowahi kuwa Mawaziri na viongozi wengine wa ngazi za juu katika Taifa
letu.
Mheshimiwa spika, Nchi nyingine duniani zimetumia njia mbali mbali
kuhakikisha fedha haramu zinazo toroshwaa zinarejea nchini kwao. Marekani na Ujerumani
wao waliamua kununua CDs kutoka kwa waliokua wafanyakazi wa mabenki ya Switzerland,
wakagundua Raia wao walioficha fedha nje na kuwatoza kodi kutokana na fedha hizo.
Ujerumani wao wameingia mkataba wa kupashana taarifa za kikodi na nchi ya Switzerland
ili kuwatoza kidi raia wao wenye fedha huko. Hata hivo mkataba huu wa kikodi haujapitishwa
na Bunge la Ujerumani Bundesrat kwani chama kikuu cha upinzani cha SPD kinapinga,
na tayari chama hicho kimenunua CDs zenye majina ya Raia wa Ujerumani wenye akiba
nje.
Hivi karibuni gazeti moja nchini Ugiriki limechapisha orodha ya wagiriki
walioficha fedha zaio huko Switzerland. Orodha hii inatokana na orodha ambayo alie
kua Waziri wa Fedha wa Ufaransa Christine Lagarde aliipa serikali ya Ugiriki, lakini
serikali hiyo haikuifanyia kazi.
Mheshimiwa Spika, Kiufupi, toka taarifa
za Benki ya Taifa ya Switzerland kutangazwa, Serikali haijachukua hatua yeyote ya
maana kuhakikisha kuwa suala hili linafanyiwa uchunguzi wa kina na hatua stahili dhidi
ya watoroshaji wa fedha hizo zinachukuliwa ikiwemo kurejeshwa kwa fedha hizo nchini
kwa ajili ya maendeleo ya Taifa letu. Ikumbukwe kwamba katika watanzania wenye fedha
huko nje wapo ambao fedha zao wamezipata kihalali kutokana na shughuli za kibiashara
na wapo ambao wamepata fedha hizi kwa njia za rushwa. Uchunguzi wa kina ni muhimu
sana ili kuweza kutofautisha kati ya Fedha haramu na fedha halali. Vilevile uchunguzi
unatakiwa kutofautisha katika watu wenye fedha halali kama walifuata taratibu za kisheria
za nchi zinazoruhusu raia wa Tanzania wanaoishi Tanzania kuwa na akiba ya fedha za
kigeni nje ya Tanzania. Kitendo cha Serikali kukaa kimya bila kuchukua hatua kinaashiria
ama kutotimiza wajibu au kwamba wanaopaswa kuchukua hatua ni washirika wa utoroshaji
huu wa fedha za nchi na kuzificha katika mabenki ya nje.
Mheshimiwa Spika, Kabla
ya kueleza kwa kina vyanzo viwili vikubwa vya fedha kwa raia wa Tanzania wanaomiliki
fedha na mali katika mabenki nje ya nchi nieleze kwamba, Watu hufungua akaunti nje
ya nchi au kumiliki mali nje ya nchi kwa sababu kuu mbili. Moja ni kuficha fedha haramu
zilizopatikana kwa njia zisizo halali na mbili kukwepa kodi kutokana na mapato yao.
Njia ya kwanza hutumiwa zaidi na wanasiasa na watendaji wa Serikali (Politically exposed
Personalities – PEPs) na njia ya pili hutumiwa na wafanyabiashara wakubwa na hasa
wafanyabiashara wanaouza bidhaa nje ya nchi. Harakati zozote za kuchukua hatua dhidi
ya makundi haya yana faida ya kuzuia ufisadi kwa kuonyesha kwamba hakuna pa kujificha
iwapo ukifanya ubadhirifu, na kuongeza mapato ya Serikali kwa kuhakikisha Raia wote
wakazi wanalipa kodi inavyostahili.
Uchunguzi wa chanzo cha Fedha.
Mheshimiwa
Spika, Kwa mujibu wa Taarifa ya Global Financial Integrity (GFI) ya mwaka 2008,
jumla ya dola za kimarekani bilioni 8 (dola bilioni nane) zimetoroshwa kutoka Tanzania
kati ya mwaka 1970 mpaka 2008. Kwa bei ya sasa ya dola za kimarekani fedha hizi ni
sawa na shilingi trilioni 13 (trilioni kumi na tatu). Mpaka Mwezi Julai mwaka 2012
Deni la Taifa kuanzia mwaka 1961 lilikuwa ni dola za kimarekani bilioni kumi. Hii
maana yake ni kwamba fedha zote zilizotoroshwa kutoka Tanzania katika kipindi cha
miaka 38 kingeweza kulipia asilimia themanini ya Deni la Taifa. Mwaka 2012/2013 Bunge
limeidhinisha jumla ya shilingi trilioni 1.9 kulipia Deni la Taifa.Suala hili ni changamoto
kwa nchi mbalimbali za kiafrika ambapo mabilioni yafedha hutoroshwa kila mwaka na
watawala wala rushwa na wafanyabiashara wasio waaminifu kwenda nje ya Afrika na kuliacha
bara la Afrika likiwa na ufukara wa kutupwa.
Mheshimiwa Spika, Sehemu ya
Fedha hizi zilizotoroshwa zilitokana na ufisadi, nyingine zilitokana na ukwepaji wa
kodi na nyingine zilitokana na madeni ambayo Serikali iliingia ambapo sehemu kubwa
ya Madeni ilibaki huko huko ughaibuni lakini bado Watanzania wanalipa madeni hayo.
Hata hivyo Fedha zilizotokana kutokana Ufisadi na zile za ukwepaji kodi ni nyingi
zaidi katika fedha zilizotoroshwa kutoka Tanzania.
Mheshimiwa Spika, Kwa
mfano kati ya mwaka 2003 - 2005 Tanzania iligubikwa na ufisadi mkubwa sana wa Fedha
kutoka Benki ya Tanzania ambapo jumla ya shilingi bilioni 155 zililipwa kutoka Benki
Kuu ya Tanzania kwenda Benki ya NedBank ya Afrika Kusini kama malipo ya mkopo ambao
Serikali iliudhamini kwa ajili ya mradi wa uchimbaji dhahabu wa meremeta. Fedha hizi
zilikuwa ni mara kumi na tano ya mkopo uliodhaminiwa na Serikali. Uchunguzi wetu unaonesha
kuwa asilimia 70 ya fedha za mradi wa meremeta ziliishia kwenye Benki nchini Switzerland
kupitia nchi ya Mauritius.
Mheshimiwa Spika, Kampuni ya Meremeta ambayo
baadaye ilibadilishwa jina na kuitwa TanGold ilianzishwa kama mradi wa kutorosha mabilioni
ya fedha za nchi kwenda kwa uhusika mkubwa sana wa Serikali. Nawasilisha mezani kwako
barua kutoka Ofisi ya Rais Ikulu ya tarehe 20 Agosti 2001, yenye kumbukumbu nambari
SHC/M.100/4/A kwenda Benki ya Deutsche Bank tawi la Uingereza kuitambulisha Kampuni
ya Meremeta na Kampuni ya Nedcor Trade Services Limited ya Afrika ya Kusini ili ipewe
mkopo. Barua hiyo inatambulisha miradi miwili ya dhahabu (mgodi wa Tembo na Mgodi
wa Buhemba) kwamba ni miradi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. Baada
ya barua hii yaliyotokea ni mtandao mpana wa kuiba fedha za Tanzania kwenda Afrika
Kusini, baadaye Mauritius na kisha kuishia kwenye akaunti za watu binafsi nchini Switzerland
na visiwa vingine vya ukwepaji kodi (tax havens). Kufuatilia barua hii kutoka Ikulu,
mkopo wa dola za kimarekani milioni kumi zilipatikana. Hata hivyo Serikali ya Tanzania
kupitia Benki Kuu ya Tanzania iliilipa Benki ya NedBank jumla ya dola za Kimarekani
138 milioni, dola milioni kumi kati ya hizi zililipwa kupitia kampuni ya Deep Green
Finance.
Mheshimiwa Spika, Nilifanya uchunguzi binafsi kuhusu suala hili.
Nilijaribu kuwasiliana na Benki ya NedBank ili kuweza kupata uhakika wa watu waliofaidika
na uchotaji huu mkubwa na wa kihistoria wa fedha za umma. Ufuatiliaji huu umeendelea
vya kutosha ila haujafika mwisho Hata hivyo taarifa nilizokusanya hadi sasa zimeonyesha
hatari kubwa namna ambavyo watanzania wenzetu wenye mamlaka wanavyokwapua fedha za
umma kwa faida yao. Nyaraka zote za wizi na utoroshaji huu wa fedha na mawasiliano
yangu na watu wa Benki ya NedBank nitayawasilisha mbele ya Kamati ya Bunge ninayopendekeza
kuundwa ili kutazama suala hili.
Mheshimiwa Spika, Kuna masuala yanayohusu
usalama wa nchi kutokana na kashfa hii ambayo pia ningependa kuyaonyesha katika Kamati
ninayopendekeza kuundwa. Nyaraka hizo zinaonyesha silaha na aina za silaha zilizonunuliwa
na kutoka nchi gani na kwamba silaha hizo ziliishia wapi. Nimeona kwamba kuyasema
masuala haya waziwazi kunaweza kuhatarisha usalama wa nchi yetu. Hata hivyo masuala
haya ni lazima yafahamike ili hatua stahili ziweze kuchukuliwa dhidi ya watendaji
wa Serikali watakaokutwa na makosa.
Mheshimiwa Spika, Fedha zilizoibwa na
kutoroshwa kupitia kampuni ya Meremeta na kampuni ya Deep green ziliishia kwenye akaunti
za watu binafsi nje ya nchi. Hata hivyo mara baada ya kuundwa kwa kampuni ya TanGold,
jumla ya dola za kimarekani milioni kumi ziliwekwa kwenye akaunti ya Kampuni hiyo
katika Benki ya NBC, Corporate Branch. Nambari ya akaunti hiyo pia itatolewa katika
kamati ninayoomba kuunda kwa ajili ya uchunguzi wa kina.
Mheshimiwa Spika, Mwaka
2004, 2006 na 2007 Tanzania iligawa vitalu vya kutafuta mafuta na Gesi katika maeneo
mbalimbali nchini. Uchunguzi wetu unaonyesha kuwa zaidi ya dola za kimarekani milioni
56 zililipwa kwenye akaunti za watu binafsi nchini Switzerland kutoka kwenye kampuni
zilizoshinda zabuni ya kutafuta mafuta na gesi.
Mheshimiwa Spika, Uchunguzi
nilioufanya kwa msaada wa wachunguzi waliobobea kwenye masuala ya mifumo ya kifedha
ya Kimataifa umeniwezesha kupata nyaraka muhimu zinazoonyesha watu na namna walivyopata
fedha walizoweka katika akaunti zao nje ya Tanzania. Mheshimiwa Spika, mwaka 2004
na 2005 Mwanasiasa wa Afrika Kusini kutoka chama cha ANC bwana Tokyo Sexwale alitembelea
nchini katika ziara ya kibiashara. Alileta marafiki zake wawili na kuanzisha kampuni
iitwayo Ophir Energy Tanzania limited. Kampuni hii inamiliki vitalu 3 katika pwani
ya bahari ya Hindi blocks 1,3,4. Bwana Tokyo Sexwale alitambulishwa hapa nchini na
raia wa Kongo aitwaye Moto Mabanga. Hivi sasa bwana Moto Mabanga ameishitaki kampuni
ya Ophir Energy kwa kutotimiza masharti waliyokubaliana kuhusiana na kufanikisha kupatikana
kwa vitalu hivyo vya mafuta. Moto Mabanga ndio alikuwa ‘deal maker’wa kampuni hii
na ili kufanikisha hali hii alihonga sana wanasiasa na maafisa wa Serikali wanaohusika
na ugawaji wa Vitalu vya kutafuta Mafuta na Gesi. Wakati Ophir wanapewa vitalu hivi
sehemu ya hisa za kampuni hii ziligawiwa kwa baadhi ya watanzania ikionekana kuwa
ni hisa kwa ajili ya chama cha CCM. Hata hivyo uchunguzi wetu unaonyesha kuwa hisa
hizo zilikuwa ni za watu binafsi. Hivi sasa hisa zimeuzwa na fedha kufichwa katika
mabenki mbalimbali nje ya Tanzania. Kuna haja ya kufanya uchunguzi wa kina kuhusu
umiliki wa kampuni ya Ophir Energy wakati wanaingia nchini na mabadiliko ya umiliki
katika kipindi cha miaka minane iliyopita. Vile vile uchunguzi unapaswa kufanywa kwa
vitalu vyote vilivyogawiwa katika ya mwaka 2003 mpaka 2008 na umiliki wa Watanzania
katika makampuni yaliyopewa vitalu hivyo.
Mheshimiwa Spika, serikali yetu iagizwe
na Bunge lako tukufu kupata taarifa za kina kupitia njia za kiserikali na njia za
wachunguzi binafsi. Mimi kama Mbunge nilipofikia sasa nahitaji msaada wa Bunge kufanikisha
jambo hili. Nilipofikia sasa ni kutoa taarifa na nyakara zote nilizo nazo na watu
TAASISI zitakazo saidia kwa kamati teule ambayo Bunge litaunda kushughulikia suala
hili mahususi.
Baada ya maelezo hayo, naomba kuwasilisha,
HOJA BINAFSI
YA KABWE ZUBERI ZITTO (MB) KUHUSU KULITAKA BUNGE KUCHUNGUZA NA KUILEKEZA SERIKALI
KUCHUKUA HATUA DHIDI YA RAIA WA WATANZANIA WALIOFICHA FEDHA NA MALI HARAMU NJE YA
NCHI
[Inatolewa chini ya Kanuni ya 54(3)]
Mheshimiwa Spika, KWA KUWAkumekuwa
na uthibitisho kutoka Mamlaka za nchi ya Switzerland kwamba kuna raia wa Tanzania
wanamiliki fedha za kigeni katika Benki nchini na kwamba kuna kanuni na taratibu za
nchi zinazoendesha na kuongoza ufunguaji wa akaunti za fedha za kigeni nje ya Tanzania
kwa Watanzania wakazi (residents). Na kwamba kitendo kilichofanywa na wahusika kuweka
mabilioni ya fedha kwenye nchi za nje kinaweza kuwa ni kinyume na sheria ya “FOREIGN
EXCHANGE ACT, 1992”
NA KWA KUWA sheria hiyo kifungu cha (10) cha Sheria ya
Fedha za kigeni kinazuia utoroshaji wa fedha za kitanzania na isipokuwa kwa kibali
cha Gavana wa Benki Kuu tu, hakuna mtu yeyote atakaye ruhusiwa kusafirisha fedha nje
ya Tanzania. Na kinaeleza kuwa kwa msafiri anayekwenda nje ya nchi hatoruhusiwa kuondoa
na kiasi cha shilingi ambazo zinazidi dola za kimarekani hamsini. Vile vile kwa mujibu
wa Sheria hiyo kifungu cha 6 na 7 na waraka uliotolewa na Gavana wa Benki Kuu kwamba
Mtanzania yeyote mwenye kutaka kufungua akaunti kwenye mabenki nje ya Tanzania lazima
apate kibali cha Gavana.
NA KWA KUWA masharti hayo ya sheria yanaweza kuwa
yamekiukwa na wahusika kwa kuhifadhi fedha za kigeni katika mabenki ya nje,
NA
KWA KUWA ukiukwaji huo ni dhahiri kuwa fedha zilizowekwa kwenye mabenki ya nje kwa
kiasi kikubwa ni fedha ambazo hazikupatika kwa njia za halali na kwamba kuna uwezekano
wa ukwepaji mkubwa wa kodi,
NA KWA KUWA, nchi yetu imekuwa katika matatizo
makubwa ya fedha za kigeni, jambo ambalo limepelekea nchi kushusha thamani ya shilingi
ili kukabiliana na gharama za manunuzi ya bidhaa nje ya nchi,
NA KWA HIYO BASI,
ninaliomba Bunge hili liazimie: 1. Kwamba Bunge lako tukufu liunde Kamati Teule
kuchunguza Raia wa Tanzania wenye kumiliki fedha za kigeni na mali nje ya Tanzania.
Kamati Teule hiyo ifanye kazi zifuatazo: - Kuchunguza mfumo mzima wa utoroshaji
wa fedha na kufichwa nje ya nchi, - kuchunguza na kupembenua mali na fedha haramu
dhidi ya halali zinazomilikiwa na raia wa Tanzania katika taasisi za kifedha nje ya
Tanzania, - kuchunguza utaratibu mzima wa kugawa vitalu vya utafutaji mafuta na
gesi kati ya mwaka 2003 mpaka 2008, - kuchunguza mtiririko mzima wa utoroshaji
wa fedha kutoka Benki Kuu ya Tanzania kupitia Kampuni ya Meremeta (pia Triannex pty
ya Afrika Kusini na Deep Green Finance ltd) na kupendekeza hatua za kuchukua dhidi
ya wahusika wote wa utoroshaji wa fedha kwenda nje, - kuchunguza umiliki wa wa
watanzania kwenye kampuni zote zenye mikataba ya utafutaji wa Mafuta na Gesi hapa
nchini na namna umiliki huo umekuwa ukibadilika, mapato (proceeds) zilizotokana na
mabadiliko hayo ya umiliki na kama kodi stahili zimekuwa zikilipwa kutokana na kubadilika
kwa umiliki huo, - kuchunguza kwa kina mali za Watanzania wote waliowahi kushika
nafasi za Uwaziri Mkuu kati ya mwaka 2003 mpaka 2010, waliowahi kushika nafasi za
Uwaziri wa Nishati na Madini, Uwaziri wa Ulinzi, Ukuu wa Majeshi, Ukatibu Mkuu wa
wizara ya Nishati na Madini, Ukatibu Mkuu wa Wizara ya Ulinzi, Uanesheria Mkuu wa
Serikali, Ukamishna wa Nishati, Ukurugenzi Mkuu wa TPDC, Uenyekiti na Ujumbe wa Bodi
wa TPDC katika ya mwaka 2003 mpaka 2010.
2. Kwamba Serikali ilete muswada wa
Sheria Bungeni ifikapo Mkutano wa 11 wa Bunge kwamba itakuwa ni marufuku kwa Kiongozi
yeyote wa Umma au mume au mke wake au watoto wake kuwa na akaunti katika mabenki nje
ya nchi isipokuwa kwa sababu maalumu na kwa kibali rasmi kutoka kwa Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania.
3. Kwamba Serikali iwasiliane na Benki ya Dunia ili
kupitia Kitengo cha Assets Recovery Unit mabilioni ya Fedha na mali zisizoondosheka
zinazomilikiwa na Watanzania katika mabenki ya nchini Switzerland, Dubai, Mauritius
na visiwa na maeneo mengine yote ambapo hufichwa fedha na Mali ili kukwepa kodi na
kwamba mali hizo na mabilioni hayo yaliyopatikana kiharamu yarudishwe nchini mara
moja
4. Kwamba katika muswada tajwa hapo juu, Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania
aimarishiwe mamlaka ya kutoa kibali kwa Mtanzania yeyote anayetaka kufungua akaunti
ya Benki nje ya nchi na kwamba kila mwaka Gavana atatangaza kwenye Gazeti la Serikali
na magazeti yanayosomwa na wananchi wengi orodha ya Watanzania walioomba na walioruhusiwa
kuwa na akaunti ya Benki nje ya Tanzania.
5. Kwamba Watanzania wote wenye akaunti
za fedha nje waeleze wamezipataje na TAKUKURU wachukue hatua za kisheria dhidi ya
watu wote wenye kumiliki fedha na mali kinyume na mapato yao halali.
6. Kwamba
Serikali, katika mkutano wa Bunge wa 11 na baada ya Taarifa ya Kamati Teule ya Bunge
kuhusu Raia wa Tanzania wenye kumiliki fedha za kigeni kwneye mabenki na mali nje
ya Tanzania ilete taarifa ya hatua ilizochukua ili kuziba mianya ya utoroshaji wa
fedha nje ya Tanzania.
7. Kwamba Serikali katika Bajeti ya mwaka 2013/14 itaanzisha
kodi maalumu ‘financial transaction tax’ ya angalau asilimia 0.5 ya thamani ya ‘transaction’
ili kuweza kuwa na rekodi za uhakika za fedha ndani na zinazotoka nje ya nchi.
Mheshimiwa
Spika,
Naomba kutoa hoja, ……………………. KABWE ZUBERI ZITTO(MB) JIMBO LA
UCHAGUZI-KIGOMA KASKAZINI 08.11.2012