2012-11-15 12:16:25

Kuna mafanikio makubwa yaliyokwisha kupatikana katika majadiliano ya kiekumene tangu baada ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican


Kardinali Kurt Koch, Rais wa Baraza la Kipapa la kuhamasisha umoja wa Wakristo, anasema kuwa maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya, ilikuwa ni fursa ya pekee kuweza kukutana na wawakilishi wa Mabaraza ya Maaskofu Katoliki kutoka sehemu mbali mbali za dunia, wote kwa pamoja wakipania kwanza kabisa: kusali, kutafakari pamoja na kushirikishana uzoefu, mang’amuzi, matatizo, changamoto mbali mbali zinazojitokeza katika maeneo yao, ili kuandaa mwongozo utakaoliwezesha Kanisa kujikita katika Uinjilishaji kama njia ya kutangaza Imani yake.

Ni matatizo na changamoto ambazo kila nchi inapoyaangalia inadhani kwamba ni yake, lakini kuna uhusiano mkubwa na kile kinachoendelea sehemu mbali mbali za dunia.

Anabainisha kwamba, katika kipindi cha miaka hamsini tangu maadhimisho ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, kumekuwepo na maendeleo makubwa katika majadiliano ya kiekumene, hususan katika lile Tamko la pamoja kuhusu “Mafundisho juu ya kuhesabiwa haki, lililotolewa Mwezi Agosti 1999, kati ya Kanisa la Kiluteri na Kanisa Katoliki. Kuna haja ya kuendelea kukazia majadiliano ya kiekumene hasa na Madhehebu mbali mbali ya Kikristo, ili kuwa ni uelewa na mtazamo unaolielewa Kanisa na Wakatoliki katika mapana yake. Kwa pamoja wanapaswa kutambua jambo ambalo ni kiini cha Kanisa.

Majadiliano ya kiekumene yanaendelea kujionesha hata miongoni mwa waamini wa Kanisa Anglikani, ambao kutokana na msukumo wao pamoja na busara ya kichungaji iliyooneshwa kwa namna ya pekee na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, baadhi yao wamekubaliwa kujiunga na Kanisa Katoliki, huku wakiendeleza Ibadan a tamaduni za Kanisa Anglikani.

Majadiliano ya kiekumene yanaendelea pia miongoni mwa waamini wa Kanisa la Kiothodox, lakini bado kuna haja ya kuelewa dhana ya Uongozi wa Sinodi na Mfumo wa Uongozi ndani ya Kanisa hili.

Kardinali Kurt Kocha anabainisha kwamba, kuibuka na kukomaa kwa tabia na dhana ya ukanimungu ni matunda yaliyojitokeza kwa namna ya pekee katika kipindi cha Karne ya kumi na sita, ambako Makanisa yalipigana na kushambuliana kwa misingi ya Imani, kiasi cha kuwakatisha tamaa wale waliokuwa wanapenda kujiunga na Ukristo, kwani kama Ukristo ulikuwa unajitambulisha kwa njia ya “mtutu wa bunduki” basi kulikuwa hakuna haja ya kujiunga na Kanisa, ambalo kimsingi lilipaswa kuwa ni mtetezi na msimamizi wa misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kweli.

Kumbe, hali ambayo mwanadamu katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia amefikia ni matunda ya mabadiliko ya kihistoria na vipaumbele vya maisha ya mwanadamu, kiasi cha kumfanya kutoona umuhimu wa uwepo wa Mungu katika maisha yake, hitimisho ambalo ni hatari kabisa, kwani bila uwepo wa Mungu, mwanadamu si mali kitu, utu na heshima yake viko hatarini. Hii ndiyo changamoto kubwa katika dhamana ya Uinjilishaji Mpya.

Kardinali Kurt Kocha anasema kwamba, Maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, uwe ni mwendelezo wa mabadiliko ya dhati yaliyopaniwa na Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, hakuna mpasuko katika utekelezaji wa mabadiliko ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican. Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, wakati wa Maadhimisho ya Siku kuu ya Noeli, kunako mwaka 2005 alibainisha mwendelezo wa Mabadiliko yaliyofanywa na Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.