2012-11-15 08:45:46

Kumbu kumbu ya miaka 10 tangu Mwenyeheri Yohane Paulo II alipotembelea Bunge la Italia


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Jumatano, tarehe 14 Novemba 2012 amewatumia ujumbe wa matashi mema viongozi na wabunge wa Seneti ya Italia wakati wa maadhimisho ya miaka kumi tangu Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili alipotembelea bungeni hapo tarehe 14 Novemba 2002. Hili lilikuwa ni tukio muhimu sana katika harakati za kuimarisha uhusiano kati ya Vatican na Serikali ya Italia, licha afya ya Baba Mtakatifu Yohane Paulo wa pili, wakati ule kuwa imeanza kudhohofu. Wabunge walimpokea kwa heshima na taadhima na kwamba, hotuba aliyoitoa inaacha chapa ya kudumu katika mioyo na akili za watu.

Ujumbe wa Baba Mtakatifu umeandikwa kwa niaba yake na kardinali Tarcisio Bertone, Katibu mkuu wa Vatican na kusomwa na Askofu mkuu Angelo Becciu, Katibu mkuu msaidizi wa Vatican.

Miaka kumi imepita, lakini katika hotuba yake, Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili alikuwa amewachangamotisha Wabunge nchini Italia, kuhakikisha kwamba, wanajichotea utajiri mkubwa unaofumbatwa katika Mapokeo ya Kikristo, ambayo kwa namna ya pekee, yanawapatia utambulisho wao: kijamii na kitamaduni pamoja na kuendeleza dhamana yake katika Umoja wa Ulaya na Ulimwengu kwa ujumla.

Aliwataka kwa namna ya pekee kabisa, kutumia urithi wao wa maisha ya kiroho na kimaadili katika kutafuta mafao ya wengi na hasa zaidi wanapokabiliana na changamoto katika utekelezaji wa majukumu yao, ili kuleta mabadiliko yanayotarajiwa na wananchi.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anasema kwamba, kuna haja ya kuendeleza ushirikiano kati ya Vatican na Italia; kati ya Kanisa na Serikali, ili Italia iweze kutekeleza wajibu na dhamana yake kwa kuenzi familia mahali pa elimu na makuzi ya kijamii; kila mwananchi akijitahidi kutekeleza wajibu wake ndani ya Jamii. Baba Mtakatifu anawahakikishia uwepo wake kwa njia ya sala na sadaka kwa ajili ya ufanisi na tija katika huduma kwa wananchi wa Italia.

Askofu mkuu Angelo Becciu anasema kuna uhusiano mkubwa kati ya siasa na maadili, kwani demokrasia isiyozingatia tunu msingi za maisha ya kimaadili na utu wema ni hatari kwa ustawi na maendeleo ya nchi; adui mkubwa katika maisha ya kiroho na kisiasa nyakati hizi ni utovu wa nidhamu, ukosefu wa maadili pamoja na watu kupenda kujikita katika mawazo mepesi mepesi.

Kwa upande wake, Kardinali Angelo Bagnasco, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia anabainisha kwamba, maadili na utu wema hayana budi kuwa ni dira na mwongozo katika utungaji wa sheria ambazo kimsingi zinapaswa kuzingatia haki. Ili kufikia lengo hili, wanasiasa wanapaswa kweli kuwa na dhamiri nyofu inayoongozwa na sheria maadili. Ni wajibu wa wanasiasa kulinda na kuzitegemeza familia, hasa katika harakati za kuwapatia watoto wao elimu bora.







All the contents on this site are copyrighted ©.