Vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanakutana Kigali, Rwanda ili kufanya hija
ya matumaini, ili kuleta mabadiliko katika sura ya nchi!
Vijana wa Jumuiya ya Taize iliyoanzishwa na Fra Roger kutoka sehemu mbali mbali za
Bara la Afrika, kuanzia tarehe 14 hadi 18 Novemba 2012 wanashiriki katika mkutano
ambao ni kielelezo cha hija ya matumaini duniani.
Mkutano huu pia unawashirikisha
baadhi ya wajumbe kutoka Ulaya, Amerika na Asia, lengo la vijana hawa ni kumwadhimisha
Kristo, wakifanya hija ya pamoja kwenye chechemi ya matumaini inayopania kuleta mabadiliko
katika maisha na utume wa Kanisa pamoja na Jamii kwa ujumla.
Ni muda muafaka
kwa vijana kutoka Eneo la Maziwa Makuu kuweza kuishi kwa pamoja, katika hali ya amani,
upendo na mshikamano wa kweli; wakishirikishana mang'amuzi na vipaumbele vya maisha
ya Kikristo, katika uwanja wa kitaifa na kimataifa; daima wakijitahidi kuonesha dhamana
na wajibu wao ndani ya Kanisa, katika mchakato wa kujenga na kuimaarisha matumaini
na amani miongoni mwa waamini wa dini zao.
Vijana kutoka sehemu mbali mbali
za dunia wanakutanika nchini Rwanda, ambako Mwaka 1994 kulitokea mauaji ya kimbari,
zaidi ya watu laki nane walipoteza maisha yao kutokana na chuki za kikabila. Tangu
wakati huo, juhudi za pamoja zinaendelea kufanyika kwa kujikita katika mchakato wa
msamaha na upatanisho wa kweli, kila mwananchi akijitahidi kutumia vipaji na karama
alizokirimiwa na Mwenyezi Mungu, ili kuijenga nchi yake akipania kutafuta mafao ya
wengi, kulinda na kusimama kidete kutetea haki msingi za binadamu.
Vijana
wanasema wako nchini Rwanda si kwa ajili ya kuwasuta Wanyarwanda, wala kujadiliana
yale yaliyopita, bali kujenga utamaduni wa kusikiliza na kuimarisha utashi wa vijana
katika harakati za kuboresha maisha yao kiroho na kimwili, wakiheshimiana na kuthaminiana
kama watoto walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.
Vijana wanafanya tafakari
ya kina kuhusu vyanzo vya imani yao, Fumbo la Mateso, Kifo na Ufufuko wa Kristo, muhtasari
wa imani ambayo inawaunganisha vijana hawa kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Vijana
wanasema, kwa pamoja wanapenda kuonja upendo mkamilifu wa Kristo, ambao una nguvu
zaidi kuliko kifo na ubaya wa binadamu.
Vijana wanapenda kukutana na kuzungumza
na wale ambao wameshuhudia utamaduni wa kifo ukigusa undani wa maisha ya Wananchi
wa Rwanda; kuwasikiliza wale ambao kimsingi wamesimama imara kulinda na kutetea haki,
amani na mshikamano wa kitaifa; kushirikiana kwa karibu zaidi na wote wanaoendeleza
kuhimiza ukweli, upatanisho na msamaha, unaopata chimbuko lake katika toba na wongofu
wa ndani.
Kwa hakika wanasema viongozi wa Jumuiya ya Taizè, vijana wanataka
kusoma Injili ya Upendo na Mshikamano, ulioneshwa kwa namna ya pekee kwa njia ya Msalaba
wa Kristo pale mlimani Kalvari.