2012-11-14 15:21:08

Kwa ushuhuda wa Imani katika matendo, waongozeni wengine kumfahamu na kumpenda Mwenyezi Mungu aliyejifunua kwa njia ya Yesu Kristo


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Jumatano tarehe 14 Novemba 2012, katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, ameendelea kutafakari kwa kina kuhusu hamu ya kukutana na Mwenyezi Mungu ambayo inajikita katika undani wa moyo wa mwanadamu. Kwa njia ya neema yake, Mwenyezi Mungu anaandamana na mwanadamu katika harakari za kumfahamu ili hatimaye, aweze kujipatia furaha ya kweli katika maisha yake.

Baba Mtakatifu anasema, leo hii katika ulimwengu mamboleo, inasikitisha kuona kwamba, Imani inaonekana kuwa ni jambo gumu sana, kiasi cha mwanadamu kufikiri na kudhani kwamba, anaweza kuishi bila ya kumtegemea Mwenyezi Mungu. Lakini ikumbukwe kwamba, Mwenyezi Mungu anapoondolewa katika maisha ya mwanadamu, anakumbana na utupu, kwani utu na heshima ya mwanadamu ni matokeo ya kuumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, mwaliko wa kujishikamanisha na Mungu.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini popote pale walipo kuhakikisha kwamba, wanatoa sababu makini juu ya Imani na Matumaini yao. Sababu hizi zinajikita kwa namna ya pekee katika kazi ya uumbaji inayoonesha utukufu wa Mungu Muumbaji; hamu ya maisha ya uzima wa milele ambayo imejificha katika undani wa moyo wa mwanadamu, hamu ambayo inapata kitulizo chake mbele ya Mwenyezi Mungu peke yake; na katika imani ambayo inaangaza na kuleta mabadiliko katika maisha ya mwanadamu, kwa kuungana na Kristo kila siku ya maisha yao.

Baba Mtakatifu anasema, kwa njia ya ushuhuda wa Imani katika matendo, waamini wanaweza kuwaongoza wengine kumfahamu na kumpenda Mwenyezi Mungu aliyejifunua kwa njia ya Yesu Kristo Mkombozi wa dunia.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, ametambua uwepo wa wajumbe wanaoshiriki katika mkutano wa ishirini na saba kimataifa amboa umeandaliwa na Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa ajili ya wafanyakazi katika sekta ya afya. Amewashukuru pia wanakwaya wa Kwaya ya Kanisa kuu la Westeminster kutoka Uingereza bila kuwasahau mahujaji kutoka sehemu mbali mbali za dunia.

Ametambua uwepo wa washiriki wa kongamano lililoandaliwa na Shirikisho la Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki Kimataifa, Caritas Internationalis pamoja na washiriki wa kozi maalum iliyoandaliwa na Chuo Kikuu cha Kipapa cha Wasalesiani. Anawakumbusha kwamba, hija yao kwenye Makao Makuu ya Mtakatifu Petro, yaamshe ndani mwao ari na mwamko wa toba ili kushiriki kwa dhati dhamana ya Uinjilishaji Mpya.

Mwishoni, Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, amewatakia kila neema na baraka wakati Mama Kanisa anapofanya kumbu kumbu ya Mtakatifu Alberti Mkuu, Msimamizi wa wachongaji na wanasayansi asilia, inayoadhimishwa kila mwaka ifikapo tarehe 15 Novemba







All the contents on this site are copyrighted ©.