2012-11-13 09:38:08

Mwanadamu anapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza katika masuala ya ulinzi na usalama


Askofu mkuu Silvano Maria Tomasi, Mwakilishi wa kudumu wa Vatican kwenye Ofisi za Umoja wa Mataifa zilizoko mjini Geneva, hivi karibuni ameshiriki katika mkutano wa kimataifa uliokuwa unajadili kuhusu silaha zenye uwezo wa kuleta maafa na madhara makubwa kwa binadamu.

Ujumbe wa Vatican kwenye mkutano huu, umeonesha hofu kubwa kutokana na madhara yanayoweza kusababishwa na silaha hizi kwa kuzingatia usalama wa kitaifa. Kuna milipuko mikubwa ya silaha ambayo haidhibitiwi wala kutolewa taarifa na wakati mwingine, silaha hizi zinaangukia mikononi mwa magaidi na hatari yake inakuwa ni kubwa zaidi, kiasi hata cha kugusa kinzani na migogoro ya kisiasa inayoendelea kufuka moshi sehemu mbali mbali za dunia. Umakini wa itifaki ya tano na utekelezaji wake, iko mashakani, ingawa hili lingepaswa kuwa ni lengo la Jumuiya ya Kimataifa.

Askofu mkuu Tomasi anaendelea kusema kwamba, kuna haja kwa Serikali husika kuweka takwimu sahihi za matumizi ya silaha zenye madhara makubwa pamoja na kushirikisha taarifa zake mara baada ya kinzani na migogoro kumalizika, kwani kushindwa kutekeleza wajibu huu, madhara yake ni makubwa kwa binadamu. Kutakuwa na mauaji ya watu wasiokuwa na hatia, madhara makubwa katika uchumi na maisha ya Jamii husika pamoja na kudumaza maendeleo ya watu.

Utekelezaji wa awamu ya tatu hauna budi kuanza mara moja anasema Askofu mkuu Tomasi, ili kufahamu fika kiasi cha silaha kilichopo pamoja na kuanza harakati za kusafisha maeneo ambayo kimsingi yameathirika kutokana na uwepo wa silaha hizi za mahangamizi, kwani utekelezaji huu, ni sehemu ya uwajibikaji kimaadili.

Jumuiya ya Kimataifa haina budi kuendeleza ushirikiano huu, ili kumwilisha utifaki katika mataifa mengi zaidi duniani, ingawa kimsingi utekelezaji wake ni mgumu, lakini hakuna haja ya kukata tamaa. Ujumbe wa Vatican unaungana na Chama cha Msalaba Mwekundu, Mashirika Yasiyo ya Kiserikali na wadau wengine kuonesha masikitiko yake makuu kutokana na nchi nyingi kushindwa kuridhia itifaki hii, ambayo inalenga kulinda na kudumisha utu na heshima ya binadamu, kwa kuzingatia sheria ya kimataifa.

Mwanadamu anapaswa kuwa ni kipaumbele cha kwanza katika masuala ya ulinzi na usalama na kwamba, raia wapewe ulinzi wa kutosha. Inasikitisha kuona kwamba, katika kinzani na vita inayoendelea kwa sasa sehemu mbali mbali za dunia, wanaopoteza maisha yao kwa wingi ni raia wasiokuwa na hatia, hali inayoonesha kwamba, kimsingi hakuna utii wa sheria za kimataifa.

Ni wajibu wa Jumuiya ya Kimataifa kuhakikisha kwamba, inatoa ulinzi wa kutosha kwa raia na mali zao dhidi ya milipuko ya silaha wakati na mara baada ya vita. Raia wana haki ya kuishi katika mazingira salama, yenye amani na utulivu bila kuwa na wasi wasi wa vitisho vya milipuko ya silaha za mahangamizi.







All the contents on this site are copyrighted ©.