Mfuko wa Mo Ibrahim wamtunukia Tuzo Maalum Askofu mkuu Desmond Tutu kwa kusimama kidete
kupinga utawala wa ubaguzi wa rangi Afrika ya Kusini
Askofu mkuu Desmond Tutu wa Kanisa Anglikani, ni kati ya viongozi maarufu sana nchini
Afrika ya Kusini, waliosimama kidete kupinga utawala wa ubaguzi wa rangi Afrika ya
Kusini na matokeo ya juhudi hizi yanaonekana kwa uhuru wa watu wa Afrika ya Kusini
ambao kwa sasa wanaendelea kucharuka katika mikakati ya maendeleo endelevu, wakishikamana
na kujisikia wamoja na kwamba, tofauti zao za rangi ni utajiri mkubwa wanaopaswa kuupokea
kwa heshima na taadhima.
Mfuko wa Mo Ibrahim kwa kutambua mchango wa Askofu
mkuu Desmond Tutu, mapema juma hili wamemtunuku Tuzo Maalum kutokana na mchango wake
wa kusimamia ukweli, tuzo ambalo linaambatana na kitita cha Dolla za Kimarekani Millioni
moja. Askofu mkuu Tutu, kwa miaka mingi tangu ujana wake, alijitoa kimaso maso kutetea:
haki msingi za binadamu, utu, heshima, na amani kwa watu wote waliokuwa wanakandamizwa
na utawala dhalimu wa ubaguzi wa rangi Afrika ya Kusini.
Askofu mkuu Desmond
Tutu ni kiongozi ambaye hakuogopa kusema ukweli ambao wakati mwingine unauma kweli
kweli. Wakati wa kupokea tuzo hii maalum, Askofu Tutu amesema kwamba, mashujaa wanaopaswa
kutuzwa ni wananchi wa Afrika ya Kusini, waliomuunga mkono wakati wa kampeni yake
dhidi ya ubaguzi wa rangi Afrika ya Kusini.
Anawakumbuka wapigania uhuru wote
waliomtia shime kusonga mbele pasi na kuogopa, wazee walioshirikiana naye kusimamia
ukweli na haki msingi za binadamu; wanawake walionesha kwa namna ya pekee tunu bora
za kimama bila kumsahau "asali wa moyo wake Mama Leah" ambaye amemwezesha kupata mafanikio
aliyo nayo wakati huu.
Mwishoni, Askofu mkuu Desmond Tutu amewakumbusha vijana
sehemu mbali mbali za dunia kwamba, ni watu wenye ndoto ya kupata dunia iliyo bora
zaidi kwa kuishi, mahali ambapo umaskini utapewa kisogo, ni vijana hawa hawa ambao
wako mstari wa mbele kuleta mabadiliko katika mapambazuko mapya yanayoendelea kwenye
nchi za Kiarabu. Kwa hakika, vijana ni tumaini la wazee!