Majiundo makini katika taalimungu na tamaduni yataiwezesha mihimili ya Injili kumtangaza
Kristo kwa ujasiri mkubwa zaidi
Kardinali Fernando Filoni, Rais wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu, mapema
juma hili amefungua Mwaka wa Masomo 2012 -2013, kwa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Kipapa
cha Urbaniana, kilichoko mjini Roma, kwa Ibada ya Misa Takatifu ili kuomba mapaji
ya Roho Mtakatifu.
Wakati wa mahubiri yake, amekumbusha kwamba, Baraza la
Kipapa la Uinjilishaji wa watu lipo kwa sababu linapania kukoleza juhudi za kutangaza
Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia, hasa zaidi kwa kuyawezesha Makanisa machanga,
katika malezi na majiundo makini ya mihimili ya uenezaji Injili katika masomo ya falsafa,
taalimungu na kitamaduni, ili vijana wanapohitimu masomo yao wawe wameiva barabara.
Kardinali
Filoni ameelezea kwamba, majiundo makini katika tamaduni yanawasaidia wanafunzi hao
kuweza kuifahamu historia ya kazi ya ukombozi kwa mataifa yote na kwamba, utume wao
kama Mapadre, Watawa na Waamini walei ni huduma kwa Mungu, Kanisa na Jirani.
Mwaka
wa Imani uwe ni kikolezo kwa wanafunzi hao kujiandaa vyema kutekeleza wajibu wao ndani
ya Kanisa kwa kuunganisha uelewa wao kuhusu Neno wa Mungu aliyefanyika mwili na historia
ya maisha ya mwanadamu mintarafu Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, kwa kuendelea kusoma
alama za nyakati sanjari na jitihada za utamadunisho, ili Injili ya Kristo iweze kuota
mizizi katika maisha ya mwamini.
Majiundo makini katika taalimungu na tamaduni
ni muhimu sana anasema Kardinali Filoni katika jitihada za Mama Kanisa kutangaza Habari
Njema ya Wokovu kati ya watu wa Mataifa. Hii ni huduma nyeti kwa Makanisa mahalia,
kwani kama mihimili ya Uinjilishaji wanatumwa na Mama Kanisa kuhubiri, lakini zaidi
kutolea ushuhuda wa imani yao kwa njia ya maisha adili na utu wema, kwa kutambua kwamba,
wanaendeleza ile kazi ya ukombozi iliyoanzishwa na Kristo mwenyewe yapata miaka elfu
mbili iliyopita, katika ulimwengu ambao una mwingiliano mkubwa wa watu kutoka katika
kila lugha, kabila na jamaa.
Mwaka wa Imani uwe ni fursa kwa Jumuiya ya Chuo
Kikuu cha Urbaniana kuweza kujishikamanisha na Kristo pamoja na Kanisa lake. Lengo
la masomo yao liwe ni kumfahamu vyema Kristo na ujumbe wake, tayari kujitoa kimasomaso
kumhubiri hadi miisho ya dunia. Umissionari na dhamana ya kuinjilisha inapata chimbuko
lake katika Imani inayoungamwa, inayomwilishwa katika Sakramenti za Kanisa, imani
ambayo kimsingi ni dira na mwongozo wa maisha adili yanayopata chimbuko lake katika
Amri za Mungu, tayari kuitolea ushuhuda katika sala.